Rafed English

Khadija-tul-Kubra

Khadija-tul-Kubra by : Sayyed A. A. Razwy Khadija, mke wa kwanza wa Muhammad Mustafa, Mjumbe wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w.) na Muumini wa kwanza, ambaye alikuwa na hisia za mtu asiye wa kawaida kabisa. Aliwajibika sana katika histo­ria ya uchanga wa Uislamu. Alikuwa yeye pamoja na Abu Talib, mmoja miongoni mwa watu wawili wafadhili wakubwa kabisa wa Uislamu na Waislamu. Wakati ambapo Uislamu ulikuwa kwenye shinikizo la utekwaji wa kudumu; na ulikuwa umezingirwa kwa kipin­di cha mfululizo wa miaka mitatu, aliudhamini kwa kujitolea kwake mhanga wa kushangaza sana.



Uthabiti wake usiobadilika, ushupavu wake, kuwa na uwezo wa kupeleka fikra mbali ya siku za usoni, na uthabiti wa imani yake kwa Mwenyezi Mungu, na kwa ujumbe wa Muhammad Mustafa - Mjumbe wake wa mwisho na mkubwa kuliko wote - haya mambo yalikuwa lazima yawepo kwani humo ndimo Uislamu uliegemea kwa kipindi cha miaka kumi ya mwanzo wake.

Kwa sababu zisizoeleweka, nafasi ya Khadija - ambayo ndiyo ilikuwa kiini cha kujenga hatima ya Uislamu- haijatambuliwa ipasavyo, kutoka kwa waandishi wengi wa wasifu na wanahistoria wa Kiislamu. Utambulisho kama huo ambao wameutoa, ni wa majaribio tu na bila uangalifu. Kwa kadiri ya ninavyo elewa na imani yangu mimi, wasifu halisi na sahihi wa Khadija, bado haujachapishwa. Huu ni upungufu mkubwa wa kusikitisha kwenye mvuto wa maandiko ya Uislamu, husu­san wakati ambapo katika nchi za Magharibi kuna mwamko mkubwa wa imani ya Uislamu, na katika simulizi zinazohusiana na viongozi wake katika siku zake za mwanzo.

Maandishi yaliyopo hadi leo juu ya maisha ya Khadija katika vyanzo mbalimbali ni machache na vipandepande. Hata haya maandishi machache na vipande pande sio salama kutokana na maelezo yasiy­obadilika au tafsiri potofu ya historia. Mwandishi wa wasifu au mwana historia, lazima alete hali ya msisimko ya kuelewa Uislamu sahihi, na lazima afanye makadirio ya haki ya majukumu ya watu wale ambao wameitengeneza historia yake.

Khadija ni mmoja wa watu waliokuwa na uwezo mkubwa na muhimu katika historia yote ya Uislamu. Haiwezekani kuzungumzia historia ya Uislamu bila kuyataja mambo aliyoyafanya kama mchango wake uliofanikisha Uislamu kuendelea kuwepo, kuimarika, na hatimaye kupata ushindi.

Uislamu una deni lisilolipika kwa Khadija. Kwa hiyo, ninaamini kwam­ba kuchapishwa kwa wasifu wa Khadija - unaoakisi moyo wa kisayansi na kanuni za kisayansi -ambazo wakati fulani niliziona kuwa za muhimu, sasa zinawakabili waandishi wa wasifu na wana historia wa Kiislamu kama sharti la ziada.

Sababu nyingine kwa nini inawalazimu Waislamu wote kupata fursa ya kuijua historia ya maisha ya Khadija, ni kwamba, kama alivyo mumewe, Muhammad Mustafa (s.a.w.w.) yeye pia ni alama ya umoja wa umma wake. Yeye (Khadija) ni alama ambayo hulea umoja wa umma wa Waislamu.

Juhudi imefanywa kwenye kitabu hiki kuweka pamoja maandishi yote yale juu ya maisha ya Khadija, ambayo yalipatikana katika vyanzo vingi vilivyotawanyika huku na huko.

Lakini, hili ni juhudi ambayo lazima likubaliwe kwamba haina matumaini ya kutoshelezea. Huelekeza kwenye mukhtasari tu-ambao utakuwa ni wa kusomwa tu. kwa ajili ya rejea, mpaka hapo wakati utakapokuwa ambako maandiko sahihi zaidi juu ya somo hili yatakapo patikana.

Hata hivyo, ni muhimu kwa Waislamu wote, hususan wanawake wa Kiislamu, wajue historia ya maisha ya Khadija na jinsi alivyotumikia Uislamu. Aliunganisha nafsi yake na Uislamu kwa ustadi wa hali ya juu sana hivyo kwamba Khadija alikuwa moyo na kiini cha Uislamu.

Kwa maana halisi, Khadija aliishi na kufa kwa ajili ya Uislamu.

Kama wanawake wa Kiislamu wanatafuta furaha hapa duniani na wokovu baada ya kufa, lazima waishi kwa kuiga maisha ya utakatifu wa Khadija. Yeye ni kiongozi wa siri ya kufuzu kupata radhi ya Mwenyezi Mungu; na yeye ndiye mwenye ufunguo utakao wafungulia wao milan­go ya kufuzu katika sehemu mbili, duniani na Akhera. Angefurahi kugawana nao 'siri' hii, kama watataka kujua siri hiyo ni nini, na atafu­rahi kuwapa 'ufunguo' huo, kama watautafuta kutoka kwake. Mwenyezi Mungu na amrehemu Khadija na familia yake.
Kitabu kilichoko mikononi mwako, ni tarjuma ya kitabu cha Kiingereza, kwa jina la"Khadija-tul-Kubra) kilichandikwa na Mwanachuoni mwanahistoria na mtafiti, Sayyed A. A. Razwy

Bibi Khadija alikuwa ndiye mke wa kwanza wa Mtukufu Mtume. Bibi huyu alikuwa tajiri miongomi mwa matajiri wakubwa wa Makka. Mtume alikuwa na miaka 25 alipomuoa bibi huyu, aliopofikisha miaka 40, alitoa tangazo la kwanza la utume wake, mtu wa kwamza kuamini utume wake alikuwa ni bibi Khadija, na hivyo kuamini Upweke (tawhid) wa Allah swt. Na kuwa Mwislamu wa kwanza ulimwenguni.

Waabudu masanamu wa Makka hawakufaurahishwa na tangazo hili, ukazuka uadui mkubwa sana kati ya Mtukufu Mtume na waabudu masanamu hawa. Kutokana na hali hii ilibidi Khadija atumie utajiri wake wote kuuhami Uislamu chini ya hifadhi kubwa ya ami yake Mtume, Abu Talib.

Mchango wa bibi huyu ni mkubwa sana katika Uislamu, lakini bahati mbaya yeye na Bwana Abu Talib wamekuwa ni madhulumu wa historia ya Uislamu. Si wanahistoria Mustashirik tu, bali hata wanahistoria wa Kiislamu wamekwepa kuandika wasifu wake kwa ukamilifu kama ambavyo wamekwepa kuandika kwa ukamilifu wasifu wa Bwana Abu Talib na kumsingizia ukafiri.

Katika kitabu hiki mwandishi ameandika angalau kwa kiasi cha kurid­hisha wasifu wa Bibi Khadija. Wasifu huu umeanzia kabla ya kuolewa na Mtukufu Mtume na baada ya kuolewa naye. Na mwandishi ameji­tahidi kuandika matukio muhumi yanayohusiana na bibi huyu, kwa kutumia vyanzo sahihi vya Kiislamu.

Kutokana na umuhimu wa maudhui ya kitabu hiki, tumeona tukutoe kwa lugha ya Kiswahili ili kizidishe mwanga wa elimu kwa Waislamu wazungumzaji wa Kiswahili.

Na hili ndilo lengo kubwa la Taasisi yetu ya 'Al-Itrah Foundation' katika kuwahudumia Waislamu, hususan wazungumzaji wa Kiswahili.

Tunamshukuru Ndugu yetu al-Akhy Salman Y. Shou kwa kukubali jukumu hili la kukifanyia tarjuma kitabu hiki. Vile vile tunawashukuru wale wote walioshiriki kwa njia moja au nyingine hadi kufanikisha kuchapishwa kwa kitabu hiki.

Mchapishaji:

Al-Itrah Foundation
S. L. P. 19701
Dar-es-salaam.
Mnamo Karne ya Sita A.D. Makka ilikuwa soko muhimu Arabuni. Mji huu ulikuwa kituo cha kimataifa cha biashara na uchuuzi. Mizigo kuto­ka India yenye bidhaa kama viungo, matunda, nafaka, vyombo vya ufinyanzi na nguo vilikuwa vikiteremshwa kwenye bandari za Yemen na kutoka hapo bidhaa hizo zilibebwa pamoja na zile za Arabu ya Kusini, kama vile kahawa, dawa, manukato na mafuta mazuri kwa kutumia ngamia kwenda Makka, na kutoka hapo kuendelea Syria hadi nchi zili­zozunguka bahari ya kati.

Makkah yenyewe ilikuwa kituo cha misafara mingi ya "udi na ubani" ya Arabuni na "viungo" vya India. Misafara mingine ilipitia Makka na Yathrib wakati inaelekea kaskazini ambako iliungana na misafara ya njia kubwa ya biashara ya hariri toka China.

Misafara kutoka kaskazini, pia ilisimama Makka. Ngamia na farasi wal­ibadilishwa hapo na mahitaji kujazwa tena hapo na halafu misafara huendelea hadi kwenye bandari za kusini ya rasi ya Bahari ya Arabuni.

Aidha, Makka ilikuwa kituo cha kubadilishana mali na bidhaa kwa ajili ya makabila ya Kiarabu yasiyo hamahama na yale yanayo hamahama; na ilikuwa sehemu ya kugawa bidhaa za kilimo na zilizotengenezwa na kupelekwa katikati ya Hijaz.

Makabila hayo yalikuja kutoka mbali katikati ya Arabuni na hata Arabia ya mashariki kwa madhumuni ya kununua bidhaa hizo ambazo zilikuwa hazipatikani nchini kwao. Sehemu kubwa ya biashara hii ya maingiliano ya makabila ilifanyika Makka kwa mfumo wa kubadilishana mali kwa mali.

