Rafed English

Jannat na Jahannam

Jannat na Jahannam by : Amiraly M.H. Datoo

 

Utangulizi

Ingawaje Qur’an Tukufu inatujulisha vya kutosha kuhusu Jannat (Peponi ) na Jahannam ( Motoni ), vile vile tunapata habari zaidi kutoka Ahadith Qudsi zilizoletwa na Malaika Jibraili a.s. kwa Mtume Muhammad s.a.w.w. ambaye ananakiliwa na Imam Ali a.s. na Maimamu Kumi na moja a.s. waliobakia. Mtume s.a.w.w. wakati wa Me’raj aliweza kuona na kutembea Jannah au Peponi, kula matunda ndani mwake na kuangalia yale yaliyokuwamo. Vile vile alitembelea Jahannam au Motoni ambamo aliweza kuwaona wale kujionea vile wahalifu walivyokuwa wakiadhibiwa kwa madhambi yao.

Al Tirmidhi na Abu Daud wananakili Ahadith Qudsi ifuatayo kutoka kwa Mtume Muhammad s.a.w.w.:

Allah swt alipoumba Jannat na Jahannam, alimtuma Malaika Jibraili a.s. kwenda Jannat, akisema, “Angalia ndani mwake kile nilichokiwatengenezea wakazi wa humo.” Malaika Jibraili a.s. alikwenda akaangalia vizuri na kwa makini, na aliporudi kwa Allah swt alisema, “Kwa utukufu wako Naapa kuwa hakuna atakayeisikia illa atatamani kuingia humo.”

Kwa hayo Allah swt alizungushia vizuizi na magumu mbalimbali, na alimwamrisha Malaika Jibraili akaangalie vizuizi na magumu yaliyozungushiwa. Malaika Jibraili a.s. aliporudi baada ya kuyaangalia kwa makini, alimwambia Allah swt, “Kwa Utukufu wako, Naapa na kuhofu kuwa hakuna hata mtu mmoja ambaye ataweza kuingia ndani mwake.” Allah swt alimwambia, “Sasa nenda kaangalie Jahannam na yale niliyowaandalia wakazi wake.” Malaika Jibraili a.s. alikwenda na kuona tabaka moja baada ya nyingine. Aliporejea akasema,”Kwa utukufu wako, hakuna hata mtu mmoja atakayetamani kuingia ndani humo atakapoisikia.” Hapo Allah swt aliamrisha kuzungushiwa vivutio na vipotoshavyo, na kumwamuru Jibraili a.s. kurudi kuangalia tena. Aliporudi Jibraili a.s. alisema, “Kwa kiapo cha Utukufu Wako! Hakika ninahofu kuwa hakuna mtu atakayeweza kujiepusha kuingia ndani humo.”

Sasa tujaribu kuchunguza na kuelewa zaidi kuhusu sehemu hizi mbili : Jannat na Jahannam.

Jannat ni mahala ambapo kunatofautiana hali ya starehe, pema na furaha za kila aina. Si kama Jahannam ambapo ni shimo refu mno la moto mkali. Jannat ni eneo (tambarare au imeinuka kidogo), kiasi kwamba hata mito yake haivunji kuta zake bali inabubujika vyema. Kuna Jannat au Bustani zaidi ya moja. Ayah ya Qur’an ya Surah Al-Rahman (Sura 55 ) inatujulisha neno moja

Mud-haam-mataan ambayo inaelezea Bustani mbili za rangi zilizoiva za kijani, ambapo Ayah ya 62 ya Sura hiyo hiyo inatuambia “mbali na Bustani hizi mbili, zipo Bustani zingine mbili,” zikijumlisha kuwapo kwa Bustani nne kwa ujumla katika Akhera.

Bora ya Jannat ni Bustani ya Eden, au Jannat ‘Adan. Katika kitabu Lisan al-‘Arab, j.13, Uk. 99, sisi twaambiwa kuwa Jannat inamaanisha: Bustani ya miche ya matunda mbalimbali.

Jannat ‘Adan ime elezwa katika:
 

Jannat ‘Adan ime elezwa katika:

Ayah Surah   Ayah Surah
72 9- Al-Tawbah   31 18-Al-Kahf
23 13-Al-Ra’d   61 19-Al-Maryam
31 16-An-Nahl   76 20-Ta-Ha
33 35-Al-Fatir   50 38-As-Sad
8 40-Al-Ghafir   12 61-Al-Saff
8 98-AlBayyinah      

Katika ukurasa wa 279, juzuu 13 ya kitabu Lisan al-‘Arab, twaambiwa kuwa Jannat ‘Adan inamaanisha kuwa “Mahala pa milele” na “Bustani ya Kati (al-awsat).” Kitabu hicho hicho kinatutambulisha katika uk.427, juzuu ya 7 kuwa al-awsat inaweza kumaanisha kuwa: iliyo Bora.

Hakuna shaka kuwa tutaweza kuona na kupata maelezo na mafafanuzi zaidi juu ya Jannat ‘Adan kuliko kusema tu al-Firdows, Jannat au Peponi, katika Qur’an Tukufu. Hali hii inatuacha sisi kwa kudadisi kuwa mahala bora kabisa, na iliyo kuu, inayolengwa katika Jannat zote ni Jannat ‘Adan.

Peponi, au al-Firdows kama vile inavyoitwa katika Kiarabu, ni neno la kuazimwa. Waarabu aliowatokezea Mtume Muhammad s.a.w.w. walikuwa hawana itikadi ya maisha baada ya kufa, na Jannat na Jahannam. Na kwa hakika swala hili lilikua gumu kwake Mtume s.a.w.w. alipoanza kuhubiri. Sura 36, Ya-sin, Ayah ya 78 inatuelezea,

“Na akatupigia mfano, na akasahau kuumbwa kwake – akasema: “Nani atakaihuisha mifupa na hali imesagika?”

Vile vile Qur’an inatuambia katika Sura Ya-Sin, Ayah 79:

Sema: “Ataihuisha yule aliyeiumba mara ya kwanza, naye ni Mjuzi wa kila (namna ya) kuumba”.

Hata mwandishi wa kazi nzuri kabisa za Kiarabu, Lisan Al-‘Arab, hana uhakika iwapo neno hili la Firdows limeazimwa kutoka Kilatini au Kiajemi, au ni al-Majlisi, kama mwandishi huyo anavyokubali katika uk. 91, Juzuu ya 8 kati ya Juzuu 110 ya Encyclopedia – bila ya kuihesabu Juzuu ya Sifuri – ijulikanayo kwa jina la Bihar al-Anwar.

Wazo la tatu, ambalo linaweza kuwa sahihi zaidi ni kwamba inawezekana uasili wake ukawa Babilonia. Neno lingine lililotumika katika Qur’an Tukufu ni Jannat au Bustani. Lakini kwetu sisi, neno Jannat inamaanisha sana kuliko kutaja Bustani au shamba la miti ya matunda.

Waarabu kamwe hawakuwa na tabia ya kuishi katika mashamba yao ya miti ya matunda.

Majumba yao yaliyokuwa yamejengwa kwa udongo uliochomwa au uliokaushwa kwa jua, walikuwa wakiishi kwa kujumuika katika mashamba yao kama ilivyo katika suala la Jannat.

Kuwapo kwa Mayahudi wengi katika mji wa Madinah ( walikuwa wengi zaidi kwa kutokana na hali ya hewa ) na wakazi wa Makkah waliwakubalia Mayahudi kuchangia katika baadhi ya maneno kama hayo. Jahannam linatokana na neno la Kihibrew Gehinnom (kwa mujibu wa Oxford English Dictionary (GED), jina lake kwa kikamilifu katika Kihibrew ni ‘ge hen Hinnom’, Bonde la mto wa L - Linnom, ikielezea mahala karibu na Jerusalem ambapo kwa mujibu wa Jeremiah 19: 5, watoto walichomwa moto kwa kutolewa mhanga kwa Baal, mungu mwenye uwezo wa kuzalisha wa makafiri wa Canaaniti au kwa Molech (Moloch). Kwa habari zaidi unaweza kurejea II Wafalme 23:10 na Jeremiah 32:35 katika Biblia) (Kilatini Zehenna), Jahannam, ni lingine.

Swala hili linaweza kujitosheleza kuandika kitabu kikubwa sana ambapo si makusudio yetu hapa, hivyo kwa mukhtasari sana tuangalie milango yake ya kuingilia kama ilivyoonwa na Mtume Muhammad s.a.w.w. ambaye ananakiliwa katika Bihar al-Anwar j. 8, uk. 144, akielezea kama ilivyofikishwa na Abdullah ibn Mas’ud kama ifuatavyo:

“Wakati Allah swt aliponiruhusu kwenda Jannat, Jibraili a.s. aliniambia, “Mimi nimeamrishwa kukutembeza na kukuonyesha yote yaliyomo ndani mwa Jannat na Jahannam.” Hivyo mimi niliiona Jannat na baraka na mema yote yaliyokuwamo na vile vile nimeiona Jahannam pamoja na mateso yote yaliyomo.

Jannat inayo milango minane, kila mlango inayo misemo minne, ambayo kila mojawapo ni bora kuliko ulimwengu mzima na kile ambacho kipo ndani mwake ni kwa ajili ya wale wanaotafakari na kufuatilia kwa kutenda kimatendo.

Na Jahannam inayo milango saba, na kila mlango inayo misemo mitatu, ambapo kila msemo ni afadhali kuliko dunia yetu hii na kilichomo ndani mwa kila msemo ni kwa ajili ya kutafakari na kuyatendea kazi. Malaika Jibraili a.s. aliniambia, “Ewe Muhammad ! Soma yaliyoandikwa katika milango hizi !” Na hivyo mimi niliyasoma yote.

Milango ya Jannat

Katika mlango wa kwanza wa Jannat kumeandikwa: Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi;

zipo njia mbalimbali za kujipatia kila kitu, na njia za kujipatia riziki ni nne : kutosheleka, kutumia katika njia sahihi, kukana kisasi na kufanya uhusiano pamoja na watu walio okoka yaani wako katika njia nyoofu.

