Rafed English

Adhana Kwa Mtazamo wa Qurani na Sunna

Adhana Kwa Mtazamo wa Qurani na Sunna by : Sheikh Jafar Subhani

 

Kitabu ulichonacho mikononi mwako ni tarjuma ya kitabu cha Kiarabu kiitwacho “Adhana” cha Sheikh Jafar Subhani.

Kitabu hiki kinazungumzia juu ya hitilafu zilizotokea juu ya maneno yanayosomwa katika Adhana. Baadhi ya wanachuoni wanasema kwamba kuna maneno yaliyoongezwa, na wengine wanasema kuna baadhi ya maneno yaliyoondolewa. Ili kujua ukweli wa asili ya Adhana na maneno yake, mwanachuoni Sheikh Jafar Subhani amefanya utafiti juu ya sula hili na kuonesha kwa uwazi na pasina shaka yoyote juu ya asili ya Adhana na maneno yake.

Mwanachuoni huyu mtafiti ametumia vyanzo halisi na sahihi katika kulifikia lengo lake hili. Vyanzo hivyo si vingine bali ni Qur’an na Sunna, pamoja na matukio ya kweli ya kihistoria, akili, mantiki na elimu.

Kutokana na umuhimu wa maudhui hii tumeona tukitoe kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ili kutoa mwanga kwa Waislamu wazungumzaji wa Kiswahili juu ya suala hili ambalo linawatatiza na kujua ukweli wake.

Tunamshukuru ndugu yetu Ustadh Hemedi Lubumba kwa kukubali jukumu hili la kutarjumu kitabu hiki. Vile vile tunawashukuru wale wote ambao wameshiriki kwa njia moja au nyingine hadi kufanikisha kuchapishwa kwa kitabu hiki.

Ni matumaini yetu kwamba kitabu hiki kitakuwa chenye manufaa sana kwa wasomaji wetu na kuzidisha elimu yao ya Dini.

Mchapishaji:

Al-Itrah Foundation
S. L. P. 19701
Dar-es-Salaam.

Kila sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu mlezi wa ulimwengu.

Rehma na Amani zimfikie mbora wa viumbe na hitimisho la mitume wake, pia kizazi chake kitakatifu ambacho ndicho kasha la elimu yake na hazina ya mafunzo yake. Hakika Uislamu ni imani na sheria. Imani ni kuamini Mwenyezi Mungu, mitume wake na siku ya mwisho.

Na sheria ni hukumu za Mwenyezi Mungu ambazo zinajukumu la kumpa mwanadamu maisha bora na kumhakikishia wema wa dunia na Akhera.

Sheria ya Kiislamu ni ya kipekee kwa kuwa inahusika na kila jambo huku ikiweka utatuzi wa matatizo yote yanayompata mwanadamu katika sekta zote za maisha yake, hivyo Mwenyezi Mungu akasema:
 

الْيَوْمَ أَكْمَلْتُ لَكُمْ دِينَكُمْ وَأَتْمَمْتُ عَلَيْكُمْ نِعْمَتِي وَرَضِيتُ لَكُمُ الْإِسْلَامَ دِينًا

“Leo nimewakamilishieni dini yenu na kuwatimizieni neema yangu na nimewapendeleeni Uisilamu uwe dini yenu.. ( 5:3 ).

Isipokuwa kuna masuala madogo madogo ambayo wanazuoni wa sheria wameikhtilafiana kwa sababu ya kutofautiana kwao kuhusu riwaya ambazo zimenasibishwa kwa Mtume. Jambo ambalo limepelekea kutofautiana kuhusu masuala madodo madogo ya sheria.

Kwa kuwa ukweli hutokana na utafiti, basi hakika katika mtiririko wa masomo haya tumejaribu kuliweka sala hili juu ya meza ya utafiti, kwani huenda ikawa ndio njia ya kuunganisha mtazamo na kusogeza hatua katika uwanja huu. Kwani tofauti iliyopo si katika asili na misingi ya dini hata ipelekee kuwa na uadui na chuki, bali tofauti iliyopo ni kuhusu riwaya zilizonasibishwa na Mtume, nalo ni jambo dogo ukilinganisha na mambo mengi ambayo tunaafikiana kati ya madhehebu za kiisilamu. Na muongozo wetu katika njia hii ni kauli ya Mwenyezi Mungu:

وَاعْتَصِمُوا بِحَبْلِ اللَّهِ جَمِيعًا وَلَا تَفَرَّقُوا ۚ وَاذْكُرُوا نِعْمَتَ اللَّهِ عَلَيْكُمْ إِذْ كُنْتُمْ أَعْدَاءً فَأَلَّفَ بَيْنَ قُلُوبِكُمْ فَأَصْبَحْتُمْ بِنِعْمَتِهِ إِخْوَانًا

Na shikamaneni na kamba ya Mwenyezi Mungu nyote wala msifarakiane. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu, mlipokuwa maadui na akaziunganisha nyoyo zenu, hivyo kwa neema zake mkawa ndugu.” (3:103).

Ja’far Subhani
Tasisi ya Imam Sadiq ( a.s.)
Qum

Imam Ja’far Sadiq (a.s.) aliambiwa: ”Wanadai kuwa kuna mtu kati yaAnswari aliona adhana usingizini.” Imam akajibu: Wamesema uongo, hakika dini ya Mwenyezi Mungu ni takatifu zaidi ya kuonekana usingizini.”

Muhammad Al-Hanafiya amesema: ”Mmelizushia uongo jambo ambalo lina asili ndani ya sheria ya Uislamu na mafunzo ya dini yenu, hivyo mkadai eti lilitokana na ndoto aliyoiona mtu kati ya Answari usingizini mwake. Ndoto ambayo huenda ikawa ni uongo au kweli, na huenda ikawa si chochote.”

Na nafasi ya muadhuni mbele ya Allah

Adhana kilugha: Ni tangazo. Mwenyezi Mungu amesema:
 

وَأَذَانٌ مِنَ اللَّهِ وَرَسُولِهِ إِلَى النَّاسِ يَوْمَ الْحَجِّ الْأَكْبَرِ

“Na ni tangazo litokalo kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake kwa watu siku ya Hijja kubwa.”(9:3).

Maana yake ni tangazo kwa watu kutoka kwa wao wawili.

Kisheria: Ni tangazo la kuingia wakati wa Sala ya faradhi kwa kutumia maneno maalumu yaliyopokewa kwa sifa mahususi. Nayo ni kati ya amali bora ambazo humkurubisha mtu kwa Mwenyezi Mungu, na ni yenye fadhila nyingi na ujira mkubwa.