Makuraishi wa Makka walikuwa kabila muhimu sana kutoka Magharibi ya Arabuni. Wote walikuwa wafanyabiashara wakubwa. Kwa kufanik­isha usafirishaji wa hariri kutoka China, bidhaa kutoka Afrika Mashariki na vitu vya thamani kutoka India - Makuraish walitawala biashara kati ya ustaarabu wa Mashariki na ule wa nchi za Bahari ya Mediterania. Ni dhahiri kwamba sehemu kubwa ya biashara hii ilikuwa ya bidhaa za anasa, lakini bidhaa za kawaida pia zilikuwepo kwenye biashara, kama vile nguo za rangi za zambarau, majora ya nguo, nguo zisizowekwa urembo wa kufuma na zile ambazo ziliwekewa nakshi ya dhahabu, zafarani, melimeli, majoho, mablanketi, mishipi, manukato ya mgando, mvinyo na ngano.

Kwa jinsi hii, uzalishaji, uuzaji, ubadilishaji na usambazaji wa bidhaa, kuliwafanya Makuraishi kuwa matajiri. Lakini palikuwepo na kitu kingine kilichowafanya kuwa matajiri. Al-Kaaba na Jiwe lake Jeusi lilikuwa mashuhuri, vilijengwa mjini Makka. Waarabu walikwenda Makka kuhiji na kuitembelea Al- Kaaba. Kwao Makka ilikuwa takatifu kama vile Jerusalem ilivyokuwa kwa Wayahudi na Wakristo.

Al-Kaaba ilikuwa hekalu kubwa la miungu wa masanamu waliomiliki­wa na koo za makabila mbalimbali ya Kiarabu. Mahujaji walileta sada­ka nyingi na zisizo za kawaida kwa ajili ya kuwafurahisha wale miun­gu-sanamu waliowaabudu. Mahujaji waliporudi makwao, makuhani wa hekalu walichukuwa sadaka zote kuwa mali yao. Misafara ya hija ilikuwa njia moja yenye kuwaingizia mali nyingi sana raia wa Makka.

Hata kama Makuraishi wa Makka wasingejishughulisha na biashara, bado wangenufaika na kutajirika kwa kazi za kutoa huduma mbalimbali ambazo walizifanya kwa kipindi cha mwaka mzima kuhudumia misa­fara ya biashara na mahujaji kutoka Kusini kwenda Kaskazini na kuto­ka Kaskazini kwenda Kusini. Lakini kama ambavyo imekwisha fahamika mwanzoni Makuraishi wengi walikuwa wafanya biashara hodari, kwa hiyo walileta utajiri mwingi Makka kutoka nchi jirani.

Ingawaje wafanya biashara wa Makka walipeleka msafara mmoja tu Syria na mmoja Yemen kwa kipindi cha mwaka mzima, palikuwepo na misafara mingine mingi sana midogo midogo ambayo ilifanya biashara katika sehemu nyingi za ghuba ya Uajemi mwaka mzima. Mingi ya misafara hiyo ama ilianzia humo humo Makka au ilipitia Makka kwen­da sehemu nyingine. Kwa hiyo, kulikuwepo na msongomano mkubwa wa misafara ya biashara Makka.

Misafara ilitofautiana kwa ukubwa. Kuanzia Misafara ya "wenyeji" iliyo na kiasi cha chini kabisa ngamia kumi, mpaka ya misafara ya "kimataifa" yenye wingi wa ngamia kiasi cha kufikia maelfu. Kupanga misafara ya biashara ilikuwa shughuli kubwa katika Bara Arabu.
Khadija alizaliwa Makka. Alikuwa mtoto wa kike wa Khuwaylid bin Asad bin Abdul Uzza bin Qusayy. Qusayy alikuwa babu aliyejulikana sana kwenye ukoo wa Khadija vile vile kwenye ukoo wa Muhammad Mustafa, wa uzao wa Bani Hashim, aliyekuja kuwa Mtume wa Uislamu (S.a.w.). Kwa hiyo Khadija alitokana na nasaba yenye asili moja na Bani Hashim. Baada ya Bani Hashim, familia yake ilikuwa tukufu na yenye kuheshimika sana Arabuni pote. Familia ya Khadija haikuwa mashuhuri kwa utajiri tu bali pia kwa ubora wa tabia yake.

Khuwaylid, baba wa Khadija pia alikuwa mfanyabiashara kama wenza­ke wengine wengi wa kabila la Quraysh wa Makka. Kama walivyokuwa wafanyabiashara wa kabila la Qurayshi wengi, baba yake Khadija naye alipata mafanikio ya utajiri kutokana na biashara ya nje. Wafanyabiashara wa Makka walituma misafara miwili kila mwaka mmoja wakati wa kiangazi ambao ulikwenda Syria na mwengine wakati wa kipupwe ambao ulipelekwa Yemen.

Misafara hii ya kibiashara ilibeba mazao ya jangwani na bidhaa zilizo tengenezwa Makka na sehemu za jirani yake na ziliuzwa kwenye masoko ya Syria na Yemen. Aidha waliuza farasi-chotara Syria. Aina hii ya farasi ilithaminiwa sana Syria na nchi jirani. Baada ya kuuza bidhaa zao na farasi-chotara wao, wafanyabiashara hao walileta nafaka, mafuta ya zeituni, matunda, kahawa, nguo, bidhaa za anasa na vitu vingine vilivyotengenezwa kwa ajili ya kuviuza Makka. Hivyo walipata faida Syria, Yemen na Makka.

(Biashara hii ya Makka imetajwa kwenye Quran Majid, Sura ya 106)

Biashara ya nje ilikuwa ndio msingi mkubwa wa uchumi wa Makka. Makka ilikuwa haina ardhi ya kilimo wala maji ya kilimo cha umwag­iliaji. Watu wa Makka, katika hali hiyo, hawakuweza kulima mazao ya chakula. Walitegemea biashara baina yao na Syria na Yemen ili wajil­ishe. Kutokana na faida waliyopata walinunua nafaka na vitu vingine muhimu katika maisha.

Kila msafara ulikuwa na kiongozi. Kiongozi huyu alitakiwa kuwa mtu mwenye sifa zisizo za kawaida. Usalama na kufaulu kwa msafara kati­ka biashara ya mauzo na manunuzi, ilitegemea sana maamuzi ya kiongozi. Kiongozi alikuwa na kazi ya kulinda msafara usishambuliwe na wanyang'anyi na mabedui wa jangwani. Kiongozi aliweza kufanya kazi hii kwa kuandikisha wapiganaji kutoka makabila mbalimbali na kuunda vikosi kufuatana na ukubwa wa msafara. Vikosi vilisindikiza misafara mpaka mwisho wa safari. Misafara yote iliyokwenda masafa marefu, ilikuwa chini ya ulinzi wa kijeshi.

Kiongozi wa msafara pia alitakiwa kuwa na kipaji cha pekee kwa kumuongoza kwenye jangwa lisilo na njia wakati wa mchana, na ali­takiwa kuwa na uwezo wa kutambua njia ya msafara wakati wa usiku. Kiongozi alitakiwa kuwa na ujuzi wa kuzitumia nyota katika safari wakati wa usiku. Alikuwa anatakiwa kuhakikisha kuwepo kwa maji wakati wa safari ndefu ya kwenda Syria au kwenda Yemen. Alitakiwa kuchukuwa tahadhari dhidi ya majanga yasiyotegemewa kama vile kim­bunga cha mchanga na msongamano wa miale ya taa za misafara. Alikuwa anatakiwa kuwa na uwezo wa kutoa huduma ya kwanza ya tiba endapo msafiri aliugua au aliumia.

Kwa ujumla, kiongozi alitakiwa kuwa na uwezo wa kushughulikia dharura yoyote ile. Wafanyabishara wa Makka, walimteua kiongozi wa misafara yao baada ya kuchunguza historia yake kwa uangalifu sana. Jopo la wasafiri wazoefu lilipitia majina ya watu waliopendekezwa kwa kazi hiyo.

Jopo la wachunguzi halikuridhishwa na sifa yoyote iliyo chini ya kiwan­go cha uwezo wa kiongozi wa msafara kuongoza kwa ustadi kwenye njia zisizo na michoro kwenye "bahari" ya mchanga, na kufaulu kwake kurudisha misafara ya "meli za jangwa" yaani ngamia pamoja na mizigo yao nyumbani salama. Ili akubalike kwa jopo, mtahiniwa alitakiwa kuonyesha kwamba alikuwa na uzoefu wa kutosha sana kuhusu utarati­bu wa usafirishaji wa misafara ya biashara na "vitambulisho" vyake vil­itakiwa awe hana kosa.

Mama yake Khadija alikufa mnamo mwaka wa 575 A.D.,na Khuwayled baba yake, alikufa mnamo mwaka wa 585 A.D. Baada ya kifo cha Khuwayled, watoto wake walirithi utajiri wake na waligawana mali hiyo. Utajiri una hatari zake. Utajiri unaweza kumfanya mtu akaishi maisha ya kubweteka na anasa. Khadija alitambua tabia ya utajiri kwa undani, na aliamua kutoruhusu utajiri kumfanya yeye asifanye kazi.

Khadija alikuwa na akili ya kiwango kisicho cha kawaida na uwezo wa tabia ya kuishinda changamoto ya utajiri, na aliamua kujenga himaya ya urithi kutoka kwa baba yake. Alikuwa na ndugu wengi lakini miongo­ni mwa wote hao, ni yeye peke yake ndiye aliyerithi uwezo wa baba yao kuwa tajiri. Lakini alionyesha katika kipindi kifupi sana kwamba hata kama hangekuwa amerithi utajiri wa baba yake, bado angeweza kupata utajiri kwa bidii yake mwenyewe.

Baada ya kifo cha Khuwayled, Khadija alichukuwa kazi ya kusimamia biashara ya familia na aliipanua haraka sana. Faida aliyoipata aliwa­saidia fukara, wajane, watoto yatima, wagonjwa na wasiojiweza.

Endapo palikuwepo na wasichana fukara, Khadija aliwasaidia waolewe na aliwapa mahari.

Mmoja wa wajomba zake alijitolea kumsaidia kama mshauri wake katika kuendesha biashara, na ndugu zake wengine kati­ka familia pia walimsaidia katika biashara wakati wowote alipohitaji msaada wao. Lakini hakumtegemea mtu yeyote katika kufanya uamuzi. Khadija alitegemea zaidi uamuzi wake mwenyewe ingawaje alikubali kushauriwa na kufikiria namna ya kuutumia ushauri huo. Ndugu wakubwa katika familia walitambua kwamba alikuwa hapendi ubia.