Katika mlango wa pili wa Jannat kumeandikwa: Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi;

zipo njia mbalimbali za kujipatia kila kitu, na na njia za kujipatia furaha katika maisha ya Aakhera ni nne : Kuonyesha huruma kwa mayatima, kuwawia wema wajane, kuwasaidia wacha-mungu katika kufanikisha malengo yao na kuwaangalia na kuwasaidia masikini na wasiojiweza.

Katika mlango wa tatu wa Jannat kumeandikwa: Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi;

zipo njia mbalimbali za kujipatia kila kitu, na njia za kujipatia siha njema katika maisha haya mafupi ni nne : Kuongea kwa uchache, kulala kidogo, kutembea kidogo na kula kidogo.

Katika mlango wa nne wa Jannat kumeandikwa : Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi;

Yeyote yule amwaminiaye Allah swt na siku ya Qiyamah basi lazima awe mkarimu kwa wageni wake; Yeyote yule amwaminiaye Allah swt na siku ya Qiyamah basi lazima awe mkarimu kwa jirani zake; Yeyote yule amwaminiaye Allah swt na siku ya Qiyamah basi lazima awe mkarimu kwa wazazi wake; Yeyote yule amwaminiaye Allah swt na siku ya Qiyamah basi lazima awe ni mwenye kusema mema au anyamaze kimya.

Katika mlango wa tano wa Jannat kumeandikwa: Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi;

Yeyote yule ambaye hataki kunyanyaswa siku ya Qiyamah, basi naye asimnyanyase mtu yeyote; Yeyote yule ambaye hataki kusengenywa siku ya Qiyamah, basi naye asimsengenye mtu yeyote; Yeyote yule ambaye hataki kudhalilishwa siku ya Qiyamah, basi naye asimdhalilishe mtu yeyote; Mtu yeyote yule ambaye anataka kujishikiza kwa umadhubuti katika maisha haya mafupi na yale ya Aakhera, basi lazima atoe shahada kuwa : Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi.

Katika mlango wa sita wa Jannat kumeandikwa: Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi;

Yeyote yule anayetaka kaburi lake liwe pana na lenye nafasi ya kutosha (na lisimbane) basi ajenge Misikiti; Yeyote yule anayetaka wadudu na minyoo ya ardhini wasimle, aifanye Misikiti iwe nyumba yake

(yaani awe akiizuru kwa mara nyingi kama kwamba anaishi humo );

Yeyote yule anayetaka kubakia freshi, (yaani asipate shida na taabu za kiu katika maisha haya na ya Aakhera ambapo kila mtu atakuwa akitafuta hata tone moja la maji ) basi awe akifagia Misikiti;

na yeyote yule ambaye anataka kuiona nafasi yake pale Jannat basi atengeneze sakafu na kuweka mazulia au mikeka katika Misikiti.

Katika mlango wa saba wa Jannat kumeandikwa: Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi;

Moyo halisi unapatikana kwa mema manne : Kuwatembelea wagonjwa, kutembea nyuma ya jeneza, kununua sanda kwa ajili ya maiti na kulipa madeni.

Katika mlango wa nane wa Jannat kumeandikwa: Hakuna mungu mwingine isipokuwa Allah swt tu; Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ni Mtume Wake; Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. ni mja (Walii) Wake halisi;

Yeyote yule anayetaka kuingia katika mlango huu basi lazima awe na sifa nne zifuatazo: Ukarimu, adabu njema, moyo wa kujitolea na kujiepusha katika kuwadhuru waja wa mungu.

Al-Majlisi, katika uk. 131, j. 8, ya kitabu chake kiitwacho Bihar al-Anwar, ananakili uk. 39, j. 2, ya AI-Kaisal, ambapo Ubayy anamnakili Sa’d anayemnakili al-Barqi akimnakili babake akimnakili na kuthibitisha kuwa ibn al-Nasr akimnakili ‘Amr ibn Shemr akimnakili Jabir ibn Abdullah al-Ansari akimnakili Imam Ja'fer al-Sadiq a.s. akisema, "Fikirieni kuhusu Allah swt kwa bora ya mawazo yenu, na mjue kuwa Jannat inayo milango nane na upana wa kila mlango ni upana wa miaka arobaini.

Katika hotuba mbalimbali katika Nahjul Balagha, Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. anazielezea kwa undani na mapana sana kuhusu Jannat na Jahannam; hapa ninawadondoshieni machache ya vile anavyoelezea Jannat :

“Kipeo cha furaha na mustarehe na pongezi au hongera inatofautiana sana baina ya mtu mmoja na mwingine au mahala moja na nyingine; starehe zake kamwe haziishi; wale waliobahatika kuingia na kuishi humo kamwe hawafukuzwi au kuhamishwa, na kamwe hawapatwi na uzee, na kamwe hakuna anayeambukizwa ugonjwa wa ubakhili (Hotuba nambari 85). Wao hawajivuni wala kujigamba wala kamwe hawazaliani watoto. (Hotuba nambari 161).

Hakuna anayeingia Jannat isipokuwa wale ambao wanao uelewano mwema (na kufuata nyayo zao) pamoja na Ma-Imamu a.s. kutokea kizazi cha Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. na ambao ndio waliothibitishwa ndivyo katika Siku ya Qiyamah (Hotuba nambari 152).

Iwapo utaingiwa na imani kwa kile utakachoelezewa kuhusu Jannat, basi nafsi yako itajitoa mbali na mavutio ya macho na mapotoshi ya duniani humu (ambayo yanafurahisha macho tu) utashangazwa kuona vile miti ilivyopangwa katika mistari na mizizi yao ikiwa imefukiwa katika marundo ya maski (mishki) katika mwambao wake. Matunda yao yanaweza kuchumwa kwa urahisi. Wakazi wake wanakarimiwa kila wakati kwa vinywaji vya asali halisi na mivinyo mbalimbali, ambayo haileweshi ulevi, wakazi wa humo watakuwa wakistarehe katika majumba yao ya fakhari. Itakuwa imeezekwa kwa ‘Arshi-ilahi (mbingu ya Allah swt); starehe zake ndizo nuru, na wakazi ndani ya Jannat huwa mara kwa mara wakitembelewa na Malaika wa Allah swt.

Raha na furaha kubwa kwa ajili ya wakazi wa Jannat itakuwa ni kule kuwa karibu na Allah swt na watakuwa na mawasiliano naye kwa ukaribu zaidi. Allah swt atakuwa akiongea nao kama vile mwenyeji anapokuwa akizungumza na wageni wake.

Katika uk. 114, j. 8, ya kitabu chake Sahib, al-Bukhari anamnakili Ma’ath ibn Asad akimnakili Abdullah akimnakili Malik ibn Anas akimnakili Zayd ibn Aslam akimnakili ‘Ata ibn Yasar akimnakili Abu Sa’eed al-Khudri, Allah swt awe radhi nae, akimnakili Mtume wa Allah swt akisema kuwa Allah swt atawahutubia wakazi wa Jannat kwa kusema:

“Enyi watu wa Jannat! nao watamjibu Allah swt kwa kusema, “Labbayk Mola wetu! Kwa furaha Yako!”

Na hapo ndipo atakapowauliza, “Je mmetosheka na kuridhika?” Nao watamjibu, “Je kweli itawezekanaje sisi tusitosheke na kuridhika wakati ambapo ulichotupatia sisi haujawapatia viumbe vyako vingine?” Hapo atasema, “Mimi nitawapatieni mema zaidi ya hayo,” nao watasema, “Ewe Mola wetu ! Je ni jambo gani lililobora zaidi ya hayo ?” Allah swt atasema, “Mimi nitawateremshieni rehema na baraka zangu ziwe juu yenu, na kamwe sitawaghadhabikieni.”

Mwandishi huyu huyu, katika Sura juu ya Tawhid, anamnakili Muhammad ibn Sinan akimnakili Fulayh akimnakili Hilal akimnakili ‘Ata ibn Yasar akisema kuwa siku moja Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. alikuwa akisema hadith na katika kikao hicho, alikuwepo bedui mmoja. Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. alisema kuwa Bedui mmoja miongoni mwa wakazi wa Jannat alimwomba ruhusa Allah swt kwa ajili ya kutaka kulima ardhi, ambapo Allah swt alimwuliza, “je! hukupata chochote kile ulichokihitaji (kutokea miti na mimea ya humu Jannat?). ”

Mbedui huyo alijibu, “Naam (nimepata kila kitu nilichokuwa nimekihitaji, lakini bado ninapendelea kulima ardhi.” Kwa hayo Allah swt alimruhusu kufanya hivyo; basi alipanda mbegu ardhini na katika sekunde chache tu zikaota na zikawa miti na kukomaa na kutoa matunda mengi mno kama milima. Kwa hayo ndipo Allah swt alipomwambia, “Chukua, Ewe mwana wa Adam, kwani hakuna kinachoweza kukuridhisha wewe!” Kwa kusikia hayo, yule Mbedui aliyekuwa ameketi anayasikia hayo, akainuka na kusema, “Ewe Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w.! Mtu huyo bila shaka alikuwa akitoka Quraish au kutokea Ansar, kwani wao ndio wakulima ambapo sisi Mabedui si wakulima.” Kwa kuyasikia hayo, Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. alionyesha tabasamu.

Tabia na shauku ya kukusanya na kulimbikiza ipo katika mishipa ya wanadamu, al-Tirmidhi, katika uk. 89-90, J. 2, ya kitabu chake Jami’, anainakili hadith ya Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ambapo anawajulisha Ma-Sahaba kuwa wakazi wa Jannat watakuwa wakijumuika kila mara humo katika karamu mbalimbali kama ukumbusho wao walivyokuwa wakizipitisha Ijumaa wakati wakiwa humu duniani, nao watakuwa wakienda bazaar (masoko au gulio) ambapo watakuwa wakijichagulia nguo, vitu vya thamani au chochote kile watakachokuwa wakikitaka na kuvichukua katika makazi yao.