Amepokea Sheikh Tusi katika (Tahdhib) kutoka kwa Muawiya bin Wahabi, toka kwa Abu Abdillah (a.s.) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu amesema: “Atakayeadhini muda wa mwaka mmoja ndani ya mji kati ya miji ya Waisilamu basi atawajibika kupata pepo.”1

Pia amepokea toka kwa Saadil-askafu kuwa: “Nimemsikia Aba Abdillah akisema: Atakayeadhini muda wa miaka saba kwa ajili ya kupata radhi za Allah basi atakuja siku ya Kiyama akiwa hana dhambi yoyote.”2

Amepokea Swaduq toka kwa Al-Urzumiy toka kwa Aba Abdillah kuwa: “Watakaokuwa na shingo ndefu sana siku ya Kiyama zaidi ya watu wote niwaadhini.”3

Ameandika Ahmadi Muhammad Al-Barqiy katika kitabu Al-Mahasini toka kwa Jafar Al-Jaafy toka kwa Muhammad bin Ali Al-Baaqir kuwa: “Mtume wa Mwenyezi Mungu amesema: Muadhini mwenye kutaka radhi za Allah ni sawa na mpiganaji katika njia ya Allah, mwenye kupigana kati ya makundi mawili.”4

Na nyingine nyingi riwaya kama hizi zenye kuhimiza kutoa adhana huku zikiwataka watu wa tabaka zote kuitangaza, na kukerwa na kitendo cha madhaifu kuificha adhana kwa udhaifu wao.

Tumeleta uchambuzi huu kwa ajili ya kubainisha mambo mawili:

Kwanza: Hakika sheria ya adhana ni sheria ya Mwenyezi Mungu haina uingiliano wowote na mwanadamu.

Pili: Kusoma historia ya tamko la الصلاةخيرمن النوم Sala ni bora kuliko usingizi (Tathwib) katika Sala ya asubuhi. Huku tukithibitisha kuwa tamko hili si sehemu ya adhana bali liliongezwa kwa kuungwa mkono na baadhi ya watu.

Hivyo mazungumzo yatahusu sehemu mbili.
________________________
1. At-Tahdhibu: 2 /283 ?1126

2. At-Tahdhibu: 2 /283 ?1128

3. Thawabul-Amali: 52

4. Al-Mahasin: 48 Namba: 68

Nafasi ya Adhana Ndani ya Sheria ya Kiisilamu

Hakuna mwanadamu yeyote aliyehusika katika kuleta sheria ya dhana

Hakika adhana na iqama ni kati ya mambo yaliyothibiti ndani ya dini na ni alama ya dini. Mwenyezi Mungu aliyateremsha ndani ya moyo wa mbora wa mitume, na bila shaka Mwenyezi Mungu aliyefaradhisha Sala na ndiye aliyefaradhisha adhana na iqama, na hakika chanzo cha vyote ni kimoja.

Na wala hakuna mwanadamu yeyote aliyehusika katika kuleta sheria hiyo, si katika hali ya macho wala ya usingizi. Na hii ndio hali ya ibada zote ambazo mwanadamu hufanya kumwabudu muumba wake. Wala ndani ya sheria ya Uislamu hatujaona ibada ya kisheria ambayo imewekwa na mwanadamu kisha Mwenyezi Mungu akaipitisha na kuiunga mkono isipokuwa katika mambo maalumu ambayo yamewekwa na Mtume mtakasifu. Jambo linalodhihirisha hilo ni kuwa vipengele vyote kuanzia takbira mpaka tahlili vina mvuto wa kimungu na maana ya hali ya juu na ya ndani zaidi, ambayo huamsha hisia za mwanadamu na kumpeleka katika maana ya juu na nzuri zaidi ya ile iliyomo akilini mwa watu.

Hivyo laiti adhana na iqama vingetokana na chanzo kisichokuwa ufunuo wa Mwenyezi Mungu basi visingekuwa na mvuto huu wa kimungu. Hivyo Mwislamu hana njia isipokuwa ni kukubali mambo mawili:

1: Hakika sheria ya adhana na iqama inatokana na Mwenyezi Mungu, na yeye ndiye aliyemfunulia mja wake adhana na iqama, wala mwanadamu hakuhusika na lolote katika jambo hilo.

2. Kama ilivyokuwa asili ya adhana ni ufunuo wa Allah aliouteremsha katika moyo wa Mtume (s.a.w.w.) basi hivyo hivyo kila kipengele kati ya vipengele vya adhana ni ufunuo alioteremshiwa Mtume (s.a.w.w.) hivyo mwanadamu yeyote hana haki ya kupunguza au kuongeza kipengele chochote katika adhana.

Historia Ya Kuletwa Sheria Yaadhana Ndani Ya Hadithi Zaahlul-Bayt

Maimam wote wa Ahlul-Bayt wamekubaliana kuwa adhana ni miongoni mwa mambo ya ibada, hivyo ina hadhi kama vile ibada nyingine, na aliyeileta ikiwa ni sheria ni Mwenyezi Mungu. Imam aliteremka na adhana kisha akamfunza Mtume na Mtume akamfunza Bilal, wala hakuna yeyote aliyeshiriki katika kuleta sheria ya adhana. Jambo hili ni kati ya mambo waliyokubaliana maimam wa Ahlul-Bait. Na kuna riwaya na maneno yao mengi yanayothibitisha hilo, na sisi hapa tutatoa machache tu kwani: Katika cheni nzima inakutosha sehemu ya shingo .1

Amepolea Kulayni kwa njia sahihi toka kwa Zararat na Al-Fadhil, toka kwa Aba Jafari Al-Baqir kuwa alisema: Mtume alipopelekwa mbinguni alifika sehemu iitwayo Nyumba inayozuriwa (Baytul-Maamur), wakati wa Sala ukaingia hapo, Imam akaadhini na kukimu hapo Mtume akatangulia kisha malaika na mitume wengine wakapanga safu nyuma yake Muhammad ( s.a.w.w.)..

2. Pia kapokea Kulayni kwa njia sahihi toka kwa Imam Sadiq amesema: Pindi Imam alipoteremka na adhana kwa Mtume wa Allah kichwa cha Mtume kilikuwa mapajani mwa Ali (a.s.) hivyo Imam aliadhini na kukimu. Baada ya Mtume kuzinduka alisema: Ewe Ali umesikia? Akajibu: Ndiyo.. 2Akasema: Umehifadhi? Akajibu: Ndiyo. Akasema: Mwite Bilal. Hapo Ali akamwita Bilal kisha akamfundisha.3

3. Pia amepokea kwa njia sahihi toka kwa Umar bin Udheynat toka kwa Sadiq (a.s.) alisema: Kundi hili limepokea nini? Nikasema niko chini yako, ni kuhusu nini? Akasema: Kuhusu adhana. Nikasema, wao husema kuwa Ubayy bin Kaab aliiona ndotoni. Akasema: Wamesema uongo, hakika dini ya Allah ni tukufu zaidi ya kuonekana ndotoni. Akasema: Sudayri Al-Swayrify akamwambia: Niko chini yako, hebu tusimulie habari za jambo hilo. Akasema: Hakika Mwenyezi Mungu ni Mtukufu sana hivyo pindi alipompeleka nabii wake Miraji na kumfikisha mbingu ya saba. Akaendelea mpaka mwisho wa hadithi ya kwanza. 4