Wafanya biashara wengi waliokuwa na mizigo ya kuuza Syria au Yemeni, walisafiri na misafara yao wenyewe na kushugulikia mauzo yao binafsi. Lakini wakati mwingine mfanyabiashara alishindwa kuon­doka Makka. Katika hali kama hiyo mfanyabiashara huyo alimkodi mtu kwenda na msafara badala yake. Mtu aliyeteuliwa kwa madhumuni haya, alitakiwa awe na tabia njema kwa uaminifu wake na uwezo wa kufanya biashara. Mtu wa namna hii aliitwa Wakala au Meneja.

Khadija alikuwa mtu wa nyumbani pia ndugu zake na binamu zake hawakupenda kusafiri na misafara. Kwa hiyo, alimuajiri wakala wakati wowote msafara ulipotoka kwenda nje (ya Hijazi), na kumfanya wakala huyo kuwa na madaraka ya kupeleka bidhaa zake kwenye masoko ya nje kuziuza huko.

Kwa uwezo mzuri wa kuteua mawakala, na kununua na kuuza wakati na mahali muafaka aliweza kupata faida kubwa sana, na baadaye, akawa mfanyabiashara tajiri sana wa Makka. Ibn Sa'ad anase­ma kwenye Tabqaat yake kwamba misafara ya wafanya biashara wa Makka ilipoanza safari, mzigo wa Khadija peke yake ulikuwa sawa na mizigo ya wafanyabishara wengine wote wa Qurayish katika msafara huo.

Alikuwa dhahiri kwa kila mtu ni kama msemo "golden touch" ("mguso wa dhahabu") yaani kila atakacho kigusa hata kama ni vumbi litageuka kuwa dhahabu. Watu wa Makka, katika hali hiyo, walimpa jina la Malkia wa Qurayish. Aidha walimwita Malikia wa Makka.

Wakati huo Bara Arabu ilikuwa jamii ya kipagani, na Waarabu wali­abudu masanamu mengi na miungu masanamu, ambao waliamini walikuwa na uwezo wa kuleta bahati njema kwao. Lakini ibada yao ya kuabudu masanamu haikuwa adilifu na ilikuwa ibada ya kishenzi, tabia, mila zao na adabu zilikuwa za kukatisha tamaa.

Ulevi ulikuwa mojawapo wa uovu wao, na walikuwa wacheza kamari wasiokanyika. Walikuwa wanagaagaa kwenye shimo la dhambi na ujin­ga. Qur'an Majid inasadikisha hali yao kwenye Aya ifuatayo:

هُوَ الَّذِي بَعَثَ فِي الْأُمِّيِّينَ رَسُولًا مِنْهُمْ يَتْلُو عَلَيْهِمْ آيَاتِهِ وَيُزَكِّيهِمْ وَيُعَلِّمُهُمُ الْكِتَابَ وَالْحِكْمَةَ وَإِنْ كَانُوا مِنْ قَبْلُ لَفِي ضَلَالٍ مُبِينٍ {2}

"Yeye ndiye aliyempeleka Mtume kwenye watu wasiojua kusoma, awa­somee Aya zake na awatakase na awafunze Kitabu na Hekima, ijapokua kabla ya haya walikuwa katika upotofu ulio dhahiri" (Qur'an 62:2).

Lakini si kwamba nchi ilikuwa haina watu ambao waliona ibada ya masanamu kuwa ya kuchukiza. Watu hawa ambao walikuwa wachache sana kwa idadi waliitwa "Mahanifi" ("Hanifs") yaani wanaume na wanawake "ambao waliasi ibada ya kuabudu masanamu." Makka nayo ilikuwa na watu hao wachache kwa idadi "Mahanifi" na baadhi yao walikuwa kwenye ukoo wa Khadija. Mmoja wao alikuwa binamu yake wa kwanza, Waraqa bin Naufal.

Waraqa alikuwa mkubwa katika ndugu zake wote, na nywele zake zote zilikwisha kuwa rangi ya jivu. Aliwashutumu Waarabu kwa kuabudu masanamu na kwa kuacha njia ya kweli ya mababu zao - Mitume Ibrahim na Ismaili. Ibrahim na Ismaili walifundisha somo la Tauhiid -Imani ya Kumpwekesha Muumba. Lakini Waarabu walisahau somo hilo, na wakaingia kwenye shiriki. Waraqa aliwadharau Waarabu kwa ibada yao ya kishirikina na maadili ya ufisadi. Yeye mwenyewe alifu­ata dini ya Mtume Ibrahim, mtumishi wa kweli na Mwaminifu wa Mwenyezi Mungu. Hakumshirikisha Mwenyezi Mungu na kitu cho­chote. Hakuwa mlevi na hakucheza kamari. Na alikuwa mwema kwa fukara na walioishiwa.

Mojawapo ya tabia za kutisha za Waarabu wakati ule ilikuwa ni kuwazi­ka watoto wa kike wakiwa hai, punde wazaliwapo.

Pale ambapo Waraqa alisikia kwamba mtu alitaka kumzika mtoto akiwa hai, alik­wenda kumshauri mtu huyo asifanye hivyo, na kama sababu ya kumuua mtoto huyo ilikuwa umaskini, alijitolea kumkomboa mtoto huyo na kumlea kama mtoto wake. Katika mifano mingi, baba wa mtoto alijutia kosa lake baadaye, na alikuja kumdai mtoto wake. Waraqa alikuwa aki­taka ahadi thabiti kutoka kwa baba mhusika kumpenda mwanae wa kike na kumtendea wema, na hapo tu ndipo alipomruhusu amchukue.

Waraqa aliishi kwenye zama za ulimwengu wa upagani. Ulimwengu karibu ulikuwa unakaribia kufurika Mwanga wa Uislamu - Dini ya Mwenyezi Mungu - iliyo bora sana - Imani ya zama za kale, iliyoanzishwa karne nyingi za nyuma na Ibrahim Rafiki na Mtumishi wa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu Alikwisha mteuwa Mtumishi wake Muhammad Mustafa bin Abdullah, wa ukoo wa Bani Hashim, kuwa Mjumbe Wake mpya na wa mwisho hapa duniani. Mtume Muhammad (S.a.w.) alikuwa anaishi Makka wakati huo lakini alikuwa bado hajatangaza ujumbe wake.

Waraqa alikuwa mmojawapo wa watu wachache sana wa Makka walioelimika. Inasemekana alitafasiri Biblia kutoka kwenye lugha ya Kiebrania kuwa Kiarabu. Aidha alikwisha soma vitabu vingine vilivyoandikwa na wanatheolojia Wayahudi na Wakristo. Alikuwa mtafutaji makini wa ukweli ndani ya giza la dunia inayoendelea kuwa ndani ya giza nene zaidi, na alikuwa na nia ya kuupata ukweli huo kabla ya kifo chake, lakini hakujua angeupataje.

Khadija aliathiriwa sana na fikira za Waraqa na alikubaliana na Waraqa kuichukia ibada ya masanamu na watu waabuduo masanamu.

Hakumshirikisha Muumba na kitu chochote. Kama alivyokuwa Waraqa na ndugu wengine katika familia, naye pia alikuwa mfuasi wa Mitume Ibrahim na Ismaili.

Khadija alikuwa Muwahhid ( mwenye kumwamini Mungu Mmoja wa Pekee)! Khadija hakujua kwamba baada ya miaka michache hatima yake ingeingiliana na hatima ya Muhammad Mustafa, Mtume wa Imani ya Mungu Mmoja (Tauhiid); na hatima ya Uislamu, imani ya Mungu Mmoja.

Kabla ya Uislamu Bara Arabu ilikuwa haina mpango wowote wa kisi­asa, na haikuwa na miundo mbinu ya aina yoyote. Hapakuwepo na mahakama au polisi au mfumo wowote wa sheria. Kwa hiyo, hapakuwepo na chombo cha kuzuia utendaji wa makosa, au kuwazuia wahalifu. kama Mwarabu alifanya kosa, hakuonyesha kujuta kokote. Badala yake alijivuna na kutamba kwamba angeweza kufanya lolote bila kujali, na kuweza kuwa katili na mkorofi.

Rasi yote ya Arabuni iliendeshwa kwa mfumo-dume. Mwanamke hakuwa na daraja kwa vyovyote vile. Waarabu wengi waliamini kwam­ba wanawake walileta mikosi. Kwa ujumla waliwaona wanawake kama mali inayohamishika na si watu.

Mwanaume aliweza kuoa wanawake wengi kwa idadi aliyopenda. Na wakati akifa, mtoto wake wa kiume wa kwanza aliwarithi wanawake (wakeze marehemu baba yake) wote isipokuwa mama yake. Kwa maneno mengine aliwaoa mama zake wa kambo wote isipokuwa mama yake aliyemzaa. Jambo kama hili, sheria na kanuni za maadili hazikuwepo kumzuia kwa njia yoyote ile. Uislamu ulisitisha desturi hii kisheria.

Waarabu walioishi kabla ya Uislamu hawakuwa na maadili mema. Mwarabu alitumia maisha yake yote kwenye ghasia za kivita. Mauaji na uporaji ilikuwa ndio kazi yake kubwa. Aliwatesa wafungwa wake wa kivita hadi kufa, na kuwatesa wanyama ilikuwa moja ya mambo yake ya kupitisha wakati. Mwarabu alikuwa na ukaidi wa hisia ya utukufu, ambao ulifanya auwe mtoto wake mwenyewe wa kike. Kama mkewe alizaa mtoto wa kike, alikuwa hawezi kuzuia uchungu na hasira zake.

"Na mmoja katika wao anapopewa khabari ya (kuzaliwa kwake) mtoto wa kike, husawijika uso wake ( huwa mweusi) akajaa sikitiko!.

(Akawa) anajificha na watu kwa sababu ya hatari mbaya aliyoambiwa! (anafanyashauri) Je, akae naye juu ya fedheha hiyo au amfukie udongo­ni (karibuni na hali ya kuwa mzima ili afe)? Sikilizeni! Ni mbaya mno hukumu yao hiyo. (Quran 16:58-59)

Mara nyingi Mwarabu alimuua mwanae wa kike kwa kuogopa kwamba angekuwa mateka wa kivita wakati wa vita vya kikabila, na kwa hiyo, kuwa mtumwa wa adui, na daraja lake kama mtumwa kungeleta aibu kwa familia yake na kabila lake. Angeweza pia kumuua kwa kuhofia kwake umasikini. Aliamini kwamba binti yake angekuwa tatizo la kiuchumi kwake. Uislamu ulifanya mauaji ya watoto kuwa ni dhambi kubwa kabisa.