“Bustani ya Eden,” yaani Jannat ‘Adan, imetajwa katika Qur’an katika mahala pengi zaidi ya moja. Kwa mujibu wa Ibn Mas’ud, ni sehemu ambayo iliyopo katikati ya Jannat. Kwa mujibu wa al-Dhahhak, ni mji uliopo ndani ya mji, ambamo wakazi wake ni Mitume a.s., Mashahidi, na ma-Imamu a.s. watakuwa wakiishi huku wamezungukwa na wengine. Majengo yake yamejengwa kwa jawhari, Lulu, na vito vyenye thamani, dhahabu, almasi, fedha na kuvikwa kwa muski, na kwa mujibu wa Muqatil na al-Kalbi, hewa nzuri na baridi itakuwa ikipepea kutokea ‘Arsh ikiitumbukiza katika (kama ukungu wa ) mushk nyeupe. Hata Ibilisi, shaytani, aliwaonea wivu wanaadamu kwa sababu ya Bustani ya ‘Eden.

Katika ukurasa wa 115 wa kitabu Al-Mahasin, Muhammad ibn Qays anamnakili Imam Abu Ja’fer al-Baqir a.s. akisema kuwa, “Siku moja Shaytani alimwona Mtume Nuh a.s.akisali, basi Shaytani alimwonea wivu Mtume Nuh a.s. na hakuweza kujizuia, akasema. “Ewe Nuh! Allah swt aliyetukuka, Mkuu, amejenga mwenyewe Bustani ya Eden, akapanda miti na kutiririsha mito ndani mwake. Na kisha akaangalia mandhari hayo na kusema, “Kwa hakika waumini na waongofu ndio washindi! La, Kwa Utukufu wangu! Mtu mwenye utovu wa adabu (mwenye madhambi) kamwe hataingia kuishi humu.’”

Aina za vyakula na vinywaji vinazungumziwa na kutajwa katika Qur’an na Sunnah, na vile vile hur al-‘ayn, wanawake wenye macho makubwa ndio watakaokuwa wake wa wale waliobahatika, lakini hapa mtu anaweza kujiuliza swali bila ya kujizuia:

Je, ni kitu gani kile kitakachowafurahisha mno wakazi wa Jannat?

Je, yatakuwa ni vinywaji, vyakula, sauti kama za muziki zitokanazo na matawi na majani ya miti ya Jannat , au nyimbo zitakazokuwa zikiimbwa na hawa hur al-‘Ayn ama mmoja mmoja au kimakundi, zitakazokuwa zikimsifu Allah swt na kumtukuza ?

Katika Tafsiri ya Tafsir, al-’Ayyashi, kama ilivyoandikwa katika uk. 139, J. 8, ya Bihar al-Anwar, anamnakili Abu Baseer akimnakili Abu Abdullah Imam Ja’fer al-Sadiq a.s. akisema, ‘Wakazi wa Jannat watastarehe vyakula na vinywaji zaidi kuliko masuala ya kujamiiana.”

Katika ukurasa wa 438-439 ya kitabu cha Ali ibn Ibrahim Tafsir, kama ilivyonakiliwa katika uk. 120-121, J. 8, ya al-Majlisi Bihar al-Anwar, imeelezwa kuwa Ibn Abu ‘Umayr anamnakili Abu Busayr kuwa yeye alimwuliza mara moja Abu Abdullah Imam Ja’fer al-Sadiq a.s. kuchochea hisia zake za matamanio kuhusu Jannat, Imam a.s. alimjibu, “Ewe Abu Muhammad ! Je! kunaweza kuhisiwa manukato mazuri kabisa ya Jannat hata kutokea mwendo wa maelfu ya miaka, na makazi patakatifu katika Jannat ni yale ambapo Majini na wanadamu watakwenda; humo watahudumiwa vyakula na vinywaji vya kila aina bila ya kupungua au kuisha kwa kitu chochote kile.

Bora miongoni mwa wakazi za Jannat ni yule ambaye, atakapoingia katika mabustani yake, ataona mabustani matatu (na wala si bustani moja) iliyojaa wanawake, wajakazi, mito na matunda ya kila aina ambayo yatafurahisha macho na moyo wake kwa furaha isiyoelezeka. Mtu huyo atakapokamilisha kumshukuru na kumtukuza Allah swt, yeye ataambiwa kukiinua kichwa chake kwa ajili ya kuiangalia Bustani ya pili, kwani kutakuwamo yale yasiyokuwamo katika Bustani ya kwanza.

Kwayo, atamsifu na kumtukuza Allah swt na kumwomba, “Ewe Mola wangu! Ninakuomba unipe Bustani hii (badala ya ile ya kwanza)! Kwa hayo Allah swt atamwambia, Iwapo nitakupa Bustani hii, basi wewe utaanza kunitaka nikupatie nyingine badala ya hii! Basi huyo mtu atasema, “Kwa hakika hii tu ndiyo ninayoihitaji, Ewe Mola wangu!” Na wakati atakapoingia humo ndani, furaha zake zitaongezeka zisizo na kifani, na atamshukuru na kumsifu na kumtukuza Allah swt, na hapo ndipo milango itakapoamrishwa kufunguliwa na ataambiwa kuinua kichwa chake.

Pale Bustani ya milele itakapokuwa wazi mbele yake, yeye ataangalia mara kwa mara kama alivyokuwa akitazama hapo awali. Wakati furaha zake zitakapokuwa zimezidi kifani, atasema, “Usifiwe Ewe Mola wangu ! Kwa hakika sifa hazina kiwango cha kukusifu kwa yale yote uliyonijaalia: Bustani na kuniepusha na Jahannam (Motoni).” Hapo, Abu Busayr hakuweza kujizuia kwa kuangua kilio, na alijikaza na akamwomba Imam a.s. amwelezee zaidi. Al-Imam Muhammad al-Baqir a.s. akaendelea kumwambia, “Ewe Abu Muhammad! Katika kingo za mito ya Jannat kuna wanawake wanaowasubiri waume zao kama vile zilvyo miti iliyoota katika mstari. Pale atakapomchukua mmoja, basi mwingine atakuwa ameshawekwa kuziba pengo hilo.”

Abu Busayr akasema, “Niwe fidia kwako! Tafadhali sana naomba uniambie zaidi!”

Al-Imam Muhammad al-Baqir a.s. aliendelea kumwambia, “Mumin ataozeshwa kwa bikira mia nane, elfu nne tayyibs (ni wanawake waliokua ama hawakuolewa ambao ni wajane wacha-mungu wema au walioachiwa na waume zao) na hur al-‘Ayn wawili.” “Bikira mia nane ?!” Abu Busayr alimwuliza Al-Imam Muhammad al-Baqir a.s. kwa mshangao mkubwa sana. “Naam. Yeye atawaona hivyo hivyo pale atakapojamiiana nao.” “Maisha yangu yawe yametolewa kwa ajili yako,” alisema Abu Busayr, “ Je hur al-‘ayn wameumbwa kwa kitu gani ?” Al-Imam Muhammad al-Baqir a.s. alimjibu kuwa wameumbwa kwa mada ya Jannat iliyoumbwa, na kuongezea, “miguu yao itakuwa ikionekana hata kama kutavishwa mavazi sabini.”

Abu Busayr alimwuliza Al-Imam Muhammad al-Baqir a.s. ,”Maisha yangu yawe fidia kwako, je wanazungumza chochote huko ?” Al-Imam Muhammad al-Baqir a.s. alimjibu, “Wao wanazungumza yale ambayo hakuna mwanadamu aliyewahi kuyasikia.” Abu Busayr aliuliza, “Je ni nini hayo ?” Al-Imam Muhammad al-Baqir a.s. alimjibu, “ Sisi tutaishi milele na kamwe hatutakufa! Sisi ni wale waliobarikiwa, hivyo kamwe hatutahangaika na kutaabika ! Sisi ni wale tuishio na kamwe hatutatengana ! Sisi ni wale wenye furaha na kutosheka, hivyo kamwe hatuna mashitaka ! Habari njema kwa wale waliokuwa wameumbwa kwa ajili yetu, na habari njema kwa ajili ya wale tuliokuwa tumeumbiwa! Sisi ni wale ambao kama tungening’inia angani, basi nuru yetu ingeling’arisha kila sehemu .’”

Ibn Qawlawayh, na vile vile al-Majlisi ambaye katika uk. 143, J. 8, ya kazi yake Bihar al-Anwar, anamnakili Sa’d akimnakili Ibn ‘Eisa akimnakili Sa’ eed ibn Janah akimnakili Abdullah ibn Muhammad akimnakili Jabir ibn Yazid akimnakili Imam Abu Ja’fer al-Baqir (as) akiwanakili Mababu zake a.s. ( yaani ma-Imamu a.s.) wakisema kuwa Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. alisema, “Mitume yote wmekatazwa kuingia Jannat kabla yangu, na mataifa yote yamekatazwa kuingia humo kabla ya waumini watufuatao sisi, Ahlul Bayt a.s., kuingia ndani mwake.” Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. amenakiliwa akisema, uk.139, J.8 ya Bihar al-Anwar, akisema, “Jannat inayo milango sabini na moja ya kuingilia : Ahlul Bayt a.s. yangu na wafuasi wao wataingilia milango sabini, wakati ambapo watu wengine wataingilia mlango uliobakia.”

Furaha nyingine ya Jannat ni kwamba kule hakuna kuzeeka kwa wakazi wa Jannat , na kamwe hawatapatwa na maumivu ya aina yoyote yale, na kamwe hawatataka kujisaidia kwa choo ndogo au kubwa; na badala yake kile wakilacho kitatoka mwilini kama jasho lenye manukato mazuri mno.