4. Muhammad bin Makkiy Al-Shahidu amepokea katika kitabu Ad-Dhikra toka kwa mwanachuoni wa kishia mwanzoni mwa karne ya nne - Nikimaanisha Ibnu Abi Aqiil Al-Aammaniy, kuwa alipokea toka kwa Imam Jafar Sadiq kuwa: Imam aliwalaani watu wanaodai kuwa eti nabii alichukua adhana toka kwa Abdallah ibnu Zaid, 5 Imam akasema: Ufunuo unateremka kwa nabii wenu kisha ninyi mnadai eti alichukua adhana toka kwa Abdallah bin Zaid?6

Si Shia peke yao ndiyo waliyopokea riwaya hizi toka kwa Maimam wa Ahlul-Bait. Hivyo Al-Hakimu na wengine nao wamepokea riwaya kama hizi toka kwa maimam. Zifuatazo ni baadhi ya riwaya zilizopokewa kwa njia ya masunni kuhusu suala hili

5. Al-Hakim amepokea toka kwa Sufiani bin Alayli kuwa: Yalipotokea yale yaliyotokea kati ya Hasan bin Ali na Muawiya bin Abu Sufian nilikwenda Madina nikamkuta amekaa, akasema:

Basi tukazungumzia adhana mbele yake, hapo baadhi yetu wakasema: Hakika chanzo cha adhana ni ndoto aliyoiona Abdallah bin Zaid. Hapo Hasan bin Ali akawaambia: Hakika hadhi ya adhana ni kubwa zaidi ya hilo, Jibril aliadhini mbinguni mara mbili mbili kisha akamfunza Mtume wa Allah. Akakimu mara moja moja 7 kisha akamfunza Mtume wa Allah.. 8

6. Al-Muttaqi Al-Hindi amepokea toka kwa Ashahidu Zaid bin Imam Ali bin Al-Husain toka kwa babu zake toka kwa Ali (a.s.) kuwa: Mtume alifunzwa adhana na kufaradhishiwa Sala usiku wa miraji9.

7. Al-Halabiy amepokea toka kwa Abi Al-Alaiy kuwa: Nilimwambia Muhammad bin Al-Hanafia kuwa: Sisi husimulia kuwa chanzo cha adhana hii ni ndoto aliyoiona mtu kati ya Answari alipokuwa usingizini. Akasema: Akashtuka sana Muhammad Al-Hanafia kwa hilo na kusema: Mmelizushia uongo jambo ambalo lina asili ndani ya sheria ya Uislamu na mafunzo ya dini yenu, hivyo mkadai eti lilitokana na ndoto aliyoiona mtu kati ya Answari usingizini mwake. Ndoto ambayo huenda ikawa ni uongo au kweli, na huenda ikawa si chochote. Akasema: Nikamwambia: Hadithi hii imeenea kwa watu. Akajibu: Naapa kwa Allah hili ni batili.10

8. Al-Mutaqiy Al-Hindiy amepokea toka kwenye Musnadi ya Rafiu bin Khudeyji kuwa: Alipopelekwa Mtume mbinguni alifunuliwa adhana, Hivyo Jibril akateremka na adhana na kumfunza Mtume. (Tabarani na yeye kapokea katika kitabu Al-Awsatwu toka kwa Mwana wa Omar).11

9. Inaonekana kuwa adhana ilitokana na ufunuo wa Allah hiyo ni kwa mujibu wa riwaya aliyopokea Abdul-Razaq toka kwa Atwai.12

10. Al-Halabii amesema: Zimepokewa hadithi zinazoonyesha kuwa sheria ya adhana iliteremshwa kipindi cha Makka kabla ya kuhama. Kati ya hadithi hizo ni Ile iliyomo ndani ya kitabu cha Tabraniy toka kwa Ibnu Omar. Na hapa akanukuu riwaya ya nane.13 Hii ndio historia ya adhana na kwa njia hii ndivyo sheria hii ya adhana ilivyoletwa, huku Shia wakiichukua toka chemchemu safi toka kwa watu ambao wao ndio wasiri wa Sunna ya Mtume, watu ambao mkweli hupokea toka kwa mkweli mpaka mwisho hukomea kwa Mtume . Pia riwaya nyingine zimeunga mkono jambo hili kama ulivyoona.

Jinsi Ilivyoletwa Sheria Ya Adhana

Kwa mujibu wa riwaya za Ahlu-Sunna

Kuna mambo yaliyomo ndani ya riwaya za Kisunni kuhusu jinsi ilivyoletwa sheria ya adhana. Mambo hayo hayasihi kabisa kunasibishwa na Mtume. Matokeo ya riwaya hizo ni kuwa: Mtume alikuwa akihimiza Sala ya jamaa lakini alikuwa hajui ni kwa njia gani angeweza kuwakusanya watu kwa ajili ya Sala kutokana na umbali uliopo kati ya nyumba moja hadi nyingine pia mtawanyiko uliopo kwa muhajirina na answari katika mitaa ya madina. Hivyo katika kutatua hili Mtume akaomba ushauri; ndipo aliposhauriwa mambo yafuatayo:

1. Atumie kuweka bendera pindi watu wakiiona watatangaziana wao kwa wao, lakini Mtume hakupendezwa na rai hiyo.

2. Wakamshauri atumie tarumbeta, lakini Mtume hakupendezwa na hilo.

3. Atumie kengele kama wanavyofanya wakristo. Mwanzo Mtume hakupendezwa na hilo lakini baadae akaamrisha itumike hivyo, ikatengenezwa kengele ya mbao ili iwe inapigwa ili watu wakusanyike kwa ajili ya Sala.

4. Mtume alikuwa katika hali kama hiyo ndipo alipokuja Abdallah bin Zaid na kumwambia Mtume kuwa, yeye alikuwa katika usingizi mwepesi ndipo alipokuja mtu na kumuotesha adhana.

Akasema Umar bin Al- Khattab kuwa alikuwa tayari keshaiona adhana hiyo kabla ya siku ishirini lakini alificha.

Akasema: Kisha Umar akamsimulia Mtume. Hapo Mtume akamuuliza: Ni kitu gani kilichokuzuia usinieleze?

Akajibu: Abdallah bin Zaidi kanitangulia hivyo nikaona haya. Hapo Mtume akasema: Ewe Bilal, simama na ufanye atakachokuamrisha Abdallah bin Zaid. Hapo Abdallah akamfunza Bilal na Bilal akajifunza adhana na akaadhini. Huu ni muhtasari wa yale yaliyopokewa na watu wa hadithi kuhusu jinsi sheria ya adhana ilivyoteremka, hivyo wajibu wetu sasa ni kuchambua maneno na upokezi wa riwaya. Na ufuatao ni uchambuzi wake.