وَلَا تَقْتُلُوا أَوْلَادَكُمْ خَشْيَةَ إِمْلَاقٍ ۖ نَحْنُ نَرْزُقُهُمْ وَإِيَّاكُمْ ۚ إِنَّ قَتْلَهُمْ كَانَ خِطْئًا كَبِيرًا {31}

"Wala msiwaue wana wenu kuogopa umasikini. Sisi tunawaruzuku wao na nyinyi. Hakika kuwaua hao ni hatia kubwa." (Qur'an 17:31).

Vilevile walikuwepo Waarabu ambao hawakuwaua watoto wao, lakini waliwanyang'anya haki zao zote. Walifikiri kwamba kwa vile binti zao watakapoolewa watakwenda kuingia nyumba nyingine za waume wao, hapakuwepo na haja ya kutumia gharama yoyote juu yao.

Ilikuwa katika mazingira ya namna hii ambayo Khadija alizaliwa, akakua na kuishi mazingira ya "kumkataa mwanamke."

Kutokea nyumbani kwake Makka, Khadija aliendesha biashara iliyokuwa inaendelea kukua na kuenea kwenye nchi za jirani. Kile ambacho alikwisha faulu kukipata kingekuwa cha kusifika katika nchi yoyote, katika kipindi chochote na kwa mtu yoyote mwanamume au mwanamke. Lakini mafanikio yake yamesifika mara mbili pale ambapo mtu atafikiria ule "mfumo-dume" wa kumpinga mwanamke, ulioen­dekezwa na Waarabu. Huu ni uthibitisho wa uwezo wake wa kumudu hatima yake kwa kutumia akili yake, nguvu ya dhamira na tabia. Wafanyabiashara wenzake walikubali mafanikio yake walipomwita Malikia wa Makuraishi na Malkia wa Makka kama ambavyo imetamk­wa huko nyuma.

Lakini zaidi ya sifa, Khadija pia alipata cheo cha tatu. Aliitwa "Tahira" maana yake ni "aliyetakasika." Nani aliyempa cheo cha "Tahira"? Ajabu ni kwamba, alipata cheo hiki, kutoka kwa Waarabu haohao waliokuwa na sifa mbaya kwa ujeuri, majivuno, kiburi na ujinsia. Lakini, tabia ya Khadija ilikuwa mfano mzuri wa kuigwa hivyo kwamba ilitambuliwa hata na wao, na wakamwita "aliyetakasika."

Ilikuwa ni kwa mara ya kwanza katika historia ya Arabuni kwa mwanamke kuitwa Malikia wa Makka na aidha kuitwa "Tahira." Waarabu walimwita Khadija Malkia wa Makka kwa sababu ya utajiri wake na walimwita Tahira kwa sababu ya utakatifu wa sifa zake. Pia walikuwa wanaelewa kwamba alikuwa na tabia njema. Kwa hiyo alikuwa mtu wa kuheshimika hata kabla ya Uislamu - kipindi cha Ujahiliya.

Ilikuwa ni jambo lisilopingika kwamba Khadija angetamaniwa na Waarabu mashuhuri na wana wa Wafalme. Wengi wao walipeleka posa ili wamuoe.

Lakini hakutaka kuolewa na yeyote kati yao. Wengi wa hao watu mashuhuri na wana wa Wafalme waling'ang'ania kutaka wamuoe.

Bila kukatishwa tamaa na kukataa kwake, waliendelea kutumia washen­ga wanaume na wanawake wenye kuheshimika kuendelea kumbem­beleza. Lakini bado aliwakataa wote. Hii labda ni kwa sababu Khadija hakutilia maanani sana umuhimu wa uongozi wa mfumo-dume uliotawaliwa na wanaume katika jamii "inayowapiga vita wanawake."

Kukataa kwa Khadija kuolewa na Waarabu mashuhuri na wenye hadhi za juu, kulizua dhana nyingi kwamba ni mwanamume wa aina gani atakaye muoa. Lilikuwa ni Swali ambalo hata Khadija mwenyewe hakuweza kulijibu. Lakini majaliwa yalifahamu jibu lake; alikuwa aolewe na mwanaume ambaye si tu alikuwa bora kabisa kuliko wote katika nchi yote ya Arabu lakini alikuwa pia bora sana kuzidi viumbe wote. Ilikuwa ni majaliwa yake iliyomchochea kukataa maombi ya kuolewa na binadamu wa kawaida.
Ingawaje nchi ya Arabu haikuwa na serikali yoyote- ya kitaifa, kijimbo au kienyeji - jiji la Makka lilikuwa linatawaliwa na kabila la Qurayishi, kama ilivyotajwa kabla. Kabila la Qurayish lilikuwa na koo kumi na mbili. Koo hizi zilishirikiana majukumu ya kudumisha kiasi kidogo cha sheria na utulivu katika mji wa Makka.

Moja ya koo za kabila la Qurayshi ilikuwa Bani Hashim. Kila ukoo ulikuwa na kiongozi wake. Kiongozi wa Bani Hashim alikuwa Abu Talib bin Abdul Muttalib bin Hashim bin Abd Manaf bin Qusayy. Kama walivyokuwa babu zake, Abu Talib pia alikuwa mfanyabiashara. Zaidi ya kuwa mkuu wa ukoo, alikuwa pia mlezi wa Al-Kaaba - Nyumba ya Mwenyezi Mungu - iliyojengwa Makka, karne nyingi zilizopita, na Mtume Ibrahim na Ismaili na wakaitoa wakfu imtumikie Mwenyezi Mungu.

Abu Talib alikuwa na mdogo wake aliyeitwa Abdullah. Mwaka wa 570 A.D., Abdullah alikwenda Syria na msafara wa biashara. Miezi michache kabla hajasafiri kwenda Syria alimuoa Amina binti Wahab, mwanamke kutoka Yathrib (Madina).

Wakati Abdullah alipokuwa anarudi kutoka Syria, aliugua na kufa. Alikuwa na umri wa miaka 17 tu alipokufa. Alipoondoka Makka, mke wake alikuwa mja mzito na alikuwa anaishi nyumbani kwa shemeji yake, Abu Talib. Miezi miwili baada ya kifo cha Abdullah, alijifungua mtoto wa kiume. Babu wa mtoto huyu, Abdul Muttalib, alimpa jina la Muhammad. Muhammad alizaliwa tarehe 8, Juni, 570, nyumbani kwa baba yake mdogo, Abu Talib mjini Makka.

Siku za usoni, mtoto mchanga Muhammed alikuwa ateuliwe na Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwa Mjumbe Wake wa dunia yote, na alikuwa abadilishe majaliwa na historia ya binadamu daima milele.

Muhammad alikuwa na umri wa miaka sita wakati mama yake, Amina binti ya Wahab, alipokufa baada ya kuugua kwa muda mfupi. Kutokana na kifo chake hicho, babu yake Muhammad, Abdul Muttalib, alim­chukua ili amlee nyumbani kwake. Lakini ilikuwa baada ya miaka miwili tu Abdul Muttalib naye alifariki.

Abdul Muttalib alikuwa na watoto wa kiume kumi. Alipokaribia kufa, aliwaita watoto wake wote, na alimteuwa mwanae Abu Talib kama mkuu mpya wa ukoo wa Bani Hashim.

Pia alimfanya mlezi wa Muhammad. Wote wawili Abu Talib na Abdullah, baba wa Muhammad, walikuwa watoto wa mama mmoja, ambapo watoto wengine wa Abdul Muttalib walizaliwa na wakeze wengine.

Abu Talib alimpeleka Muhammad nyumbani kwake. Muhammad ali­washinda wote (kwa tabia). Abu Talib na mkewe walimpa Muhammad mapenzi makubwa sana. Walimpenda zaidi kuliko walivyowapenda watoto wao. Muhammad alizaliwa ndani ya nyumba yao. Kuzaliwa kwa Muhammad ndani ya nyumba hiyo ilisababisha nyumba hiyo iwe na neema nyingi; na sasa baada ya kifo cha Abdul Muttalib, alirudi tena ndani ya nyumba hiyo.

Muhammad alipokuwa mtoto, hakuonyesha kuvutiwa na mwanasesere na michezo ya watoto. Katika ujana wake, hakuonyesha kupenda michezo na burudani, au kuwa katika makundi ya vijana wa rika lake. Pamoja na kwamba alikuwa kijana, alipendelea zaidi upweke kuliko kuchanganyika kwenye makundi ya vijana wenzake.

Kama walivyokuwa watu wengine wa kabila la Qurayish, Abu Talib pia alikuwa akipeleka bidhaa zake Syria na Yemen kila mwaka. Wakati mwingine alikwenda yeye mwenyewe na misafara, na kipindi kingine aliajiri Wakala ambaye aliuza bidhaa zake kwenye masoko ya nchi hizo. Mnamo mwaka wa 582 A.D. Abu Talib aliamua kutembelea Syria akiwa na msafara. Mpwa wake, Muhammad, alikuwa na umri wa miaka 12 wakati huo. Abu Talib alimpenda sana hivyo kwamba alikuwa hawezi kuachana naye hata kwa muda wa miezi michache. Kwa hiyo, alimchukua na kwenda naye Syria.

Akili ya Muhammad ilikomaa upesi, na pamoja na kwamba umri wake ulikuwa bado mdogo sana, alikuwa mchunguzi na mdadisi aliyebariki­wa. Wakati wa safari yake nje na ndani ya Syria, kwa uangalifu sana ali­wachunguza watu na mila zao, desturi zao, namna wanavyo abudu, mavazi yao, hotuba na upembuzi wao wa mambo. Na kila alichokiona, alikumbuka.

Aliporudi Makka, aliyakumbuka yote yale aliyoyaona toka mwanzo hadi mwisho na aliweza kukumbuka uchunguzi wake wote bila kubakisha kitu. Hakusahau kitu; kwa hakika, alikumbuka kila kitu. Ingawaje alikuwa mdogo kwa umri, alikomaa kihekima na matumizi ya akili ya kawaida. Abu Talib alitambua kwamba Muhammad alikuwa na hekima na akili iliyopevuka kuliko umri na uzoefu wake. kwa hiyo, hakumchukulia kama mtoto mdogo kwani ilibidi aonyeshe heshima kwake kama ile anayostahili kupewa mtu mzima wa jamii ya Kiarabu.