Hawatakuwa na ukiritimba wa aina yoyote ile na kamwe hawatanyimwa kitu chochote kile. Matamanio yao yatatimizwa, na furaha zao kamwe hazitaisha na kamwe hawatajisikia wanyonge wasio na raha. Tunamwomba Allah swt atuingize Jannat bila ya kujali mema kiasi gani tufanyayo, kwani Yeye ndiye pekee wakutuhurumia na kutufanyia hisani. Yeye ndiye anayetujaalia moyoni mwetu moyo wa kufanya mema: Ni yeye pekee anayetuwezesha sisi kufanya mema, na ni Yeye pekee ambaye anakubalia mema yetu na kutulipa thawabu zake, kwani ni dhahiri kuwa sisi tusingaliweza kujifanyia mema kwa uwezo wetu wenyewe. Allah swt ndiye pekee chanzo cha wema na ndiye wema pekee.

Mwishoni, kila mtu anajawa na shauku ya kujiuliza vile Jannat itakavyokuwa kwa ujumla. Kwa mujibu wa habari tulizozisoma hapo juu, kuhusu Jannat ‘Adnan inaelezwa kuwa itakuwa ni mzunguko na Bustani ya Eden itakuwa katikati ikizungukwa na Bustani zinginezo za wale waliokuwa wafuasi na wapenzi wa Ahlul Bayt a.s. ya wananyumba ya Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. na kuyafuata matendo yake, wakizungukwa na wale waliokuwa waaminifu kwao kwa maneno na vitendo, n.k.

Iwapo utaendelea kutoa hoja hiyo, iwapo upeo wa matendo na malipo yako yatakavyokuwa kidogo, ndivyo itakavyo kuwa katika Jannat na furaha zake. Ukiwa na daraja la juu basi utafaidika zaidi, na ikiwa daraja lako ni chini kidogo, basi, na starehe za huko pia zitakuwa zimepungua kidogo. Uduara unamaanisha kudumu kwa milele. Bustani hiyo inadhaniwa kuwa ni duara, lakini Allah swt ndiye ajuaye zaidi.

1. Imani na matendo mema

Kwa hakika Imani na matendo mema ndiyo masuala bora kabisa na ambayo yanamletea furaha mtu na inasadikiwa kuwa ndiyo ufunguo wa Jannat na baada yake sababu zote zitakazoendelea kuelezwa basi mutaona kuwa zote hizo ni matawi ya hoja hili na Allah swt pia anasema kuhusu Imani na Matendo mema kuwa mtu yeyote atakayetekeleza hayo humu duniani basi Allah swt lazima atamjaalia Jannat. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Baqarah ,2 , Ayah 82:

“Na wale walioamini na wakatenda mema, hao ndio watu wa Jannat , humo watadumu”.

2. Taqwa

Taqwa inamaanisha kujiepusha - yaani yale yote yaliyosemwa na Ahlul Bayt a.s. ya Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. kuwa ni halali basi ndiyo halali na yale yote yaliyosemwa ni haramu basi yawe ni haramu. Allah swt ametoa ahadi kuwa atakayeishi kwa Taqwa basi mahala pake patakuwa ni Jannat. Na hivyo ndivyo maana anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Maryam ,19 , Ayah 63 :

“Hiyo ndiyo Jannat tutayowarithisha katika waja wetu walio kuwa wachamungu”.

Vile vile twaambiwa katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Hujurat ,49, Ayah 13 :

“Enyi watu ! Hakika Sisi tumekuumbeni kutokana na mwanamume na mwanamke. Na tumekujaalieni kuwa na mataifa na makabila ili mjuane. Hakika aliye mtukufu zaidi kati yenu kwa Allah swt ni huyo aliye mchamungu zaidi katika nyinyi ...”

3. Ihsani na matendo mema

Yaani kuwafanyia watu mambo mema na matendo yetu yawe mema kwa ujumla na kwa hakika haya ndiyo mambo mema na bora kabisa na ndiyo sababu za kuingia Jannat. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Maidah,5, Ayah 85 :

“Basi Allah swt atawalipa, kwa yale waliyoyasema, Bustani zipitazo mito katika yake; humo watadumu. Na haya ndiyo malipo ya wafanyao wema”.

4. Jihadi na kuwa shahidi

Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al- Tawbah, 9, Ayah 111:

Hakika Allah swt amenunua kwa Waumini nafsi zao na mali zao kwa kuwa wao watapata Jannat. Wanapigana katika Njia ya Allah swt – wanauwa na wanauwawa. Hii ni ahadi aliyojilazimisha kwa Haki katika Taurati na Injili na Qur'ani. Na nani atimizae ahadi kuliko Allah swt ? Basi furahini kwa biashara yenu mliyofanya naye. Na huko ndiko kufuzu kukubwa.

5. Kutokufuata nafsi yake

Yaani mtu hafuati matamanio ya nafsi yake na badala yake anaikhilafu. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Naziat, 79, Ayah 40 – 41 :

“Na ama yule anayeogopa kusimamishwa mbele ya Allah swt Mlezi, na akijizuilia nafsi yake na matamanio, Basi huyo, Jannat itakuwa ndiyo makaazi yake!”

6. Kushindania katika kuleta Imani

Allah swt atuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura al- Waqia, 56, Ayah 10 – 13 :

Na wa mbele watakuwa mbele.

Hao ndio watakao karibishwa

Katika Bustani zenye neema.

7. Hijrah na Jihad

Tumeshaona kuwa Jihadi imeshatajwa hapo mwanzoni (Jihadi na kuwa Shahidi, nam. 4) hapa Jihadi imekuja lakini pamoja na Hijrah. Yaani Hijra ni Jihadi mojawapo kwa ajili ya Mumin. Tumeona kuwa Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. aliiacha Makkah na kwenda Madina, hii ilikuwa ndiyo Jihadi mojawapo ambayo ndiyo kwa ajili ya Allah swt na Dini.

Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura al-Tawbah, 9,

Ayah 20-22 :

“Wale walioamini na wakahama, na wakapigana Jihadi katika njia ya Allah swt kwa mali yao na nafsi zao, hao wana cheo kikubwa zaidi mbele ya Allah swt . Na hao ndio wenye kufuzu.

Mola wao Mlezi anawabashiria rehema zitokazo kwake, na radhi, na Bustani ambazo humo watapata neema za kudumu.

Watadumu humo milele. Hakika kwa Allah swt yapo malipo makubwa”.

8. Subira na Ustahimilivu wakati wa shida

Kufanya Subira na Ustahimilivu wakati mtu anapopatwa na shida na matatizo mbalimbali ama yakupoteza mali, kufiwa, kuugua n.k. Katika vitabu tunapata habari kuwa Mitume a.s na Maimamu a.s. pia wamepitia shida kali kali ambazo wao wamezifanyia subira na ustahimilivu kwa ajili ya furaha ya Allah swt . Qur’ani Tukufu , Sura al-Dahar, 76, Ayah 12 :

“Na atawajaza Bustani za Jannat na maguo ya hariri kwa vile walivyo subiri”.

Vile vile Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Ra’d, 13, Ayah 24 :

Hao ndio watu wa Jannat, watadumu humo, kuwa ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyatenda.(Wakiwaambia) Assalamu ‘Alaikum ! Amani iwe juu yenu, kwa sababu ya mlivyo subiri! Basi ni mema mno malipo ya Nyumba ya Akhera.

9. Kuwa imara katika Dini

Inambidi mtu awe madhubuti katika Dini kama ukuta wa Shaba yaani awe na uwezo wa kukabiliana na kila hali itakayojitokeza mbele yake kiasi kwamba kamwe hataweza kulega lega katika dini na kamwe hataweza kurudi nyuma katika msimamo wake wa Dini. Allah swt anasema katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Ahqaf, 46, Ayah 13 – 14 :

“Hakika waliosema: Mola wetu Mlezi ni Allah swt; kisha wakatengenea, hawatakuwa na khofu, wala hawatahuzunika.

10. Kumtii Allah swt na Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w.

Inatubidi sisi kumtii Allah swt pamoja na Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ili kuwa mustahiki wa Jannat. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Nisaa, 4, Ayah 13 :

“... Na anayemtii Allah swt na Mtume wake, Yeye atamtia katika Jannat zipitazo mito kati yake, wadumu humo. Na huko ndiko kufuzu kukubwa”.

11. Ikhlas (Uhalisi)

Iwapo kama hakutakuwapo na uhalisi katika kila jambo basi hakutakuwa na usahihi wa kitu au jambo hilo. Uhalisi lazima uwepo katika Imani, matendo na akili na fahamu zetu na kwa hakika huu ndio ufunguo wa kuingia Jannat na ndivyo maana Allah swt ameweka sharti hili la kumwezesha mtu kuingia Jannat na Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura al-Safaat, 37, Ayah 39 – 43 :

“Wala hamlipwi ila hayo hayo mliyokuwa mkiyafanya.

Isipokuwa waja wa Allah swt walio khitariwa.

Haom ndio watakaopata riziki maalumu,

Matunda, nao watahishimiwa”.

12. Ukweli

Kwa hakika sharti hili ni la umuhimu wa aina yake kwani kila jambo tulifanyalo linahitaji ukweli na kama hakuna ukweli basi kila kitu kitaharibikiwa. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura al-Maidah,5, Ayah 119 :

Allah swt atasema: Hii ndiyo Siku ambayo wasemao kweli utawafaa ukweli wao. Wao watapata Bustani zipitazo mito kati yake. Humo watadumu milele. Allah swt amewawia radhi, nao wawe radhi naye. Huku ndiko kufuzu kukubwa.

13. Kujitakasisha mwenyewe

Inambidi kila mtu atulie na kujitakasisha nafsi yake mwenyewe kwa kila jambo na hivyo alete mapinduzi ndani mwake. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura Ta-Ha, 20, Ayah 75– 76 :

Na atakayemjia naye ni Muumini aliye tenda mema, basi hao ndio wenye vyeo vya juu.

Bustani za milele zipitazo mito kati yake,wadumu humo. Na hayo ni malipo ya mwenye kujitakasa.