Riwaya Kuhusu Jinsi Sheria Yaadhana Ilivyoletwa Ndani Ya Vitabu Tegemezi Vya Hadithi ( Sunan )

1-Amepokea Abu Daudi (202 . 275) kuwa: Ametusimulia Abadu bin Musa Al-Khataly na Ziad bin Ayyub (Na hadithi ya Abadi ndiyo timilifu) wao wawili wamesema: Ametusimulia Hashimu toka kwa Abi Bashiri toka kwa Abi Amiri bin Anasi toka kwa ami zake wa ki-Answari. Amesema: Mtume alitilia umuhimu sana Sala hivyo akawa akitafuta namna ya kuwakusanya watu kwa ajili ya Sala hapo akaambiwa: Wakati wa Sala ukiingia weka bendera, pindi watakapoiona bendera hiyo watatangaziana wao kwa wao. Lakini akupendezwa na hilo.

Akasema: Akatajiwa tarumbeta. Ziad anasema: Yaani tarumbeta la Mayahudi. Lakini hakupendezwa na hilo huku akisema: Hilo ni jambo la Mayahudi..

Akasema: Akatajiwa kengele. Akasema: Hilo ni jambo la Wakristo. Ndipo alipoondoka Abdallah bin Zaid huku akifikiria jambo linalomshughulisha Mtume. Ndipo alipooteshwa adhana usingizini. Akasema: Asubuhi mapema akaamkia kwa Mtume na kumwambia: Ewe Mtume, mimi nilikuwa katika usingizi mwepesi ndipo aliponiijia mtu na kunionyesha adhana ..

Akasema: Umar bin Al-Khattabi alikuwa tayari kesha iona adhana hiyo kabla ya siku ishirini lakini akaificha14 Akasema: Kisha Umar akamsimulia Mtume. Hapo Mtume akamuuliza: Ni kitu gani kilichokuzuia usinieleze? Akajibu: Abdallah bin Zaidi kanitangulia hivyo nikaona aibu. Hapo Mtume akasema: Ewe Bilal simama na ufanye atakachokuamrisha Abdallah bin Zaid. Akasema: Hapo Bilal akaadhini. Abu Bashiri akasema: Hapo Abu Umairi akaniambia: Answari wanadai kuwa laiti si Abdallah bin Zaidi kuwa mgonjwa siku hiyo basi Mtume angamfanya kuwa muadhini.

2- Ametusimulia Muhammad bin Mansur At-Tusi, Ametusimulia Yaqubu, Ametusimulia baba yangu toka kwa Muhammad bin Ishaq. Ametusimulia Muhammad bin Ibrahim bin Al-Harith At-Taymy toka kwa Muhammad bin Abdallah bin Zaid bin Abdallah amesema: Ametusimulia baba yangu Abdallah bin Zaid amesema kuwa: Pindi Mtume alipoamrishwa itengenezwe kengele ili ipigwe kwa ajili ya kuwakusanya watu kwa ajili ya Sala, basi nikiwa usingizini alinizunguka mtu huku akiwa amabeba kengele nami nikamwambia: Ewe mja wa Mwenyezi Mungu, je unauza kengele? Akanijibu: Unataka ufanyie nini kengele hii? Nikamjibu: Tuwaitie watu waje kwenye Sala. Akasema: Je hutaki nikufundishe njia bora kuliko hiyo?. Nikasema: Nataka. Anasema: Akasema: Uwe ukisema:
 

الله اكبر الله اكبر لااله الا الله لااله الا الله

(Allah mkubwa Allah mkubwa. Allah mkubwa Allah mkubwa. Nashuhudia kuwa hapana mola wa haki isipokuwa Allah. Nashuhudia kuwa hapana mola wa haki isipokuwa Allah. Nashuhudia kuwa hakika Muhammad ni Mtume wa Allah. Nashuhudia kuwa hakika Muhammad ni Mtume wa Allah. Njooni kwenye Sala. Njooni kwenye Sala. Njooni kwenye ushindi. Njooni kwenye ushindi. Allah mkubwa Allah mkubwa. Hapana mola wa haki isipokuwa Allah).

Akasema: Kisha akarudi nyuma kidogo na kusema: Wakati wa kukimu Sala sema:

الله اكبر الله اكبر لااله الا الله لااله الا الله

(Allah mkubwa Allah mkubwa. Nashuhudia kuwa hapana mola wa haki isipokuwa Allah. Nashuhudia kuwa hakika Muhammad ni Mtume wa Allah. Njooni kwenye Sala. Njooni kwenye ushindi. Imesimama Sala imesimama Sala. Allah mkubwa Allah mkubwa. Hapana mola wa haki isipokuwa Allah).

Nilipoamka asubuhi nilikwenda kwa Mtume na kumpa habari ya yale niliyoyaona. Mtume akasema: Inshaallah hiyo ni ndoto ya kweli, simama umfundishe Bilal uliyoyaona ili aadhini kwa namna hiyo, hakika yeye ana sauti nzuri kuliko wewe.. Nikasimama na Bilal nikawa nikimfundisha na yeye akiadhini.

Akasema: Omar bin Al-Khatabu akasikia, wakati huo alikuwa nyumbani kwake hivyo akatoka huku akiburuza joho lake na kusema: Naapa kwa yule aliyekupa unabii kwa haki ewe Mtume wa Allah, hakika mimi niliona mfano wa hili aliloliona..

Mtume akajibu: Basi kila sifa njema ni ya Allah15

Ibnu Majah ( 207 . 275) amepokea kwa njia mbili zifuatazo:

3. Ametusimulia Abu Ubaydi: Muhammad bin Maymun Al-Madaniy. Ametusimulia Muhammad Salmat Al-Haraniy. Ametusimulia Muhammad Is.haqa. Ametusimulia Muhammad Ibrahim Al-Tamimiy, toka kwa Muhammad Abdallah Zaid, toka kwa baba yake amesema: Mtume alichukizwa na tarumbeta akaamrisha ichongwe kengele ndipo alipooteshwa Abdallah bin Zaid adhana usingizini..