Haikupita muda mrefu Muhammad alipata umri unaozidi miaka kumi. Ingawa katika rika la kijana aliye balehe, alikuwa bado hakuvutiwa na starehe ambazo vijana wengine huzitafuta. Alijiepusha na purukushani za aina zote na kama ilivyoelezwa huko nyuma, alipendelea kuwa peke yake na tafakuri yake. Alikuwa na fursa ya kutosheleza upendeleo huu alipokwenda kuchunga kondoo wa ami yake. Alikuwa peke yake chini ya anga. Jangwa lililo kimya na kujitandaza hadi upeo wa macho, na ambalo lilimpa matumaini ya kutafakari kuhusu maajabu ya Uumbaji, siri za mbingu na ardhi, na maana na madhumuni ya maisha.

Alitazama mandhari ya ardhi kutoka upeo wa macho huu hadi mwingine, na ilionekana kama vile ukubwa wa ulimwengu ulikuwa ndio swahiba pekee "aliyekuwepo" pamoja naye. Upweke kwake ulionekana kuwa "kipimo" kipya cha ulimwengu wake. Wakati Muhammad alipokuwa amevuka ujana wake, watu wa Makka walikwishaanza kumtambua. Walijua kwamba kamwe hakupotoka kuto­ka kwenye maadili mema na utu mwema na hakufanya kosa kamwe. Aidha walitambua kwamba hakupenda kusema sana na alipofanya hivyo, aliongea kweli tupu, na alitamka maneno ya hekima tu. Kwa kuwa watu wa Makka walikuwa hawajamsikia akisema uongo, wal­imwita "As-Sadiq" (Mkweli).

Katika kipindi cha miaka michache iliyofuata, raia wa Makka walimpa Muhammad cheo kingine. Kwa kutambua kwamba alikuwa makini sana, wengi wao walianza kumpa mali zao ili awatunzie kama vile: fedha taslimu, vito, mapambo, na vitu vingine vya thamani. Wakati mtu yoyote alipotaka mali yake, Muhammad alimrudishia yote. Kamwe hapakutokea kasoro yoyote katika kurudisha mali za watu.

Baada ya kuthibitisha kuwa alikuwa na tabia ya namna hiyo, kwa kipindi cha miaka kadhaa watu walianza kumwita Muhammad "Al-Amin". (Mwaminifu) Ni yeye, na yeye peke yake aliyeitwa As-Sadiq na Al-Amin na watu wa Makka.

A. Yusuf Ali mtarjumi na mfasiri wa Qur'anTukufu, amelielezea neno "A-Amin" kama ifuatavyo: "Al-Amin Mtu ambaye amana imewekwa kwake, pamoja na maana mbali mbali kidogo zimedokezwa:

1. Aanyestahiki kuaminiwa;

2. Anayewajibika kuitoa amana yake, kama Mtume yeye huwajibika kutoa Ujumbe wake;

3. Anawajibika kabisa kutenda kama ambavyo amana inaelekeza, kama mtume anawajibika kufikisha Ujumbe wa Mwenyezi Mungu tu, na asiongeze chochote cha kwake, na

4. hatafuti masilahi yake mwenyewe."

Waarabu walioishi kabla ya Uislamu kila mwaka walifanya "Msimu wa maonyesho" sehemu mbalimbali za nchi. Baadhi ya maonyesho haya yalionyeshwa Makka na sehemu nyengine za karibu yake. Maonyesho yaliyojulikana sana ni: Ukkaz, Majanna na Dhul-Majaz. Muhammad aliyatembelea maonyesho hayo pale muda ulipomruhusu kufanya hivyo. Maonyesho yote haya yalionyeshwa wakati wa miezi minne mitakatifu ya Rajab, Dhil-Qaada, Dhil-Hajj na Muharram, kufuatana na mila za Waarabu wa kale. Ndani ya miezi hii minne, mambo yafuatayo yalip­igwa marufuku: vurugu, vita, kuteka nyara na unyang'anyi. Mnamo mwanzo wa "Msimu wa amani" tangazo la kusimamisha vita lilitolewa. Tangazo la kusitisha vita lilitambuliwa na kuheshimiwa na makabila yote ya Waarabu.

Wafanya biashara, wakulima na wastadi (wachonga sanamu) waliku­sanyika kwenye maonyesho haya kutoka sehemu za mbali na za karibu (kwa ajili ya) kuuza, kununua na kubadilishana. Walileta pamoja nao mazao yao yaliyo bora kabisa, na kwa fahari waliyafanyia maonyesho. Sanaa nyingine za amani, mashairi yakiwa miongoni mwao, yalikuzwa (na kutukuzwa katika wakati zilipositishwa vurugu (na vita)

Mashairi yalikuwa penzi la kwanza la Waarabu. Kama kipaji cha mashairi kiligunduliwa kwenye kabila lolote, lilikuwa jambo la kush­erehekewa na kila mmoja. Makabila mengine yenye uhusiano mzuri na kabila husika, yalilipongeza kabila hilo kwa kuzalisha kipaji cha namna hiyo. Waarabu walikuwa washabiki wakubwa wa maneno ya Kiarabu na maana yake nyingi. Wao walijiita "watoto wa Kiarabu."

Kwenye maonyesho haya washairi walisoma tunzi zao mpya, sifa ambayo Waarabu waliithamini kuwa ya muhimu na maana sana. Mojawapo ya misemo yao ni kwamba uzuri wa mwanamke upo kwenye uso wake; lakini uzuri wa mwanamume upo katika uhodari wake wa kujieleza. Walipenda ustadi wa utunzi na ufasaha wa yale yanayosemwa kwenye mashairi.

Mafumbo yasiyo ya kawaida ya jangwani na watabiri wanao­fanana na wanyama pori na waaguzi wa makabila, huwafurahisha wasikilizaji kwa hotuba zao za mafumbo hadithi zao za mafumbo na siri za ubashiri, hata hivyo, wachache waliweza kuelewa ishara hizo. Waarabu wengi waliamini kwamba utabiri wa nyota uliamua mwisho mzuri au mbaya wa maisha ya mtu.

Kwa hiyo, watu wa nchi nzima waliwaogopa watabiri, iliaminika kwamba walikuwa na uwezo wa kuzungumza na nyota. Waimbaji, wacheza dansi, wachekeshaji, wana sarakasi na wana mazingaombwe wote walishindana ili wapate kusifiwa na watazamaji.

Maonyesho haya yalihudhuriwa na watawa, makuhani na watu watakat­ifu ambao walihubiri imani ya ibada zao. Wote walikuwa huru kueneza itikadi zao na fikira zao bila woga wa kuonewa na mtu yeyote katika kipindi chote cha miezi minne. Amani na sanaa za amani vilishamiri dhidi ya mfululizo wa mambo ya uchangamfu wa binadamu usio na mipaka.

Kwenye maonyesho haya, Muhammad alipata fursa ya kuchunguza wakazi wa rasi ya Bara Arabu. Pia alijifunza, kwa mara ya kwanza, mila na imani za watu wa jamii tofauti, na utamaduni na usuli za kijogorafia.

Mnamo majira ya kuchipua ya mwaka wa 595 A.D., wafanyabiashara wa Makka walikusanya msafara wao wa majira ya kiangazi ili wapeleke bidhaa zao Syria. Pia Khadija alitayarisha bidhaa zake lakini alikuwa hajapata mtu mwanamume atakayesimamia msafara wake na kuwa wakala wake. Majina machache yalipelekwa kwake lakini hakupata lililompendeza.

Kupitia kwa baadhi ya weza wake wa chama katika wachuuzi wa Makka, Abu Twalib alipata habari kwamba Khadija alikuwa anatafuta wakala ambaye atachukua mizigo yake pamoja na msafara kwenda Syria na kuiuza kule.

Ilipita akilini mwa Abu Twalibu kwamba mpwa wake Muhammad ambaye sasa alikuwa na miaka ishirini na tano angelifaa kwa kazi hiyo Alikuwa na hamu kubwa ya kumtafutia kazi mpwa wake. Alijua kwam­ba yeye (Muhammad) hana uzoefu wa kazi ya uwakala lakini pia alijua kwamba yeye (Muhammad) angeweza kazi hiyo kwa sababu ya kipaji chake.

Alikuwa na imani na uwezo na akili za mpwa wake na alikuwa na uelewa wa kutosha kufanya kazi yake ya uwakala kwa tajiri yake. Kwa hiyo, pamoja na makubaliano yake ya kimya (na Muhammad), alikwenda kwa Khadija, na alianzisha mazungumzo kuhusu suala la uteuzi wake (Muhammad), kama wakala wake mpya.

Kama ilivyo kwa raia wengine wengi wa Makka, Khadija pia alikwisha sikia kuhusu Muhammad. Khadija alijua kwamba hangehoji kuhusu heshima ya Muhammad. Aliona kwamba angeweza kumwamini Muhammad kwa wazi na kwa siri. Kwa hiyo alikubali kumteua Muhammad kuwa wakala wake. Hakufikiria kutokuwa na uzoefu ingekuwa tatizo kwa Muhammad, na akasema kwamba, kwa jinsi yoy­ote ile, angempeleka mtumwa wake Maysara, ambaye alikuwa na uzoe­fu wa kusafiri, awe pamoja naye (Muhammad) amsaidie katika kazi zake.

Khadija alikuwa mwendeshaji mzuri sana na mpangaji aliyekamilika. Lakini pia alikuwa na bahati njema. Kila mara alikuwa na bahati ya kupata mawakala wazuri kwa biashara yake. Hata kama alikuwa na hali ya kufuzu, alistaajabu baada ya kipindi kifupi kugundua kwamba akiwa na Muhammad kama wakala wake, bahati yake iliongezeka kwa kiwan­go ambacho ilikuwa haijapata kutokea. Kwa Khadija, kamwe palikuwa hapajatokea siku za nyuma, na kamwe haingetokea kwa siku za baadaye kuwa na wakala kama Muhammad.

Kama Khadija alikuwa na kile kitu kinachoitwa "mguso wa dhahabu" (golden touch) mkononi mwake, Muhammad alikuwa na "mguso wa baraka" mkononi mwake.