14. Kutoa katika njia ya Allah swt na kuomba Tawba

Allah swt anatutaka sisi tule na tuwalishe wengine pia tuwe wakarimu na kamwe tusiwe mabakhili na tuombe Tawba kwa ajili ya madhambi yetu. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura Ali Imran, 3, Ayah 133-136 :

Na yakimbilieni maghfira ya Mola wenu Mlezi, na Jannat ambayo upana wake ni mbingu na ardhi, iliyowekwa tayari kwa wachamungu,

Ambao hutoa wanapokuwa na wasaa na wanapokuwa na dhiki, na wanajizuia ghadhabu, na wasamehevu kwa watu; na Allah swt huwapenda wafanyao wema;

Na ambao pindi wafanyapo uchafu au wakjidhulumu nafsi zao humkumbuka Allah swt na wakamwomba msamaha kwa dhambi zao – na nani anayefuta dhambi isipokuwa Allah swt? – na wala hawaendelei na waliyo yafanya na hali wanajua.

Hao malipo yao ni msamaha kwa Mola wao Mlezi, na Bustani zipitazo mto kati yake. Humo watadumu, na mwema mno ujira wa watendao.

15. Hofu ya Allah swt

Kuna msemo kwamba Mwogopeni yule mtu ambaye hamwogopi Allah swt! Na wala musimwogope yule mtu ambaye anamwogopa Allah swt! Kwa sababu yule mtu ambaye anamwogopa Allah swt kamwe hatakudhuru nyuma yako na atakuwa akijua kuwa Allah swt hatafurahishwa na hatua yoyote ile ya kukuletea madhara. Ndiyo maana tunaambiwa kuwa tusiwaogope Waumini, tuongee nao waziwazi bila ya kuwa na hofu ya aina yoyote, lakini bila ya kuwatuhumu. Lakini yule asiye na hofu ya Allah swt atatafuta kila hila na mbinu za kukudhuru wewe kwa sababu hana hofu ya Allah swt. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura al-Rahman, 55, Ayah 46 :

Na mwenye kuogopa kusimamishwa mbele ya Allah swt atapata Jannat (Bustani) mbili

Vile vile nitapenda kuwaleteeni Hadith ya Al-Imam Ja’afar as-Sadiq a.s. amesema katika Majma’ul Bayan :

“Mtu yeyote ambaye anajua na kutambua wazi kuwa mimi nifanyapo jema au baya, basi Allah swt yupo anashuhudia matendo yangu haya, basi mtu kama huyu daima atakachokuwa akikifanya basi atakuwa mwangalifu mno katika matendo yake na atajiambia kuwa lau nitafanya kazi hii njema basi Allah swt atalipa mema kadha na kadha na lau nitafanya maasi na madhambi, basi Allah swt ataniandikia adhabu kadha wa kadha. Kwa hivyo watu kama hawa wamewekewa Bustani mbili katika Jannat.”

16. Tawalla na Tabarra

Ama kuhusu mtu atakaye fuata masuala haya mawili basi Allah swt atamjaalia Jannat na uthibitisho wake ni kwa mujibu wa Qur’ani Tukufu, Sura al-Mujadilah, 58, Ayah 21:

Allah swt ameandika: Hapana shaka Mimi na Mtume wangu tutashinda. Hakika Allah swt ni Mwenye nguvu, mwenye kushinda.

Tawalla maana yake ni kuwa rafiki wa Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. na Ahl al-Bayt a.s. na Tabarra ina maana ya kujiepusha na kujiweka mbali na kutokuwa na uhusiano wowote na maadui wa Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. pamoja na maadui wa Ahl al-Bayt a.s.

17. Kudumisha Sala

Katika maana yake ni kwamba inambidi kila Mwislamu awe akisali sala zote zilizofaradhishwa juu yake kwa kuzingatia umuhimu na nyakati zake. Zipo Sala nyingi ambazo tumefaradhishiwa katika Islam kwa mfano Sala tano za siku, Sala za matukio kama mitetemeko, kupatwa kwa jua au mwezi, n.k. (rejea vitabu vya fiq-hi). Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura al-Ma’arij, 70, Ayah 22 -34:

Isipokuwa wanaosali,

Ambao wanadumisha Sala zao,

Na ambao katika mali yao iko haki maalumu

Kwa mwenye kuomba na anayejizuilia kuomba;

Na ambao wanaisadiki Siku ya Malipo,

Na ambao wanaiogopa adhabu itokayo kwa Mola wao Mlezi.

Hakika adhabu ya Mola wao Mlezi si ya kuaminika nayo

Na ambao wanahifadhi tupu zao.

Isipokuwa kwa wake zao, au iliyo wamiliki mikono yao ya kuume, basi hao hawalaumiwi –

Lakini wanaotaka kinyume ya haya, basi hao ndio wanaoruka mipaka.

Na ambao wanazichunga amana zao na ahadi zao,

Na ambao wanasimama imara katika ushahidi wao,

Na ambao wanazihifadhi sala zao.

Hao ndio watakao hishimiwa Jannat.

Maelezo juu ya Jahannam ( Motoni )

Waislamu wanatimiza nguzo ya Saumu kwa sababu waweze kuepukana na adhabu za Jahannam . Je, Jahannam ni mahala pa namna gani na humo kuna adhabu za aina gani ?

Kumeandikwa vitabu vingi vikizungumzia swala hili. Qur’an Tukufu inayo maelezo ya kutosha yanayozungumzia mateso na adhabu za kiakili na kimwili kwa ajili ya wale watakaoingizwa humo kwa kutokana kwao kutoishi vile alivyotaka Allah swt, kwa sababu wao hawakutimiza ahadi yao pamoja na Allah swt alivyokuwa amewapa, ambao hawakutimiza makusudi ya kuumbwa kwao yaani kumwabudu Allah swt na si mwingine.

Adhabu kama hizo zinaweza kuangaliwa na kurejewa katika Surah zifuatazo :

al-Baqarah,Aali-’Imran, al-Maaida, al-An’am, al-A’raf, al-Anfal, Younus, Hud, al-Ra’d, al-Hijr, al-NahI, Maryam, Taha, al-Hajj, al-Muminoon, al-Noor, al-Furqan, al’Ankabut, Luqman, al-Sajdah, al-Ahzab, Saba, al-Zumar, al-Ghafir, al-Tur, al-Hashr, al-Ma’arij, al-Buruj, al-Fajr, al-Nisaa..., Katika Surah nyingi, kwa hakika Qur’ani imeteremka kuwaonya wanaadamu dhidi ya moto wa Jahannam na kuwaelekeza katika furaha ya kudumu milele : Ufalme usiokwisha kamwe.

Je, Jahannam ina umbo gani la kuonekana ? Tupitie Ayah ya Qur’an Tukufu Surah ya Al-Balad, 90, Ayah ya 19-20 zisemazo :

Lakini waliokanusha Aya Zetu, hao ndio watu wa upande wa shari. Moto uliofungiwa (kila upande) utakuwa juu yao.

“Kufungiwa inamaanisha kufunikwa; Jahannam inaweza kulinganishwa kama mtungi, wenye kifuniko, juu ya jiko, kwamba chungu kinachomwa ndani na nje. Maana itakuwa wazi zaidi tusomapo Ayah zifuatazo za Qur’ani Tukufu Surah al-Humazah, 104, Ayah 5 – 9 :

Hasha! Bila shaka atavurumizwa katika (Moto unaoitwa) Hutama. Na ni jambo gani litakalokujulisha (hata ukajua) ni nini (Huo Moto unaoitwa ) Hutama ? Ni Moto wa Allah swt uliowashwa (kwa ukali barabara ). Ambao unapanda nyoyoni. Hakika huo (Moto) watafungiwa (wewemo ndani yake ). Kwa magogo marefu marefu

“Kufunikwa juu yao” inamaanisha sawa na vile ilivyo katika Ayah ya 90 : 20 hapo juu. Na mistari yake inaweza kumaanisha kwenda undani zaidi, na mistari hiyo ‘inaongezeka,’ kiurefu, na kwa hakika Allah swt ndiye ajuaye zaidi.

Je miale ya moto wa Jahannam iko yenye ukubwa kiasi gani ? Jibu lake tunapewa na Muumba wetu na Jahannam Qur’ani Tukufu Surah al-Mursalat, 77: Ayah ya 32: "Hakika (Moto huo) hutoa macheche yaliyo kama majumba."

Milango ya Jahannam

Katika mlango wa kwanza wa Jahannam kumeandikwa sentenso tatu: Yeyote yule atakayekuwa na matumaini katika Allah swt basi daima atakuwa mtu mwenye furaha na mafanikio; Yeyote anayekuwa na khofu ya Allah swt basi anajaaliwa usalama; mtu mwovu na aliyepotoka na mstahiki wa adhabu za Allah swt ni yule ambaye hana matumaini yoyote kwa Allah swt na wala hana khofu ya aina yoyote ile ya Allah swt.

Katika mlango wa pili wa Jahannam kumeandikwa yafuatayo: Yeyote yule asiyetaka kufanywa uchi Siku ya Qiyama, basi awavalishe nguo wale walio uchi humu duniani, Yeyote yule asiyetaka kupatwa na kiu Siku ya Qiyamah, basi awanywishe wale wenye kiu humu duniani, Yeyote yule asiyetaka kupatwa na njaa Siku ya Qiyamah, basi awalishe wale wenye njaa humu duniani.

Katika mlango wa tatu wa Jahannam kumeandikwa : Allah swt huwalaani wale wasemao uongo, Allah swt huwalaani wale walio mabakhili, Allah swt huwalaani wale wanaowanyanyasa na kuwakandamiza wanyonge.

Katika mlango wa nne wa Jahannam kumeandikwa sentenso tatu: Allah swt humdhalilisha yule ambaye anaidharau Dini ya Islam, Allah swt humdhalilisha yule anayewakashifu Ahlul Bayt a.s. ya wananyumba ya Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w.; Allah swt humdhalilisha yule ambaye anawasaidia wadhalimu katika kuwadhulumu watu.