4. Ametusimulia Muhammad bin Khalid bin Abdallah Al-Wasatwiy. Ametusimulia baba yangu toka kwa Abdul-Rahmani Is.haqa, toka kwa Al-Zahriy toka kwa Salim, toka kwa baba yake kuwa: Mtume alitaka ushauri wa watu kuhusu namna ya kuwakusanya kwa ajili ya Sala. Wakamtajia tarumbeta lakini hakupendezwa nalo kwa sababu ya mayahudi. Kisha akatajiwa kengele nayo ikamchukiza kwa sababu ya wakiristo. Ndipo usiku huo mtu mmoja kati ya Answari akaoteshwa wito, na mtu huyo anaitwa: Abdallah bin Zaid na Umar bin Al-Khattab. Al-Zahriy akasema: Bilal akaongeza katika wito wa asubuhi :

الصلاة خيرمن النوم

(Sala ni bora kuliko usingizi). Mtume akaridhia16

Tirmidhi kapokea kwa njia ifuatayo:

5- Ametusimulia Said bin Yahya bin Said Al-Amawiy, ametusimulia Muhammad bin Is.haqa toka kwa Muhammad Ibrahim Al-Harith Al- Tamimiy, toka kwa Muhammad Abdallah bin Zaid, toka kwa baba yake. Amesema: .Tulipoamka asubuhi nilikwenda kwa Mtume na nikamsimulia ndoto yote.... mpaka mwisho.

6-Tirmidhi amesema: Hadthi hii kaipokea Ibrahim bin Saadi kwa utimilifu sana na urefu zaidi toka kwa Muhammad Is.haqa. Kisha Tirmidhiy akaongeza: Na Abdallah bin Zaid ndiye Ibnu Abdurabah. Na sisi hatujui chochote kilicho sahihi alichopokea toka kwa Mtume isipokuwa ni hadithi hii ya mpokezi moja inayohusu adhana. 17

Haya ndiyo yaliyopokewa na watu wa Sunna toka kwenye Sahihi Sita au vitabu sita huku vikiwa vina umuhimu mkubwa zaidi ya vitabu vingine vya Sunna, kama vile: Sunanil-Daramy au Ad-Darqutniy au yaliyopokewa na Ibnu Saad katika kitabu chake Twabaqat na Bayhaqiy katika kitabu chake Sunan. Kutokana na nafasi maalumu ya vitabu hivyo sita ndiyo maana tumebainisha yale yaliyomo ndani ya vitabu hivyo maarufu vya Sunna na kuacha yale yaliyomo ndani ya vitabu vingine. Hebu sasa tusome riwaya hizi kuanzia ibara (matnu) na sanadi (njia za upokezi) ili tupambanukiwe na ukweli kisha tutataja maelezo mengine yaliyomo ndani ya vitabu vingine.

Uchambuzi Wa Madhumuni Ya Riwaya

Riwaya hizi hazifai kuwa dalili kwa sababu mbalimbali:

Kwanza: Zinapingana na hadhi ya unabii Hakika Allah alimtuma Mtume ili yeye na waumini wasimamishe Sala ndani ya nyakati tofauti, hivyo asili ya suala hili inalazimu Mwenyezi Mungu amfunze Mtume jinsi ya kutimiza matakwa haya. Hivyo hamna maana yoyote Mtume kubakia hajui chochote kipindi chote hiki muda wa siku ishirini kama alivyopokea Abu Daudi katika riwaya ya mwanzo, eti abakie huku hajui ni jinsi gani atatimiza jukumu alilopewa huku akihangaika mara atumie njia hii mara njia ile mpaka akapata njia na sababu zitakazompa matumaini ya kufikia kusudio lake ilihali Mwenyezi Mungu anasema kuhusu Mtume kuwa:

وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّهِ عَلَيْكَ وَرَحْمَتُهُ

Na lau kuwa sifa fadhila ya Mwenyeezi Mungu juu yako na rehema. (4:113)..

Na makusudio ya fadhila hapa ni elimu hiyo ni kutokana na mazungumzo ya sentensi ya kabla yake: Na amekufundisha yale uliyokuwa huyajui..

Hakika Sala na Swaumu ni kati ya mambo ya kiibada na wala si kama vita na mapigano ambayo huenda Mtume akashauriana na maswahaba wake. Na wala kushauriana kwake na maswahaba katika vita na mapigano si kwa kuwa alikuwa hajui ni lipi linalofaa, bali alishauriana nao kwa ajili ya kuta ka kuvuta nyoyo zao kama anavyosema Mwenyezi Mungu:

فَبِمَا رَحْمَةٍ مِنَ اللَّهِ لِنْتَ لَهُمْ ۖ وَلَوْ كُنْتَ فَظًّا غَلِيظَ الْقَلْبِ لَانْفَضُّوا مِنْ حَوْلِكَ ۖ فَاعْفُ عَنْهُمْ وَاسْتَغْفِرْ لَهُمْ وَشَاوِرْهُمْ فِي الْأَمْرِ ۖ فَإِذَا عَزَمْتَ فَتَوَكَّلْ عَلَى اللَّهِ ۚ إِنَّ اللَّهَ يُحِبُّ الْمُتَوَكِّلِينَ

Basi ni kwa sababu ya rehema itokayo kwa Mwenyeezi Mungu ndio umekuwa laini kwao. Na lau ungeli kuwa mkali, Mwenye moyo mgumu, bila shaka wangeli kukimbia. Basi wasamehe, na waombee maghfira, na shauriane nao katika mambo. Na ukisha kata shauri basi mtegemee Mwenyeezi Mungu.. ( 3: 159)

Hivi huoni kuwa ni kuidharau dini kwa ndoto za watu wa kawaida kuwa chanzo cha amri ya kiibada iliyo muhimu sana kama vile adhana na iqama. Jambo hili linatupelekea kusema kuwa: Ndoto kuwa chanzo cha adhana ni uongo mtupu dhidi ya sheria na ni rahisi sana kusema kuwa ami zake Abdallah bin Zaid ndiyo waliyoeneza ndoto hiyo na kuipamba ili familia zao na makabila yao yapate ubora, hivyo ndiyo maana tunaona katika baadhi ya sanadi kuwa watoto wa ami zake ndio wapokezi wa hadithi hii, na yule aliyewategemea katika kunukuu basi alifanya hivyo kwa kuwadhania vizuri.

Pili: riwaya hizi kiundani zinapingana. Hakika riwaya zilizopita zinazohusu mwanzo wa adhana na jinsi sheria ya adhana ilivyoletwa kiundani zinapingana kwa sababu zifuatazo:

1. Kulingana na riwaya ya kwanza ya Abi Daud ni kuwa Umar aliiona adhana kabla ya Abdallah siku ishirini zilizopita. Lakini kwa mujibu wa riwaya ya nne ya Ibnu Majah ni kuwa aliiona usiku huo huo aliyoiona Abdallah bin Zaid.

2. Ndoto ya Abdallah ndio chanzo cha sheria ya adhana na Umar aliposikia adhana akaja kwa Mtume na kudai kuwa hata yeye aliota ndoto mfano wa hiyo hata hivyo hakuinukuu kwa Mtume kwa kuona aibu.