Khadija na Abu Talib walitayarisha vipengele vyote vya mpango mpya. Na Muhammad alipokwenda kumuona tajiri wake mpya kwa madhu­muni ya kukamilisha mkataba, alimwambia mambo yote kuhusu biashara hiyo. Muhammad alielewa haraka sana katika yote Khadija aliyomwambia na hakuuliza swali lolote lile lililohitaji ufafanuzi. Khadija alimwambia Abu Talib kwamba ujira ambao atampa Muhammad kwa kazi yake utakuwa mara mbili zaidi ya ule aliokuwa anawapa mawakala wengine huko nyuma.

Jambo ambalo Khadija hakulijua wakati huu ni kwamba ulikuwa ni ule mkono wa majaliwa ndiyo uliokuwa unafanya kazi katika kuusukuma mpango huu. majaliwa yalikuwa na mipango mingine kwake yeye na Muhammad. Mipango hiyo ilivuka mipaka ya ulimwengu huu na masu­ala ya thamani ndogo ya pesa, kama kupata faida kwenye biashara, kama ambavyo hivi punde matukio yatakavyoonyesha.

Kwa wakati huo, "msafara wa kiangazi" wa wafanya biashara wa Makka ulikwisha kamilika, na ulikuwa tayari kuondoka kuelekea kwenye safari yake ndefu. Wafanyabiashara walileta mizigo yao kuto­ka kwenye maghala ili ipakiwe kwenye ngamia. Mikataba ilitayarishwa na kusainiwa. Mahitaji ya njiani yalichukuliwa, na viongozi na wasindikizaji waliajiriwa. Kwa muda uliopangwa, Muhammad na Abu Talib na ami zake wengine walifika. Walisalimiwa na ami yake Khadija ambaye alikuwa anawangojea akiwa na Cheti cha orodha ya Shehena na hati nyingine.

Muhammad aliamua kuhesabu mali ya kuuza huko Syria. Akisaidiana na Maysara, alikagua mali yote na aliona kila kitu kiko sawa sawa. Maysra alifanya kazi ya makaratasi yahusuyo mauzo na manunuzi. Alikuwa mtunza taarifa ya mali.

Abu Talib alitoa maelekezo maalumu kwa Maysara na kwa kiongozi wa msafara kuhusu usafiri wa raha na salama kwa Muhammed. Waliahidi kuhakikisha kwamba Muhammed angesafiri kwa raha na salama. Abu Talib na ndugu zake waliwashukukuru kwa kuonyesha ushirikiano kuhusu safari ya Muhammad.

Walimwombea dua apate mafanikio kati­ka kazi yake mpya na kurudi salama. Halafu wakamkabidhi Mwenyezi Mungu amlinde arudi salama, na wakaagana.

Wakati wa kiangazi misafara mingi ilisafiri usiku kukwepa joto kali la mchana, na kupumzika mchana. Safari ya mchana ingechosha sana wafanya biashara, ngamia na farasi. Kwa hiyo, misafara mingi iliondo­ka Makka saa za alasiri, kama walivyosema Waarabu, au jua linapokuwa limepita katikati, na joto huwa limepungua.

Msindikizaji mmoja aligonga kengele. Wasafiri wote walijitayarisha na msafara ulikuwa tayari kuondoka. Ngamia waliokuwa wamepumzika walisimama, bila kupenda, walionyesha kutokutaka kuondoka kwa kukataa na kukoroma lakini waliingia kwenye msafara. Takribani saa tatu kabla ya jua kuchwa kiongozi wa msafara alitoa ishara, na msafara ukawekwa tayari kwa kuondoka.

Msafara ulielekea Kaskazini. Ndugu na marafiki wa wasafiri walikaw­ia kwa muda fulani huku wakiwa wanapunga mikono na kutazama msa­fara unavyosonga mbele. Ngamia wa mwisho alipokingizwa na vilima, wasindikizaji nao walisambaa.

Wasafiri wapya walikaa pamoja na wasafiri wazoefu ambao walikuwa wanawaonyesha sehemu za kuvutia walizokuwa wanazijua na walielezea upekee wa sehemu hizo. Maysara alimwonyesha Muhammad sehemu nyingi za kupendeza. Muhammad pia alizitambua sehemu nyingi alizoziona barabarani alipopita humo miaka kumi na tatu iliyopita akiwa na ami yake. Hakuna kilicho badilika wakati wa miaka hiyo 13.

Maysara alithibitisha kuwa msafiri mwenza mchangamfu ambaye aliweza kusimulia hadithi nyingi na aliweza kukumbuka matukio mengi sana aliyoyaona wakati wa safari zake za siku za nyuma. Muhammad aligundua kwamba wasafiri wengine pia walikuwa wachangamfu na wenye kufanya urafiki.

Baada ya takribani mwezi mmoja, msafara ulifikia mwisho wa safari yake ulipofika Syria. Mipango ya nyumba ya kupanga ilikwisha tayarishwa kwa ajili ya wasafiri waliochoka kwa msafara, na wote wal­itaka kupumzika baada ya safari ndefu iliyowapitisha kwenye mandhari zilizosababisha safari kuwa ngumu na joto kali. Waliweza kupumzika kiasi cha wiki moja ili kuponyesha sehemu muhimu za mwili zilizo athirika.

Wafanyabiashara walipokwisha pumzisha viungo vyao vilivyokuwa vinauma na kupata nguvu upya tena, walikwenda sokoni kuuza mali zao walizoleta kutoka Makka. Kiasi fulani cha mali waliuza kwa fedha taslimu, na iliyobaki walibadilisha mali kwa mali kwa bidhaa za Syria. Iliwabidi pia wanunue bidhaa kwa ajili ya soko la nyumbani, na wal­itafuta na kupata mali nyingi yenye faida. Shughuli za msafara ziliweza kudumu kuanzia miezi miwili hadi minne.

Muhammad pia aliuza na kununua mzigo mpya. Ingawa kwake yeye ilikuwa msafara wa kwanza wa kibiashara, hakusita kwa sababu ya kutokuwa na uzoefu, katika shughuli za biashara. Hakika alimshangaza Maysara kwa werevu wake katika biashara. Aidha Maysara aligundua kwamba Muhammad alikuwa mwepesi kuelewa na kuamua katika mazungumzo ya biashara na upevu wake wa akili na uaminifu wake kama muuzaji. Muhammad alilinda maslahi ya tajiri yake na wateja wake, na bado alipata faida kubwa zaidi katika shughuli hiyo ya Khadija kuzidi mara zote alizokuwa amefanya biashara tangu bibi huyo kurithi biashara ya baba yake. Na bidhaa alizonunua Syria kwa ajili ya biashara ya Khadija zilikuwa safi sana kwa ubora wake na hakika zingepata bei nzuri Makka, na ilitokea hivyo.

Huko Syria yeyote aliyemuona Muhammad, alivutiwa naye. Alikuwa na umbo la kuvutia ambalo liliwafanya watu wasimsahau hata kwa kumuona mara moja tu. Ingawa Muhammad alijishugulisha na kuuza mali, mapatano ya biashara, kuchunguza soko, na kununua, Maysara aling'amua kwamba hata hivyo alipata muda wa kukaa peke yake.

Kwa maoni ya Maysara, hivi vipindi vya ukimya wa Muhammed, vilikuwa chanzo cha jambo lililojificha, lakini hakuviingilia kati. Maysara hakuwa anajua kwamba bosi wake mwenye umri mdogo alikuwa na desturi ya kutafakari kuhusu hali na majaliwa ya mwanadamu.

Wakati akiwa Syria Muhammad alikutana na Wakristo na Wayahudi wengi. Alidhani kwamba kila kundi kati ya hayo mawili yangekuwa na "imani ya Mungu Mmoja." Lakini alistaajabu alipofahamu kwamba haikuwa hivyo. Makundi yote mawili yaligawanyika katika makundi mengine madogo mengi, na aina ya ibada ya kila kundi ilikuwa tofauti na ile ya makundi mengine. Miongoni mwao kundi lipi lilikuwa sahihi na lipi halikuwa sahihi? Hili lilikuwa swali ambalo lilimsumbua Muhammad.

Utafiti wa udadisi wa jibu la swali hili, na maswali mengine madogo madogo yenye kufanana na hili yalimfanya Muhammad asilale usingizi wakati kila mmoja amekwenda kulala.

Hatimaye, shughuli za biashara zilipokwisha, na zawadi za ndugu na marafiki kununuliwa, msafara ulirudi Makka. Kwa wasafiri wakum­bukao sana nyumbani, kurudi nyumbani mara zote ni tukio la kufu­rahisha. Ni tukio lililojaa matumaini kwani mtu atakutana na awapendao ambao mtu hakuwa nao kwa miezi mingi. Wasafiri wachovu hawawezi kungoja kwa muda mrefu kusikia vicheko vya furaha vya watoto wao na wanatambua kwamba wakati mzuri kama huo ukiwadia hawawezi kuzuia na kuficha machozi.

Wanajua kutokana na uzoefu wa muda mrefu kwamba pangekuwapo na kulia machozi - machozi ya furaha. Kicheko na Machozi vyenye mchanganyiko ulio huru kabisa katika vipindi vya heri na furaha isiyo na upeo.

Kuwasili kwa msafara mara kwa mara kulisisimua mji. Kwa hakika ulikuwa wakati wa kusherehekea kwa kila mkazi wa Makka na vitongoji vilivyomo pembezoni mwake. Sehemu zilizotengwa maalum kwa ngamia kushushia abiria na mizigo, zilikuwa changamfu mno. Raia walio wengi na hata yale makabila yanayohamahama waliona pilika pilika za kuwasili kwa msafara kwamba yalikuwa mabadiliko ya kutia moyo katika mwenendo wa maisha.

R.V.C. Bodley, ameandika katika kitabu chake:

"Kuwasili na kuondoka kwa misafara yalikuwa matukio muhimu kwa maisha ya watu wa Makka. Karibu kila mkazi wa Makka alikuwa na aina fulani ya uwekezaji kwenye mali iliyobebwa na maelfu ya ngamia, mamia ya watu, farasi na punda:- bidhaa hizo zilikuwa ngozi, zabibu kavu, vinoo vya fedha, na walirudi na mafuta, manukato na bidhaa zili­zozalishwa viwandani kutoka Syria, Misri na Uajemi, na viungo na dhahabu kutoka Kusini.

(The Messenger- the life of Muhammed,1946)

Watu walikuja kuwasalimia wapenzi wao ambao walikuwa wanarudi nyumbani baada ya kutokuwepo kwa kipindi cha miezi sita. Wengi wao walikuja wakiwa na fikira mchanganyiko wa matumaini na woga.