Katika mlango wa tano wa Jahannam kumeandikwa sentenso: Msiendekeze matamanio yenu, kwani matamanio yanapingana na tendo la kusadikisha; Musiyaongelee zaidi yale yasiyowahusu kwani mtaondoka katika Baraka za Allah swt; na kamwe msiwe wasaidizi wa madhalimu.

Katika mlango wa sita wa Jahannam kumeandikwa sentenso: Mimi nimeharamishiwa kukubalia Mujtahid (hawa ni wale ambao wamefikia upeo wa Ijtihad, uwezo wa kutoa fatwa. Rejea vitabu vya Fiqh ndipo utakapoweza kupata ilimu zaidi katika somo hili). Mimi nimeharamishiwa kukubalia wale wanaofunga saumu.

Katika mlango wa saba wa Jahannam kumeandikwa sentenso tatu: Ujihisabie mwenyewe matendo yako kabla hujafanyiwa hisabu ya matendo yako; ikaripie nafsi yako kabla wewe hujakaripiwa; na mwabudu, Allah swt aliye Mkuu na aliyetukuka, kabla ya wewe hujafika mbele yake na ambapo hautaweza tena kumwabudu na kumtukuza.

Kwa kuwa marejeo kuhusu Jahannam yapo yanapatikana kwa wingi kutoka Qur’ani Tukufu, sisi sasa tutajaribu kurejea mapokezi na maelezo kuhusu Jahannam kutokea Ahadith za Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. na Ma-Imamu a.s. kuhusu adhabu, vitisho vya Jahannam , mahala palipojaa joto la hali ya juu yenye kuumiza, mahala ambapo moto wake unawekewa vipande vya kiberiti au mrututu ambayo kila moja ni kubwa kama milima mikubwa kabisa ulimwenguni. Zipo sehemu kubwa kabisa kama hizo ambapo wale waliokwisha adhibiwa hupelekwa kupoozwa na kugandishwa kama barafu. Kwa maneno mengine, wanatolewa kutoka hali moja ya moto mkali kabisa na kupelekwa katika hali nyingine ya baridi kabisa. Katika sayari yetu kuna milima yenye theluji na milima yenye kutoa volkeno ambayo hutoa miyeyuko ya mawe kama lava; na hivyo ndivyo ilivyo hali ya Jahannam : kuna hali zote mbili za joto kali na baridi kali.

Katika uk.309 ya kitabu cha al-Selek, The Divine Traditions, mkusanyiko wa Ahadith al-Qudsi, Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. amenakiliwa akisema kuwa siku moja Jahannam ilimlalamikia Allah swt kwa kusema, : “Ewe Mola! Hata sehemu zangu zinateketezana!” na kwa hayo Allah swt aliiruhusu kupumua mara mbili, mara moja katika majira ya baridi na mara nyingine katika majira ya joto kali. Kwa sababu ya kupumua kwake huku ndiko kumetokezea misimu hii miwili yenye joto kali na baridi kali. Iwapo Allah swt angalikuwa ameruhusu zaidi ya mara mbili basi kusingalikuwapo na maisha ulimwenguni humu.

Chakula cha watu wa Jahannam na Jannat

Wakati wakazi wa Jannat watakuwa wakila kila aina ya matunda mazuri na yenye ladha tamu, wakazi wa Jahannam watakuwa wakila chakula kama miiba ambayo itakuwa ikiwasakhama katika koo zao, kamwe haitawafikia tumboni mwao, na wala hawataweza kutapika. Na hii ndiyo chakula mojawapo ya watu wa Jahannam . Aina nyingine ya chakula kinachotayarishwa kwa ajili ya wakazi wa Jahannam ni usaha wa majeraha ya wale wanaopata mateso katika Jahannam , na kuchemshwa katika joto la kupasua matumbo yao.

Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. amenakiliwa katika uk.145, J.1 ya al-Zamakhshari’s Rabee’ al-Abrar akiwa amemwuliza Malaika Jibraili a.s., “Je ni kwa nini mimi kamwe sijamwona Malaika Mikaili a.s. akicheka au kutabasamu?” Malaika Jibraili a.s. alimjibu: “Mikaili kamwe hakucheka wala kutabasamu kuanzia pale Jahannam ilipoumbwa. ” Anas, Allah swt airehemu roho yake, amenakiliwa na al-Zamakhshari akisema kuwa mfano wa kiwango kidogo kabisa cha adhabu ya Jahannam ni kama kwamba mtu anatengenezewa pea ya viatu ambavyo anapovaa bongo inachemka na kutokota. Habari zaidi kuhusu sehemu hii ya kutisha zinapatikana katika al-Zamakhshari, ambazo ni kama zifuatazo :

Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. amesema, “Katika safari yangu ya usiku wa (‘Israa), mimi nilisikia sauti kubwa mno, hivyo nilimwuliza Malaika Jibrail a.s., ‘Je sauti hii kubwa ni ya nini, Ewe Jibraili ?’ Naye alinijibu, ‘Ni jiwe lililotupwa kutokea juu kuangukia ndani mwa Jahannam , na imekuwa ikianguka kwa muda wa vipindi sabini vya baridi, na sasa ndipo ilipofika chini.”

Abu ‘Asim ‘Ubayd ibn ‘Umayr ibn Qatadah al-Laythi, Hakimu wa Makkah (d. 68 A.H.), amesema, “Jahannam hupumua mara moja kwa sababu yake Malaika na Mitume a.s. yote hutetemeka, kiasi kwamba hata Mtume Ibrahim a.s. hupiga magoti na kusema, “Ewe Mola wangu ! Nakuomba uniokoe!”

Abu Sa’eed al-Khudri amenakiliwa akisema, “iwapo milima itapigwa kwa rungu mara moja inayotumiwa na Malaika wa Jahannam , basi itavunjika vipande vipande na kuwa vumbi.”

Tawoos ibn Keesan al-Khawlani amenakiliwa akisema, “Wakati Jahannam ilipoumbwa, Malaika walishtushwa mno, na wakati nyie wanaadamu mulipoumbwa, basi walitulia.”

Al-Hasan ibn Yasar al-Basir amesema, “Kwa kiapo cha Allah swt! Hakuna hata mja mmoja wa Allah swt anayeweza kustahimili joto la Jahannam! Tumeambiwa iwapo mtu atasimama Mashariki na Jahannam ikawa upande wa magharibi na ikafunuliwa kidogo tu, basi bongo ya mtu huyo aliye Mashariki itachemka. Iwapo kama kiasi cha ndoo moja ya usaha wa Jahannam ukimwagwa juu ya ardhi hii ya dunia, basi hakuna hata kiumbe kimoja kingalibakia hai.”

Hisham ibn al-Hassan al-Dastoo’i alikuwa hazimi taa wakati wa usiku, na wakati wananyumba yake walipompinga kwa kumwambia, “Sisi hatuwezi kutofautisha baina ya usiku na mchana!” Yeye aliwajibu, “Kwa kiapo cha Allah swt! Mimi ninapozima taa wakati wa usiku, hukumbuka kiza kikali cha kaburini, na hivyo sipati usingizi.”

Adhabu katika Jahannam itakuwa kwa mujibu wa aina za madhambi zilizofanywa wakati wa maisha ya mtu humu duniani. Kwa mfano, Wale ambao walilimbikiza mapesa humu duniani bila ya kutoa Zaka na kodi zinginezo za kidini, basi hao watachomwa kwenye paji la uso kwa yale waliyoyalimbikiza, pembeni mwao, na migongoni mwao. Kwa maneno mengine, sehemu zote za mwili wao.

Abu Dhar al-Ghaffari, Allah swt amwie radhi, alikuwa akisema, “Waambieni wale ambao hupenda kulimbikiza utajiri wao kuwa watachomwa nayo juu ya paji la uso wao, pembeni mwao, na migongoni mwao hadi watakapokuwa wamejaa kwa mioto.”

Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. amesema, kama vile tuambiwavyo katika uk.243, J.8, ya Bihar al-Anwar, “Hakuna Mja wa Allah swtmwenye utajiri au mali na hataki kulipa Zaka isipokuwa kwamba atachomwa kwa vipande hivyo vya mapesa vitakavyokuwa vimepashwa moto katika moto wa Jahannam na kwamba watatumbukizwa katika adhabu hizo kuanzia juu ya vipaji vyao vya nyuso zao na migongo yao hadi pale Allah swt atakapokuwa amemaliza kupokea mahisabu na adhabu za waja wake Siku ya Qiyamah, muda ambao ni wa maelfu ya miaka kwa mujibu wa mahisabu yetu. Hapo ndipo watatumwa ama kuingia Jannat au Jahannam.”

Abu Umamah anamnakili Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. akielezea aina na vinywaji watakaopewa wakazi wa Jahannam. Anasema, “Italetwa mbele yake, naye atachukizwa nayo; na itakapoletwa karibu yake, itauchoma uso wake na kifuvu kitadondoka. Iwapo ataweza kunywa hata kidogo kutoka humo, basi matumbo yake yatakatika vipande vipande na kutokezea sehemu za nyuma ya kutokezea choo.”

Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. ameripotiwa akisema, “Sala za mtu anayekunywa pombe hazikubaliwi kwa siku arobaini; na iwapo atakufa huku pombe ikawamo tumboni mwake, basi Allah swt atamlazimisha anywe sadiid, maji yatokayo kwenye sehemu za uchi wa malaya ambayo yatakusanywa katika birika huko Jahannam na kupewa watu hawa, na kwayo matumbo na ngozi zao zitachomwa.”

Riwaya hii imeelezwa na Shu’ayb ibn Waqid ambaye anamnakili al-Husain ibn Zayd ambaye anamnakili Imam Ja’fer al-Sadiq a.s. kama ilivyoelezwa katika uk. 244, J. 8, ya Bihar al-Anwar, “Wale wenye madhambi mbali na zinaa au mauaji, watapewa vinywaji vya risasi na shaba iliyoyeyushwa”, kama vile Ibn Mas’ud anavyonakiliwa katika Bihar al-Anwar akisema.