3. Hakika chanzo cha sheria ya adhana ni yeye mwenyewe Umar wala si ndoto yake kwa sababu yeye ndiye aliyetoa wazo la kupatikana wito kwa ajili ya Sala, wito ambao kwa ibara nyingine ndio adhana. Tirmidhi kapokea ndani ya kitabu chake (Sunan) kuwa: Waislamu walipofika Madina ...mpaka akasema: Baadhi yao wakasema: Tengenezeni tarumbeta kama tarumbeta la mayahudi. Akasema: Hapo Umar akasema: Hamumteui mtu anadi kwa ajili ya Sala? Amesema: Hapo Mtume akasema: Ewe Bilal simama na unadi kwa ajili ya Sala, yaani adhana 18 Pia hadithi hii kaipokea An-Nasaiy19 na Al-Bayhaqiy 20 ndani ya Sunan zao (vitabu vyao). Ibnu Hajari kafasiri kuwa makusudio ya wito kwa ajili ya Sala ni tamko (Salati jamia ) Wala hakuna dalili yoyote juu ya tafsiri hiyo.

4. Hakika chanzo cha sheria ya adhana ni Mtume mwenyewe. Amepokea Bayhaqiy. Wakasema wapige kengele au wawashe moto, hapo akaamrishwa Bilal aadhini mara mbili mbili na aqimu mara moja moja. Akasema: Ameipokea Bukhari toka kwa Muhammad toka kwa Abdul- Wahabi At-Thaqafy. Na ameipokea Muslim toka kwa Ishaqa bin Ibrahim 21

Je? Itakuwaje tutegemee nukuu hizi zenye kupingana kwa kiasi hiki.

5. Hakika kwa mujibu wa riwaya, kwanza ni kuwa Omar alikuwepo kwa Mtume pindi Abdallah akisimulia ndoto lakini kwa mujibu wa riwaya ya pili hakuwepo kiasi kwamba alitoka nyumbani kwake pindi aliposikia adhana ya Bilal baada ya kuwa Abdallah tayari amekwisha simulia ndoto yake.

Tatu: waotaji wa ndoto hiyo walikuwa ni watu kumi na nne, si mtu mmoja.

Kwa mujibu wa yale aliyopokea Al-Halabiy inaonekana kuwa aliyeota ndoto ya adhana si Ibnu Zaid na Ibnu Al-Khatabi peke yao bali amedai kuwa hata Abubakari aliota kwani aliona mfano wa yale waliyoyaona hao wawili. Na inasemekana kuwa na wengine saba kati ya Answari. Na inasemekana ni watu kumi na nne22 wote walidai kuwa waliiona adhana ndotoni. Sheria si matakwa ya kila mtu, hivyo ikiwa sheria na hukumu zinafuata ndoto ya kila mtu basi Uislamu umekwisha.

NNE: mgongano kati ya riwaya za Bukhari na nyinginezo

Hakika tamko la wazi la Sahihi Bukhari ni kuwa Mtume alimuamrisha Bilal atoe wito kwa ajili ya Sala wakiwa katika kikao cha ushauri. Umar alikuwepo wakati amri hiyo inatoka. Amepokea kutoka kwa mtoto wa Umar kuwa: Walipofika Madina Waislamu walikuwa wakikusanyika na wakiitana kwa ajili ya sala bila ya kuwepo wito mahususi kwa ajili ya Sala.

Hivyo siku moja wakajadiliana kuhusu suala hilo. Baadhi yao wakasema: Fanyeni kengele kama kengele ya wakristo, wengine wakasema: Fanyeni tarumbeta kama za mayahudi, hapo Umar akasema: Hivi hamumteui mtu anadi kwa ajili ya Sala? Hapo Mtume akasema: Ewe Bilal simama, hapo akanadi kwa ajili ya sala23.

Uwazi wa hadithi ya ndoto ni kuwa Mtume alimuamuru Bilal kunadi baada ya kuwa amesimuliwa ndoto na Ibnu Zaid wala Umar hakuwepo bali alisikia adhana akiwa nyumbani kwake akatoka huku akiburuza nguo yake akisema: Naapa kwa yule aliyekutuma kwa haki ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika niliona mfano wa aliyoyaona.24.

Hatuwezi kufasiri neno wito lililopokewa na Bukhari kuwa ni tamko: (salat jamia ) na neno wito lilomo ndani ya hadithi za ndoto kuwa ni adhana, kwa sababu kufanya hivyo kwanza ni kuoanisha bila dalili. Pili laiti kama Mtume angemuamrisha Bilal ainue sauti kwa kutamka: (Salat jamia) basi tatizo lingekwisha na utata ungeondoka hasa hasa kama sentesi salat jamia ingekaririwa mara kwa mara na wala isingebakia tena sehemu ya utata. Na hii ni dalili kuwa kunadi huku alikoamrisha Mtume kulikuwa ni kwa kutumia adhana hii ya kisheria. (Adhana ya kawaida )25

Mjadala Juu Ya Njia Za Upokezi (Sanadi)

Sababu tano zote tulizozitaja zinahusu madhumuni ya hadithi huku zikitosha kabisa kuvunja utegemezi juu ya hadithi hizo. Na sasa ni uchambuzi wa njia za upokezi moja baada ya nyingine. Njia ambazo baadhi ya mtiririko wake haujafika kwa Mtume (s.a.w.w.) na nyingine zina watu wasiojulikana au wasio waaminifu au madhaifu wasiyokubalika, Ufuatao ni uchambuzi kwa kufuata utaratibu uliopita:

Riwaya Ya Kwanza

Ambayo kaipokea Abu Daudi nayo ni riwaya dhaifu: Kwa sababu mwisho imekomea kwa mtu au watu wasiojulikana pale anaposema: toka kwa ami zake wa kianswari. Abu Umayri bin Anas naye kapokea toka kwa ami zake. Ibnu Hajari katoa wasifu wake kwa kusema: Amepokea riwaya kuhusu kuuona mwezi mwandamo na adhana toka kwa ami zake wa kianswari miongoni mwa swahaba wa Mtume. Na Ibnu Saadi kasema: Alikuwa mkweli mchache wa hadithi. Ibnu Abdul-Bari amesema: Hajulikani, huyu si hoja26.

Jamalud-dini amesema: Haya aliyosimulia katika hizi maudhui mbili: Kuona mwezi mwandamo adhana ndiyo yote aliyonayo kwao27.