Ilipotokea mtu anaondoka mjini kwenda na msafara, hapakuwepo na njia yoyote kwa ndugu zake kujua kama wangemuona akiwa mzima tena. Wasafiri wengine walikufa wakiwa safarini na walizikwa kwenye sehemu ambazo ni njia za ndani ndani sana, na hazipitiki. Ndugu zao kamwe hawakuweza kuyatembelea makaburi yao.

Na ilikuwa hapo tu ambapo msafara ulifika ndipo wakazi wa Makka waliweza kusikia habari za dunia nje ya bara Arabu. Waarabu wa siku hizo waliishi katika hali ya upweke sana katika dunia yote. Katika dunia hiyo Waarabu walikuwa na njia moja tu ya kupata habari nayo ni msa­fara.

Takriban kila raia wa Makka aliwekeza fedha kwenye msafara wa biashara. Watu matajiri miongoni mwao waliweza kutembelea nchi za nje kwa muda mrefu zaidi wa miezi mingi. Lakini watu ambao hawakuwa na uwezo wa kifedha walibaki nyumbani.

Hivyo, waliwapa bidhaa zao watu walio waaminifu kuwa mawakala wao wauze kwa niaba yao, na waliwapa wao fedha ya kwenda kununua bidhaa ambazo zilikuwa zinatakiwa Arabuni na ziliweza tu kupatikana kwenye masoko ya Syria, Yemen, Habeshi na Misri.

Baada ya mawakala wao kuleta mali za nje Makka, waliuza bidhaa hizo na kupata faida. Ulikuwa ni utaratibu ambao baada ya uzoefu wa muda wa miaka mingi, mpango huu ulionekena unafaa na unatekelezeka.

Wafanyabiashara na mawakala waliokuwa kwenye msafara pia walileta zawadi kutoka nchi za nje na tuzo kwa ndugu na marafiki zao, kufuatana na mila za zamani. Kila mtu alitaka kuona zawadi hizo ambazo zili­wakumbusha utajiri uliopo Syria na anasa za Falme za Ajemi na Roma.

Muhammad alipofika Makka, kitu cha kwanza kufanya ni kuzunguka Al-Kaaba mara saba kama ilivyokuwa desturi, na halafu alikwenda kumuona muajiri wake.

Alimwelezea tajiri wake kwa kina kuhusu safari na shughuli za biashara alizozifanya kwa niaba yake. Baadae, alimwelezea ami yake Abu Talib, kuhusu matukio ya kuvutia kwenye uzoefu wake kama mfanyabiashara.

Maysara, mtumwa wa Khadija, naye alikuwa na taarifa yake mwenyewe ya kumpa mmilki wake. Alimwambia Khadija kuhusu safari ya kwen­da na kurudi kutoka Syria, na faida ambayo Muhammad aliingiza kwenye biashara yake. Lakini kwake yeye (Maysara), kilichompendeza zaidi kuliko kufuzu katika biashara, ni tabia na utu wa Muhammad. Maysara alimwambia Khadija kwamba alipendezwa na kipaji cha Muhammad katika biashara. Aliendelea kumtaarifu Khadija kwamba uwezo wa Muhammad kuona mbali kibiashara ilikuwa kinga; uamuzi wake ulikuwa wa uhakika na uelewa wake haukuyumba. Maysara pia alimwambia Khadija kuhusu bashasha, uungwana na kukubali madara­ka yaliyo chini ya uwezo wake, Muhammad.

Khadija alivutiwa na taarifa hiyo, na alimuuliza Maysara maswali kuhusu msimamizi wake mpya, Muhammad. Pengine Khadija hange­shangaa hata kidogo kama Maysara angemwambia kwamba Muhammad alikuwa mtu asiye wa kawaida kulinganisha na watu ambao amewaona katika maisha yake, na alikuwa mtu anayeweza kufanya mambo yasiyo ya kawaida. Siku iliyofuata, Waraqa bin Naufal alikwenda kumuona Khadija. Yeye pia alitaka kusikia habari zilizoletwa na wasafiri kutoka ng'ambo. Habari zilizomvutia yeye sana ni zile za ugomvi wa siku nyingi baina ya Falme za Ajemi na Roma.

Kila moja ya hizo Falme ilitaka kuwa na mamlaka kwenye kanda yote iliyojulikana kama "Bara lenye Neema." Pengine pia kama walivyokuwa raia wengine Waraqa aliwekeza fedha kwenye biashara ya Makka ya kusafirisha nje na kuingiza ndani ya nchi bidhaa na alitaka kujua jinsi ambavyo msafara ulifanikiwa kibiashara.

Khadija alimwambia binamu yake habari zote kama alivyozipata kuto­ka kwa Muhammad mwenyewe na Maysara. Aidha alisema kwamba msimamizi wake mpya alipata faida kubwa ambayo hakuitegemea.

Waraqa pia alizungumza na Maysara kuhusu safari na kuhusu Muhammad. Maysara, hata hivyo, alitaka kuzungumzia tu kuhusu Muhammad. Hakuna kitu kingine chochote kilichomvutia, hata hizo shughuli za biashara za kuuza na kuuziwa hakuzitia maanani kabisa..

Waraqa aliposikia taarifa hiyo ndefu inasemekana alipatwa na mawazo mengi sana. Baada ya kipindi kirefu cha kimya, alimwambia Khadija:

“Baada ya kusikia yale ambayo wewe na Maysara mmesema kuhusu Muhammad, na pia kufuatana na vile ninavyomjua, mimi ninaona kama kwamba anazo sifa zote, tabia, ishara na uwezekano wa kuwa Mjumbe wa Mungu. Hakika, inawezekana Muhammad atakuja kuwa mmoja wao katika siku zijazo."

Kwa mtazamo wa makini ndani ya giza la upagani wa Arabuni, Waraqa aliwezeshwa labda na ubashiri wake, kuona dalili ndogo za Mwanga wa Uislamu ambazo si muda mrefu zingejitokeza kwenye upeo wa macho na Muhammad ndiye ambaye angeleta Mwanga huo.

Vitabu vingi vinavyoeleza maisha ya Muhammad Mustafa, Mtume wa Uislamu (S.a.w.) vimetaja miujiza kadhaa inayodaiwa kufanywa naye wakati wa safari yake ya kwenda na kurudi kutoka Syria. A. Yusuf Ali, mtrjumi na mfasiri wa Qur'an Tukufu, ameandika ifuatavyo: "Hakuna Mtume yeyote aliyeweza kufanya mujiza wowote au kuonye­sha "Alama", bila ridhaa ya Mungu.

Ridhaa ya Mungu (Mashiyat) ni Mpango wenye hekima unaohusu dunia yote, mpango huu upo si kwa faida ya kabila, mila, kipindi au nchi moja. Mujiza mkubwa kuliko yote katika historia ni Qur'an.

Tunaweza kutambua uzuri wake na utukufu wake leo kama ambavyo walitambua watu wa zama za uhai wa Mustafa, hata zaidi, kwani jumuisho la uelewa wetu kuhusu asili na Uumbaji wa Mungu umeongezeka."

Mahali pengine A. Yusuf Ali anasema: "Dalili zilizopelekwa kwa Mtukufu Mtume Muhammad, zilikuwa:

(1) Aya za Qur'an na (2) Maisha na kazi yake, ambamo humo mpango na makusudio ya Mungu yalifunuliwa."

Inaonyesha kwamba uchangamfu na kipaji cha Muhammad pia vil­imuathiri Khadija. Kama ilivyotokea kwa Maysara, Khadija naye aliin­gia kwenye kundi la watu wanaompenda Muhammad, na ni nani awaye yeyote miongoni mwa watu ambaye angekataa kumpenda. Khadija alimfahamu Muhammad kuwa mtu mpole mwenye staha, mkimya na asiye mpinzani.

Aidha Khadija alitambua kwamba watu wa Makka walimpa jina la Sadiq na Amin. Na sasa alionyesha uwezo wake wa kuwa mfanyabiashara.

Ustadi na werevu wake vilikuwa sababu ya mtu huyo kuwa na kipaji. Tathmini mpya ya Khadija kuhusu Muhammad, ni kwamba mtu huyu hakuwa mwenye masihara bali alikuwa na uwezo wa kufanya mambo.

Tathmini hii ilimshawishi Khadija kufanya uamuzi wa kumwajiri Muhammad kuwa Meneja wa biashara yake kwenye misafara yote ya baadaye.
Msafara wa kibiashara wa Muhammad kwenda Syria ulikuwa ndio chanzo cha ndoa yake na Khadija.

Mtarjumi na mfasir wa Qur'an Majid, A. Yusuf Ali, anauliza swali: "Tunaweza kushangaa jinsi Yakuub alivyokutana tena na mwanawe Yusuf, au jinsi Musa alivyokutana na Harun, au jinsi Muhammad Mustafa alivyokutana na Bibi Khadija?"

La. Hatuwezi kushangaa. Ilikuwa ni amri ya Mwenyezi Mungu kwam­ba watumishi wake wawili- Muhammad na Khadija wangekutana kati­ka ndoa, na walioana.

Kuna taarifa isemayo kwamba mmoja wa marafiki wa Khadija alikuwa anatoka kwenye ukoo bora wa Makka jina lake Nafisa (au Nufaysa) binti Mumyah. Mwanamke huyu alikuwa na habari kwamba Khadija alikwisha kataa posa nyingi za ndoa. Alikuwa anashangaa kama pange­tokeza mtu katika Bara Arabu ambaye angekuwa wa kiwango alichoafi­ki Khadija. Marafiki hawa wawili walilizungumzia jambo hili mara nyingi.

Hatimaye, Nafisa alifanya mazungumzo ya mara ya mwisho kuhusu jambo la ndoa yake Khadija na akapata kutambua kwamba rafi­ki yake (Khadija) hakujali utajiri, cheo au uwezo wa mume mtarajiwa. Nafisa alijua kwa hakika kwamba rafiki yake Khadija alitaka kuolewa na mtu mwenye tabia nzuri, tabia inayokubalika. Khadija alitaka kuole­wa na mwanamume mwenye maadili mema na msimamo wa uadilifu.

Pia Nafisa (au Nufaysa) alijua kwamba alikuwepo mtu wa aina hiyo Makka na jina lake alikuwa Muhammad.