Mujahid anasema kuwa hayo yatakuwa ni usaha na damu za wale walioadhibiwa, ambapo Ibn Jubayr anasema ni ‘maji meusi; kwani Jahannam ni nyeusi, miti yake ni meusi, na nyuso na miili ya wakazi wake pia inakuwa imegeuka kuwa nyeusi.

Hoja hii inachukuliwa na al-Dhahhak. Adhabu za ziada zitakazokuwa zikitolewa Jahannam zitakuwa za nyoka na ng’e ambao makucha yao yatakuwa, kwa mujibu wa Ibn ‘Abbas na wengineo wanaripoti hivyo, makubwa na marefu kama minazi. Nyoka watakuwa wanene kama tembo, na ng’e watakuwa wakubwa kama punda weusi. Na mara kwa mara wakazi wa Jahannam watakuwa wakipigwa vipigo kwa makonde yao kama marungu: Iwapo wao watakuwa katika tabaka za juu za Jahannam, basi vipigo hivyo vitawaangusha katika tabaka zinginezo, na kila tabaka litakuwa na joto na mateso makali kuliko tabaka lililotangulia, kwa muda wa miaka sabini. Mara watakapofikia tabaka la chini, miale mikali ya moto itawatupa tena, na vivyo hivyo itakavyokuwa itaendelea. Hakutakuwa na muda wa kuomba msamaha kwa ajili yao.

Je ni mahala gani palipo pabaya zaidi katika Jahannam?

Ibn Mas’ud na Ibn ‘Abbas wamenakiliwa katika uk.241 – 242, J.8, ya al-Majlisi Bihar al-Anwar anasema kuwa wanafiki watawekwa katika tabaka la chini kabisa la Jahannam ambapo kuna adhabu kali kuliko zote. Watafungwa katika vyumba kama majiko yaliyojaa mioto mikali.

Kwa sasa turejee Nahjul Balagha na tuangalie vile Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. anavyotupatia picha ya Jahannam, tumwombe Allah swt asitutumbukize humo :

‘Janga kubwa kwa mtu ni kule kutumbukia katika Jahannam; yeye atajihisi kuwa anachemshwa mzimamzima, na ataona mateso yake yasiyo na mwisho, na kiumbe fulani kinakoroma na kupumua, viumbe vyote vilivyo humo hukosa raha na kamwe hawapati fursa ya kupumzika, na kamwe hawatapata kupumzika kutokana na adhabu zake au mauti ya uhakika. Yeye hasinzii hata kidogo wala hakutakuwa na mapumziko katiko mateso yake: Kutakuwa na maumivu yakudumu kiasi ambacho tunamwomba Allah swt atunusuru na kutusaidia.’ (Hotuba 83).

‘Kwa hakika ni mahala pabaya kabisa kuliko sehemu yoyote ile, mahala ambapo mikono ya wakazi wake yanakuwa yamefungwa shingoni mwao, na vichwa vyao vimefungwa na miguu yao kwa minyororo na mavazi yao yametengenezwa kwa lami. Mashati yao yametengenezwa kwa moto wakati ambapo adhabu zao za moto usiozimika kamwe hazitakwisha kamwe mahala ambapo mlango wake utakuwa umejazwa watu, katika moto mkali kabisa kiasi kwamba sauti zao zinasikitisha na kutisha, na miale ya moto ikipaa na kufikia kila sehemu na wala hakuna kujitoa kutoka humo na wala hakuna muda utakaokwisha, na wala haina mwisho wake kwa wale wanaoteketezwa na kuchomwa humo.’ (Hotuba 109).

‘Joto lake ni kali mno, kufikia chini kwake ni mbali mno, sakafu yake ni chuma, vinywaji vyake ni usaha.’ (Hotuba 120)

‘Siku ya Qiyamah, madhalimu wote wataletwa bila ya kuwapo na mtu yoyote wa kuwasaidia au kuwatetea, na hivyo watatumbukizwa katika moto wa Jahannam na humo atasagwasagwa kama vile machine za kusaga zifanyavyo, hadi hapo atakapojigonga kichwa katika sakafu ya chini kabisa.’ (Hotuba 164)

‘Iwapo Malik (msimamizi wa Jahannam) atakuwa mkali, husababisha sehemu yake moja kuminyana na sehemu zingine, anapogombeza, milango yake huruka juu na chini (hutema kama volkano). (Hotuba 183)

Mazungumzo juu ya Jahannam yanatudhihirishia wazi kuwa umbali, mahala na nafasi ni vitu vya uhakika katika maisha yajayo kama vile yalivyo katika maisha yetu haya. Ushahidi wa kusema kuwa Jahannam itasogezwa au kupelekwa sehemu moja kutokea sehemu nyingine, unapatikana katika Ayah ya 23 ya Surah al-Fajr (Surah namba 89 ) na katika Ayah zinginezo pia :

Basi Siku hiyo italetwa Jahannam. Siku hiyo mwanadamu atakumbuka, lakini kukumbuka huko kutamfaa nini?

Kwa hakika wale watakaokuwa wakiihamisha Jahannam kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine kwa Amri ya Allah swt, hawatakuwa wengine isipokuwa ni Malaika ambao sisi hatuwaoni duniani humu lakini punde tutakapo kufa, tutaanza kuwaona, naomba mazungumzo haya juu ya Malaika tuyaachilie hapa kwani yatahitaji kutungiwa kitabu kingine, na kwa sasa hivi somo hili litatuchukua mbali, Insha-Allah, tutaweza kuwatungieni kitabu kingine juu ya Malaika.

Lazima ikumbukwe kuwa picha yote iliyotolewa kuhusu Jahannam hatujaelezea kuhusu mateso na adhabu yanayotokana kuwa pamoja na Mashetani, Pepo mbaya na Majini waliolaaniwa ambao wote hao watakuwa pamoja na wanaadamu waliolaaniwa. Tukiangalia mateso wanayopewa viumbe hivi, makelele yao, sehemu zao zikivutwa na kunyofolewa, na wakichunwa ngozi kutoka miili yao … yanatisha mno kama Jahannam yenyewe. Kumbuka vile Allah swt alivyomwelezea mwanadamu kuwa ameumbwa kwa ubora wote. Wanaadamu watakaotumbukizwa katika Jahannam wataelewa vyema zaidi kuliko wengine, wakati ambapo wale watakaokuwa wameongoka watakuwa wamepona uhakika wa kuteswa.

Wale ambao wamesoma masimulizi ya Saint Joan of Arc (1412 – 1431), Mfaransa mashuhuri, mbali na umri wake wa kati, aliwaongoza Wafaransa katika ushindi dhidi ya majeshi ya Waingereza huko Orleans, kumbuka kuwa yeye alikuwa ni Pepo mbaya, na anapendelea kutembea juu ya miti iwakayo moto kutokea ncha moja ya dunia hadi nyingine kuliko kuangalia tu. Sasa hebu fikiria kuwa nao hawa Pepo mbaya za milele. (Yeye haoni ajabu kutembea juu ya moto, je na wewe unao msimamo kama huo ...?)

Kwa kifupi hivyo ndivyo ilivyo Jahannam na adhabu na mateso yake. Kama tungaliweza kuangalia hata mara moja au kuwaangalia wakazi wake, basi kwa hakika tusingalijali kufunga saumu kila siku ya maisha yetu, na wala si katika mwezi wa Ramadhani tu, Mwezi wa Allah swt, mwezi wa msamaha na baraka, lakini maisha yetu yote.

1. Kufr na Nifaq

Hoja hii ipo ya kwanza katika mfululizo wa sababu za kumfanya mtu aingie Jahannam na sababu zote zifuatazo ndizo matawi ya Kufr na Nifaq na Allah swt amewafanyia makhususi Jahannam watu wenye sifa hizi mbili. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura al-Nisaa, 4, Ayah 140 :

Naye amekwisha kuteremshieni katika Kitabu hiki ya kwamba mnapo sikia Aya za Allah swt zinakanushwa na zinafanyiwa kejeli, basi msikae pamoja nao, mpaka waingie katika mazungumzo mengine. Hivyo mtakuwa nanyi mfano wao hao. Hakika Allah swt atawakusanya wanafiki na makafiri wote pamoja katika Jahannam.

Vile vile Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Nisaa, 4 , Ayah 145 :

Hakika wanafiki watakuwa katika tabaka ya chini kabisa Jahannam , wala hutompata yeyote wa kuwanusuru.

2. Kuwazuia wale wanaotenda kazi katika njia ya Allah swt

Kuna watu wengi ambao wanatabia ya kuzua uzushi na kuwazuia kwa njia mbali mbali wale wanaofanya tabia na kutenda matendo mema kwa mujibu wa Sunnah na tabia ya Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. na Ahlul Bayt a.s. kwa hivyo watu kama hawa ndio waliowekwa katika sababu ya kwanza ya kuingizwa Jahannam. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu, Sura al-Nisaa, 4 , Ayah 55 :

Basi wapo miongoni mwao walioamini, na wapo walioyakataa. Na Jahannam yatosha kuwa ni moto wa kuwateketeza.

3. Kutomtii Allah swt

Leo kila mzazi anataka watoto wake wamfuate na kumtii vile atakavyo yeye mwenyewe akiwa kama mzazi na vile vile kila atengenezacho mtu hutegemea kuwa kitu hicho kitamfaa na kumfanyia kazi kwa makusudio ya kukitengeneza na ndivyo vivyo hivyo Allah swt ametuumba sisi pamoja na viumbe vingine vyenye uhai na visivyo na uhai kwa sababu na makusudio maalumu, nayo ni utiifu kwa Amri Zake na kumfuata Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. pamoja na Ahlul Bayt a.s.

Hivyo kwa kutomtii Allah swt na Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. pamoja na Ahlul Bayt a.s. ni dhambi kuu na ndicho kitakachotutumbukiza Jahannam moja kwa moja. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Jinn, 72 , Ayah 23 :

... Na wenye kumuasi Allah swt na Mtume wake, basi hakika hao watapata Moto wa Jahannam wadumu humo milele.