Riwaya Ya Pili

Katika sanadi ya riwaya hii kuna watu wasiosihi kuwa hoja, mfano wa:

1. Muhammad Ibrahim Al-Harithi bin Khalidi At-Taymiy Abu Abdallah aliyefariki mwishoni mwa miaka ya 120. Amesema Abu Jafar Al-Aqiliy toka kwa Abdallah bin Ahmadi bin Hambali: Nilimsikia baba yangu akimtaja Muhammad bin Ibrahim At-Taymiy Al-Madaniy nakusema: Katika simulizi zake kuna shaka kwani hupokea hadithi zisizokubalika au isiyokubalika28

2. Muhammad bin Ishaqa bin Yasari bin Khiyari. Hakika riwaya zake huwa si hoja kwa masunni. Japokuwa yeye ndiyo msingi wa Sira ya Ibnu Hisham.-Iliyochapishwa . Amesema Ahmadi bin Abi Khaythamat. Na Yahya bin Muini aliulizwa kuhusu yeye (Ibnu Is.haqa) akajibu: Yule si chochote ni dhaifu. Akasema: Na nikamsikia Yahya bin Muini mara nyingine akisema: Kwangu mimi Muhammad bin Ishaqa ni dhaifu mwenye dosari. Amesema Abul-Hasani Al-Maymuni: Nilimsikia Yahya bin Muini akisema: Muhammad bin Is.haqa ni dhaifu. Al-Nasai naye kasema: Sio tegemeo29

3. Abdallah bin Zaidi: Mpokezi wa hadithi moja tu. Inakutosha ufahamu kuhusiana na yeye kuwa ni mchache sana wa hadithi. Amesema Tirmidhiy: Hatufahamu chochote kilicho sahihi alichokipokea toka kwa Mtume isipokuwa hadithi moja tu kuhusu adhana. Al-Hakim amesema: Ni sahihi na yeye aliuwawa katika vita vya Uhud na riwaya zote zilizopokewa toka kwake ni pungufu..

Ibnu Adii amesema: Hakuna tunachikifahamu kuhusu yeye kinachosihi kutoka kwa Mtume isipokuwa hadithi hii ya adhana.30

Tirmidhiy kapokea toka kwa Bukhari kuwa hatuna chochote tunachokijua toka kwake isipokuwa hadithi ya adhana31. Al-Hakim amesema: Abdallah bin Zaidi ni yule aliyeoteshwa adhana ambayo wanazuoni wa Kiisilamu wameikubali na wala haijatoka ndani ya sahihi mbili kwa sababu ya kutofautiana wapokezi katika njia za upokezi wake.32

Riwaya Ya Tatu

Mtiririko wa sanadi yake umemjumuisha Muhammad bin Is.haqa bin Yasari na Muhammad bin Ibrahim At-Taymiy. Tayari umeshaujua wasifu wao kama ulivyojua kuwa Abdallah bin Zaidi alikuwa mchache zaidi wa

Riwaya Ya Nne

Katika mtiririko wa sanadi yumo Abdur-Rahmani bin Is.haqa bin Abdallah Al-Madaniy. Amesema Yahya bin Said Al-Qataniy: Niliuliza watu wa Madina kuhusu yeye. Sikumuona yeyote akimsifia. Na hivyo ndivyo alivyosema Ali Al-Madayniy. Pia Ali amesema: Sufiyani aliulizwa kuhusu Abdur-Rahmani nikamsikia akijibu: Alikuwa ni qadiriya, hivyo watu wa Madina wakamkanusha akaja hapa wakati wa kifo cha Al-Walidi wala hatukukaa naye.

Abu Twalibu Amesema: Nilimuuliza Ahmadi bin Hambali kuhusu yeye. Akajibu: Alipokea hadithi zisizokubalika kwa Abi Al-Zanadi. Amesema Ahmadi bin Abdallah Al-Ajaly: Hadithi zake huandikwa lakini si tegemeo.

Abu Hatimu amesema: Hadithi zake huandikwa lakini si hoja. Bukhari amesema: Si mtu anayetegemewa kwa yale aliyohifadhi..Hana mwanafunzi anayejulikana Madina isipokuwa Musa Az-Zamiiyu, Amepokea vitu kutoka kwake, vitu ambavyo vingi kati ya hivyo ni utata mtupu..

Ad-Daruqutniy amesema: Ni dhaifu wa kutupiliwa mbali. Amesema Ahmadi Adii: Katika baadhi ya hadithi zake kuna mambo yasiyokubalika wala hayafuatwi33.

2- Muhammad bin Khalidi bin Abdallah Al-Wasitwiy (150- 240 A.H. ) Jamalul-Dini Al-Maziy ametaja wasifu kwa kusema: Amesema Ibnu Muiniy: Huyu si chochote, na amekanusha riwaya zake alizipokea toka kwa baba yake. Abu Hatimu amesema: Nilimuuliza Yahya bin Muiniy kuhusu yeye akajibu: Huyo ni mtu mbaya, muongo sana. Kisha akatoa mambo yasiyokubalika. Abu Uthman Saidi bin Amru Al-Baradaiy amesema: Nilimuuliza (Yaani Aba Zariat) kuhusu Muhammad bin Khalid akajibu: Ni mtu mbaya. Ibnu Habani kataja wasifu wake ndani ya kitabu chake kiitwacho Thuqati akasema: Hukosea na huenda kinyume34. Na As- Shaukaniy baada ya kunukuu riwaya akasema: Ni dhaifu sana katika upokezi wake35

Riwaya Ya Tano

Kaitika mtiririko wa njia hii yumo:

1. Muhammad bin Is.haqa bin Yasari
2. Muhammad bin Al-Harithi At-Taymiy
3. Abdallah bin Zaid. Tayari umeshajua dosari za wawili wa mwanzo na jinsi zisivyo timilifu kila riwaya anazipokea wa tatu. Kwa ajili hiyo inadhihirika wazi hali ya sanadi ya riwaya ya sita.

Haya ndiyo yaliyopokewa ndani ya Sunan. Ama yaliyomo ndani ya vitabu vingine tutayataja baadhi kama yalivyopokewa na Imam Ahmadi na Al- Daramiy na Ad-Dariqatwaniy katika vitabu vyao vya hadithi.

Pia Imam Maliki katika kitabu chake Al-Muwatwau. Na Ibnu Saadi katika Twabaqati yake. Na Bayhaqiy katika Sunan. Na ufuatao ni uchambuzi.

Riwaya Za Adhana Katika Vitabu Vingine Mbali Na Sahih Sita

Kutokana na maelezo ya Al-Hakim umefahamu kuwa mashekhe wawili (Bukhari na Muslim) hawakuitoa hadithi ya Abdallah bin Zaid kwa sababu ya kutofautiana wapokezi katika njia zao hao wawili. Isipokuwa mtu aliyeitoa hadithi hiyo kati ya waandishi wa vitabu sita ni Abu Daud, Tirmidhiy, na Ibnu Majah. Na tayari umeshajua jinsi madhumuni ya riwaya hizo yanavyopingana, huku sanad (njia zake) zikiwa dhaifu. Hivyo twende pamoja ili tusome yale yaliyoandikwa na waandishi wa hadithi na wengine kati ya watu ambao vitabu vyao huhesabika ni makini na sahihi baada ya vitabu sita.

a: Aliyopokea Imam Ahmadi ndani ya Musnadi yake:

Imam Ahmad amepokea ndoto ya adhana ndani ya Musnad yake toka kwa Ibnu Zaid kwa njia tatu:36

1-Katika njia ya kwanza yumo Zaidi bin Al-Hababi bin Al-Rayani At- Tamimiy (Aliyefariki mwaka 203 A.H. ). Yeye kasifika sana kwa kukosea na amepokea toka kwa Sufian At-Thauriy hadithi zenye kushangaza jinsi anavyozipokea.