Kuna taarifa isemayo kwamba siku moja Muhammad alikuwa anarudi nyumbani kutoka Al-Kaaba, Nafisa alimsimamisha na mazungumzo yalifanyika kama ifuatavyo:

Nafisa: Ewe Muhammad, wewe ni kijana wa kiume na bado hujaoa. Wanaume ambao unawazidi umri, wamekwisha oa na wengine wamezaa watoto. Kwa nini hujaoa?

Muhammad: Bado sina uwezo wa mali; mimi ni fukara. Nafisa: Bila kujali ufakiri wako, ungejihisi vipi endapo ungemwoa mwanamke mwenye sura nzuri, tajiri, mashuhuri na mwenye kuheshimika?

Muhammad: Mwanamke huyu anaweza kuwa nani?

Nafisa: Mwanamke huyu ni Khadija, binti Khuwaylid.

Muhammad: Khadija? Inawezekanaje Khadija kukubali kuolewa na mimi? Unajua kwamba wanaume wengi matajiri na uwezo na wakuu wa makabila wamemposa na amewakataa wote.

Nafisa: Kama wewe upo tayari kumuoa Khadija, sema hivyo, na niachie mambo mengine mimi. Nitapanga kila kitu.

Muhammad alitaka kumwambia ami wake na mlezi wake, Abu Talib, kuhusu azima ya Nafisa, na kupata ushauri wake kabla hajatoa jibu.

Abu Talib alimfahamu Khadija kama alivyokuwa anamfahamu mpwa wake. Alikubali ushawishi wa Nafisa. Hakuwa na shaka kwamba Muhammad na Khadija wangekuwa wanandoa makini. Kwa hivyo, alilibariki pendekezo la ndoa yao.

Hapo hapo Muhammad alimtaarifu Nafisa kwamba pendekezo lake limekubaliwa na hivyo amepata mam­laka ya kuendeleza mazungumzo kuhusu ndoa yake na Khadija.

Mara tu baada ya Abu Talib kuthibitisha ndoa hiyo, alimtuma dada yake, Safiya, kumuona Khadija, na kuzungumza naye kuhusu jambo hilo. Wakati huohuo, Nafisa alikwisha fanya mazungumzo ya awali, na Khadija alikuwa anategemea kupata mgeni kutoka nyumbani kwa wakwe wategemewa. Khadija alimpokea Safiya kwa uchangamfu, alimkirimu, na kumwambia kwamba yeye Khadija alimteua mpwa wake Safiya kuwa mwenzi wake wa maisha bila masharti yoyote. Safiya ali­furahishwa sana na mafanikio ya ujumbe wake. Kabla hajaondoka kurudi kwao, Khadija alimpa Safiya kanzu nzuri sana na ambayo ali­ikubali kwa furaha na shukrani nyingi.

Abu Talib aliamua kutekeleza kanuni za desturi za ndoa. Alimpa Khadija zawadi, na aliwachukuwa kaka zake, Abbas na Hamza, wote watatu wakaenda nyumbani kwa Khadija na kulifikisha pendekezo la ndoa ya mpwa wake na Khadija rasmi. Khadija alikubali zawadi ali­zopewa na Abu Talib na kama ilivyotarajiwa alikubali pendekezo la ndoa. Pande zote mbili zilikubaliana na kuweka tarehe ya harusi.

Abu Talib mwenyewe alichukuwa madaraka ya matayarisho ya ndoa ya mpwa wake mpendwa. Kwa ajili ya tukio hilo lenye baraka, Abu Talib alileta kumbukumbu zote zenye kuheshimika sana za urithi wa familia. Vitu hivi vilikuwa pamoja na joho na fimbo ya Abdul Muttalib, mare­hemu, mkuu wa kabila la Bani Hashim. Bwana harusi alivaa joho na kuishika mkononi mwake ile fimbo. Abu Talib alimvisha kichwani Bwana harusi kilemba cheusi cha ukoo wake, na alivaa pete yenye kito cha kijani kwenye kidole chake. Pete hii, ilikuwa raslimali ya Hashimu bin Abd Manaf bin Qusayy - mnamo siku za nyuma.

Harusi ilihudhuriwa na wakuu wote wa Quraysh na mamwinyi wa Makka. Bwana harusi alipanda farasi mwenye kutembea kwa majivuno, na vijana mashujaa wa Bani Hashim walitikisa Majambia yao yaliyokuwa yanameremeta juu ya vichwa vyao wakati walipokuwa wana msindikiza kutoka nyumbani kwa Abu Talib kwenda nyumbani kwa Khadija. Wanawake wa ukoo wa Quraysh walikwisha mtangulia bwana harusi, na tayari walikuwa wanakirimiwa nyumbani kwa bibi harusi.

Nyumba ya Khadija ilipambwa kwa taa nyingi sana. Ndani ya nyumba, mashada ya taa zenye mapambo yalining'inizwa kwa minyiroro ya dha­habu kwenye dari, kila shada lilikuwa na taa saba. Wageni walifika wakati giza lilianza kuingia. Msimamizi mkuu wa eneo la makazi ya Khadija aliunda kamati ya kumkaribisha Bwana harusi na wageni mashuhuri. Kamati ya makaribisho iliwaongoza wageni ndani ya nyumba kupitia kwenye lango la juu na kuingia kwenye ukumbi wenye umbo la mstatili ambao kuta zake zilibandikwa vigae na dari yake ili­pakwa dhahabu. Wageni waliketi kwenye mazulia na mito.

Kwa madhumuni ya shughuli hii maalum, Khadija aliagiza washonewe sare watu wote wa nyumbani mwake - wanaume na wanawake. Wanaume walivaa vilemba vyenye kumetameta, mashati mekundu, na walivaa mikanda (mishipi) kwenye viuno vyao yenye rangi nyeusi. Mashada ya hariri yenye rangi ya pembe za ndovu yalishikizwa kwenye vilemba. Wasichana walivalia mavazi yaliyonakishiwa kwa kutonewa dhahabu na kumetameta. Walivalia taji dogo kichwani na lulu nyingi na vito vyenye kumetameta. Nywele zao ziliporomoka hadi kwenye mabega na kutoka kwenye mabega hadi kiunoni zilisokotwa kwa lulu.

Mapambo ya chumba cha Bibi harusi yalikuwa mazuri sana, na hakika hayakuzidiwa kwa ustadi. Hariri iliyoning'inizwa na nguo iliyotariziwa kwa rangi nyingi nyororo, ilipamba ukuta; na busati, jeupe laini lili­tandikwa sakafuni. Moshi wa ubani ulichomoza kutoka kwenye chate­zo cha rangi ya fedha na almasi inayometameta, johari ya rangi ya bluu na rubi.

Khadija, bibi harusi, aliketi kwenye jukwaa lililofunikwa kwa nguo iliy­onakishiwa kwa urembo mwingi wa kufuma. Alionekana mchangamfu na kung'aa kama jua linalochomoza. Kichwani kwake alivaa taji la dha­habu na lulu yenye thamani na uzuri wa kushangaza. Gauni lake, lenye mchanganyiko wa rangi nyekundu iliyoiva na kijani, ilirashiwa dhahabu na kuwekwa mapambo ya lulu na Zamaradi. Walikuwepo wanawake wawili wa kumsaidia yeye binafsi, kila mmoja wao alikuwa amevalia taji la dhahabu, gauni la hariri lenye rangi ya zambarau, na makubazi yaliyotapakaa vito. Baada ya wageni wote kuketi kwenye nafasi zao, Abu Talib, mlezi wa Bwana harusi, alisimama na kusoma hotuba ya harusi.

"Utukufu na sifa zote ni zake mwenyezi Mungu, Muumba wa Mbingu na dunia, na shukrani zote ni Zake kwa neema Zake zote, riziki na huru­ma. Ametuleta sisi hapa duniani kutokana na vizazi vya Ibrahim na Ismael. Alitufanya sisi waangalizi wa Msikiti na kuwa viongozi wa Nyumba yake, Al- Kaaba, ambayo ni kimbilio la viumbe wake wote. Baada ya utangulizi huu Abu Talib aliendelea:

"Mpwa wangu, Muhammad bin Abdullah bin Muttalib, ni mtu mzuri kuliko wote katika jamii ya binadamu kiakili, hekima, uzao ulio safi, utakatifu wa maisha yake mwenyewe, na kwa heshima ya familia. Anazo dalili zote za mtu ambaye hatimaye atakuwa mtu mkubwa. Anamuoa Khadija binti Khuwayled kwa mahari ya vipande 400 vya dhahabu. Natangaza kwamba Muhammad na Khadija sasa ni mume na mke. Mwenyezi Mungu na awabariki wote, na Awe Mlinzi wao.”

Kwenye hotuba yake, Abu Talib alitangaza kwamba ukoo wa Bani Hashim walikuwa warithi wa Ibrahim na Ismail, na walikuwa wabebaji au wachukuaji wa urithi huo. Kwa hiyo, hawakuchafuliwa na ibada ya masanamu.

Abu Talib alipomaliza hotuba yake, Waraqa bin Naufal alisimama kuso­ma hotuba ya harusi kwa niaba ya bibi harusi. Alisema: "Sifa zote na utukufu wote anastahili kupewa Mwenyezi Mungu.

Tunashuhudia na kukiri kwamba yale ambayo umeyatamka kuhusu Bani Hashim ni kweli. Hapana mtu anayeweza kukanusha ubora wao.

Kwa sababau ya uzuri wao, tunakubali ndoa ya Khadija na Muhammad. Ndoa yao inaziunganisha familia zetu mbili na kuoana kwao imekuwa chanzo cha furaha kubwa kwetu. Enyi Walezi wa Quraysh, nawatakeni kuwa mashahidi kwamba ninaridhia Khadija kuolewa na Muhammad bin Abdullah kwa mahari ya vipande 400 vya dhahabu. Mwenyezi Mungu na ajaalie ndoa yao iwe ya furaha.”

(M. Shibli, mtaalam wa historia kutoka India, anasema kwamba mahari ya Hadhrat Khadija ilikuwa vipande 500 vya dhahabu - Siira).

Amr bin Asad, ami yake Khadija mwenye umri mkubwa, naye pia alise­ma kwenye sherehe hiyo na aliyaunga mkono, kwa maneno yake mwenyewe, yale aliyoyasema Waraqa bin Naufal. Na alikuwa yeye ambaye kama mlezi, wa bibi arusi, aliridhika na kumtoa Khadija aolewe na Muhammad bin Abd

Share this article

Comments 0

Your comment

Comment description

Latest Post

Most Reviews

MOST READ