Vile vile twaambiwa na Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Nisaa, 4 , Ayah 115 :

Na anayempinga Mtume baada ya kudhihirikia uwongofu, na akafuata njia isiyokuwa ya Waumini, tutamuelekeza aliko elekea, na tutamwingiza katika Jahannam. Na hayo ni marejeo maovu.

4. Kudhihaki Ayah za Allah swt

Kuna baadhi yetu tunayo tabia ya kuzifanyia dhihaka Ayah, amri na hukumu za Allah swt ambavyo ni tabia ovu kabisa na hatimaye humtumbukiza Jahannam bila ya yeye kutambua athari mbaya ya tabia yake hiyo. Upeo wetu wa ilimu na maarifa ni mdogo sana kiasi cha kutufanya sisi tukajivunia na kufanya ufakhari mbele ya Allah swt na tukajifanya hodari mbele ya maamrisho yake. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Kahaf, 18, Ayah 106 :

Hiyo Jahannam ni malipo yao kwa walivyokufuru na wakafanyia kejeli Ishara zangu na Mitume wangu.

5. Kutotumia viungo vya mwili dhidi ya Allah swt

Tunaonywa kuwa tusivitumie viungo vyetu vya mwili kama macho, mdomo, masikio, miguu na mikono, n.k. dhidi ya Allah swt katika kutenda maasi na madhambi. Tunaelewa vyema kabisa kuwa Siku ya Qiyamah viungo vyote hivi vitatoa ushahadi wa kipekee kwa kila kilichotenda humu duniani na Allah swt amesema wazi wazi katika Sura al-Ya-Sin kuwa Siku hiyo ya Qiyamah hakuna nafsi yoyote ile itakayolipwa mema au kuadhibiwa isipokuwa kwa yale waliyoyatenda tu.

Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-‘A’raf, 7, Ayah 179 :

Na tumeiumbia Jahannam majini wengi na watu. Wana nyoyo, lakini hawafahamu kwazo. Na wana macho, lakini hawaoni kwayo. Na wana masikio, lakini hawasikii kwayo. Hao ni nyama howa, bali wao ni wapotofu zaidi. Hao ndio walio ghafilika.

6. Kumtii na kumfuata Shaitani

Humu duniani watu wengi mno tumekuwa wafuasi na mashabeki wakubwa wa Shaitani kiasi kwamba hata Allah swt tumemsahau kama yupo na anayajua yale yote tuyafanyayo. Sisi tunayakimbilia kila yaliyo maovu bila hata ya kuyafikiria matokeo yao kama yatatunufaisha au kutudhuru. Na kwa hakika mambo mengi mno tuyafanyayo sisi kimatokeo ni kutudhuru tu.

Kila aina za tabia mbaya sisi tunaongoza kama kunywa pombe, bangi, madawa ya kulevya, zinaa na uasherati wa kila aina, wizi, uongo, kudhulumiana na kufanyiana khiana, n.k. na hata wengi wetu kuthubutu kusema kuwa sala, saumu havina umuhimu wowote katika Islam na maisha ya mwanadamu. Kwa hakika tunakuwa tumejawa na kasumba za Kishetani ambazo zinatuangamiza moja kwa moja. Allah swt anasema katika Ayat ul-Kursi kuwa wale wanaokufuru na wanaomfanya Shaitani kuwa kiongozi wao, basi Allah swt huwatoa katika Nuru na kuwatumbukiza katika Kiza.

Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-‘A’raf, 7, Ayah 18 :

Akasema : Toka humo, nawe umekwisha fedheheka, umekwisha fukuzwa. Hapana shaka atakaye kufuata miongoni mwao, basi nitaijaza Jahannam kwa nyinyi nyote.

7. Majivuno

Kwa hakika hii ni tabia mbaya kabisa katika maisha ya mwanadamu kwani anajiona yeye yu bora na afadhali kuliko watu wengine wote ama kwa kujivunia ilimu aliyoipata, uzuri, watoto, mali, siha, n.k. lakini yote hayo si ya kujivunia kwani vyote ni vitu vyenye kuangamia na kuisha pasi na sekunde hata moja. Mfano mtu kama huyo anaweza akaugua ugonjwa kwa muda mfupi atawehuka au akapoteza fahamu zake, hivyo akasahau yote aliyokuwa akiyajua. Vile vile mtu anayejivunia afya na mwili wake anaweza kupatwa na ugonjwa wa moyo, na akapooza mwili kiasi kwamba hata chakula analishwa akiwa amelala na anajisadia choo kidogo na kikubwa akiwa kitandani, hoi hawezi hata kujipangusa mwenyewe. Je majivuno yamekwenda wapi ? Na huu ni uatamaduni wa Shaitani ambao kwetu sisi ndio tunaouona kama ndio desturi nzuri. Mtu masikini akiketi karibu nawe, je utakuwa masikini au utajiri wako utamwendea huyo masikini ?

Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura az-Zumar, 39, Ayah 32 :

Basi ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule aliyemsingizia uwongo Allah swt na kuikanusha kweli imfikiapo ? Je! Siyo katika Jahannam makazi ya hao makafiri?

Na vile vile Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-A’raf, 7, Ayah 36 :

Na wale watakaokanusha Ishara zetu na wakazifanyia kiburi, hao ni watu wa Motoni; humo watadumu.

8. Kuwaomba msaada Wadhalimu

Kwa kutaka misaada kutoka wadhalimu kunatupeleka katika Jahannam bila kipingamizi kwani tunaelewa wazi kabisa kuwa mdhalimu (jina linajitosheleza kwa kujieleza ) ni mtu ambaye anamdhulumu mtu au watu, hivyo hakuna kheri kwao kwani watataka kila mtu adhulumiwe tu kwa njia moja au nyingine. Na kwa kumwomba yeye msaada atajenga chuki na uhasama baina ya watu ili yeye aweze kunufaika. Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Hud, 11, Ayah 113 :

Wala msiwategemee wanao dhulumu, usije ukakuguseni Moto. Wala nyinyi hamna walinzi badala ya Allah swt , wala tena hamtasaidiwa.

Vile vile Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Maidah, 5, Ayah 2 :

…. Na saidianeni katika wema na uchamungu. Wala msisaidiane katika dhambi na uadui ...

9. Kuisahau Akhera

Kwa hakika sisi binadamu tunajitumbukiza katika maasi na madhambi basi tunasahau kuwa Allah swt yupo anatuangalia na kuyajua matendo yetu yote. Na katika hali hii sisi huwa tunasahau kuwa baada ya maisha ya humu duniani na kufa kwetu, kuna Aakhera. Na kuisahau huku ndiko kunakotutumbukiza Jahannam.

Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Jathiyah, 45, Ayah 24 :

Na walisema:Hapana ila huu uhai wetu wa duniani – twafa na twaishi, na hapana kinacho tuhiliki (tuangamiza) isipokuwa dahari (huu ulimwengu). Lakini wao hawana ilimu ya hayo, ila wao wanadhani tu.

10. Kuiabudu Dunia

Sisi tumepotea kiasi kwamba dunia hii tumeichukulia kama kwamba ndipo tutakapoishi milele wakati tunawaona watu wanakufa usiku na mchana, wote hawa wanaiacha dunia kwa mikono mitupu. Wapo humo wanao bahatika sanda au kuzikwa na wengine humo wapo ambao hata sanda hawabahatiki na badala ya kuzikwa wanaliwa na wanyama na kuoza kama vile kufa maji, kuchomwa moto n.k.

Lakini haya yote tunayaona kama mzaha bila kuyatilia maanani kuwa nasi pia tuko njiani kwenda huko na tutayaacha yote humu humu duniani isipokuwa matendo yetu mema ndiyo yatakayotufaa katika safari yetu ya Aakhera. Al-Imam 'Ali ibn Abi Talib a.s. anasema Safari ndefu lakini matayarisho ya safari ni madogo. Tukiwa watumwa wa dunia basi tutatumbukia Jahannam .

Hapa Mtume Muhammad Mustafa s.a.w.w. amesema katika Mizanul Hikmah kuwa “Mapenzi ya dunia ndiyo chanzo chote cha kila aina ya madhambi.” Na vile vile Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al - ‘Asra’, 17, Ayah 18 :

Anayetaka yapitayo upesi upesi, tutafanya haraka kumletea hapa hapa tunayoyataka kwa tumtakaye. Kisha tumemwekea Jahannam ; ataingia humo hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa na kufurushwa.

11. Kulimbikiza utajiri wa mali na mapesa

Sisi wanaadamu tunayo tabia ya kulimbikiza utajiri yaani kulimbikiza mali na mapesa bila ya kujali haki zilizowekwa na Dini yetu Tukufu kama vile kutoa Zaka, Khums, Sadaqa, kuwasaidia jamaa na mayatima, wajane na wale wenye shida n.k. Kwa hakika Qur’ani Tukufu inatuambia waziwazi kuwa sisi tunapenda kujiongezea tu hadi hapo tutakapofika makaburini, kamwe hatukinai wala kutosheka, na tufikapo makaburini ndipo tutakapo amka na kuzindukana na usingizi wetu huo wa upotofu.

Allah swt anatuambia katika Qur’ani Tukufu , Sura al-Tawbah, 9, Ayah 34 – 35 :

Enyi mlioamini! Hakika wengi katika makuhani na wamonaki wanakula mali za watu kwa batili na wanazuilia Njia za Allah swt. Na wanaokusanya dhahabu na fedha, wala hawazitumii katika Njia ya Allah swt. Wabashirie khabari ya adhabu iliyochungu.

Siku (mali yao) yatakapotiwa moto katika moto wa Jahannam , na kwa hayo vikachomwa vipaji vya nyuso zao na mbavu zao na migongo yao, “Haya ndiyo (yale mali) mliojilimbikia nafsi zenu, basi onjeni (adhabu ya ) yale mliyokuwa mkikusanya.”

(Imeelezwa katika riwaya kuwa neno lililotumika katika Ayah hii ‘kanz??

Share this article

Comments 0

Your comment

Comment description

Latest Post

Most Reviews

MOST READ