Ibnu Muini amesema: Riwaya zake toka kwa Al-Thauriy zimegeuzwa37.

Pia imemjumuisha Abdallah bin Muhammad bin Abdallah bin Zaid bin Abdurabah ambaye ndani ya sahihi sita na vitabu vya hadithi hana riwaya isipokuwa moja tu, nayo ndiyo hii ambayo ndani yake mna ubora kwa familia yake, na kwa ajili hiyo hatuitegemei sana riwaya hii.

Njia ya pili yumo Muhammad bin Is’haqa bin Yasari ambaye tayari umeshamfahamu. Njia ya tatu yumo Muhammad bin Ibrahimu Al-Harithi At-Taymiy, ukiongeza na Muhammad Ishaqa na mwisho inakomea kwa Abdallah bin Zaid na yeye ndiye yule mchache sana wa hadithi.

Katika riwaya ya pili ni kuwa baada ya kutaja kisa cha ndoto na Bilal kujifunza adhana amesema: Hakika Bilal alikuja kwa Mtume akamkuta kalala hapo. Bilal akanadi kwa sauti ya juu: .Sala ni bora kuliko usingizi,. basi ndipo tamko hili likaingizwa katika adhana ya asubuhi.. Yaliyopo mwishoni mwa hadithi hii yanatosha kuthibitisha kuwa ni hadithi dhaifu.

b: Aliyopokea Ad-Daramiy katika Musnadi yake

Ad-Daramiy kapokea kwa njia nyingi ndani ya kitabu chake kisa cha ndoto na njia zote ni dhaifu. Na hapa tunakuonyesha baadhi ya njia hizo: Alitupa habari Muhammad Hamid kuwa: Alitusimulia Salamat kuwa: Alinisimulia Muhammad Is’haqa kuwa: Mtume alipofika Madina alikuwa.

Njia hiyo hiyo baada ya Muhammad Ishaqa imekuja: Amenisimulia hadithi hii Muhammad bin Ibrahim Al-Harithi At-Taymiy toka kwa Muhammad bin Abdallah bin Zaidi bin Abdurabah toka kwa baba yake, akataja hadithi hii.

Ametupa habari Muhammad bin Yahya kuwa ametusimulia Yaaqubu Ibrahim bin Saadi kuwa ametusimulia baba yangu toka kwa Is’haqa . Maelezo yaliyobaki ni kama yale ya njia ya pili38 .

Njia ya kwanza si kamilifu. Njia ya pili yumo Muhammad bin Ibrahim Al-Harithi At-Taymiy ambaye tayari umeshaujua wasifu wake. Njia ya tatu yumo Ibnu Is’haqa naye tayari umeshaujua wasifu wake.

C: Aliyopokea Imam Malik katika kitabu chake al-Muwatwau

Imam Maliki kapokea kisa cha ndoto ya adhana ndani ya Muwatwau toka kwa Yahya toka kwa Maliki toka kwa Yahya bin Saidi kuwa alisema: Mtume alitaka kutengeneza kengele ya mbao ili iwe inagongwa39.

Njia yake ni pungufu na makusudio ya Yahya hapa ni Yahya bin Saidi bin Qaysi aliyezaliwa kabla ya mwaka 70 akafariki eneo la Hashimiyat mwaka 143.40

d: Aliyopokea Ibnu Saadi katika Twabaqati yake

Ibnu Saadi kapokea ndani ya kitabu chake kwa njia pungufu41 zisizokuwa hoja.

Kwanza: Inakomea kwa Nafi.u Jubayrii ambaye alifariki ndani ya kumi la tisini na inasemekana mwaka 99 A.H.

Pili: Inakomea kwa Urwatu bin Al-Zubairiy ambaye alizaliwa mwaka 29 na kufariki mwaka 93 A.H.

Tatu: Inakomea kwa Zaidi bin Aslamu ambaye alifariki mwaka 136 A.H.

Nne: Inakomea kwa Saidi bin Al-Musayyab ambaye alifariki mwaka 94 A.H. na pia inakomea kwa Abdurahmani bin Abi Layli ambaye alifariki mwaka 82 A.H. au 83. A.H.

Katika kutoa wasifu wa Abdallah bin Zaidi amesema Ad-Dhahabi kuwa: Wamesimulia toka kwake Saidi bin Al-Musayibu na Abdu-Rahman bin Abi Layli ili hali hawakukutana nae42.

Pia amepokea kwa njia ifuatayo: Ametujulisha Ahmadi bin Muhammadi bin Al-Wahidi Al-Azraqiy kuwa: Ametusimulia Abdurahmani bin Umar toka kwa Abdallah bin Umar kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu alitaka Uchambuzi wake utakuijia sehemu ya pili. kuweka kitu kitakachomsaidia kuwakusanya watu mpaka mtu katika Answari alipooteshwa, Mtu huyo anaitwa Abdallah bin Zaid. Ndani ya usiku huo huo Umar naye akaoteshwa. Akaendelea mpaka akasema: Bilal akaongeza katika Sala ya asubuhi (Sala ni bora kuliko usingizi); Mtume akaipitisha.

Njia hii imemjumuisha :

1. Muslimu bin Khalidi bin Qarqurat, pia huitwa Ibnu Jarhat ambaye kadhoofishwa na Yahya bin Muini.

Amesema Ali Al-Madayniy kuwa: Huyo si chochote. Bukhari amesema: .Hadithi yake haikubaliki.. An-Nasai amesema: .Ni dhaifu.. Abi Hatimu amesema:43. .Huyo ni dhaifu hadithi yake haikubaliki, hadithi yake huandikwa lakini si hoja, hadithi zake hujulikana na hukanushwa..

2. Muhammad bin Muslim bin Ubaydullah bin Abdallah bin Shahabu Az- Zahariy (51 . 123 A.H.) Anas bin Iyadhi amenukuu toka kwa Abdallah bin Umar kuwa: nilikuwa nikimuona Az-Zahariy akitoa kitabu lakini hakuna anayekisoma wala anayesoma kwake, mwisho huambiwa tupokee haya toka kwako? Naye hujibu ndiyo.

Amesema Ibrahim Abu Sufiyani Al-Qaysaraniy toka kwa Al-Faryabiy kuwa: Nilimsikia Sufyani At-Thauriy akisema: .Nilimuendea Az-Zahriy yakanizidia mambo. Nikamwambia: Ni vizuri kama ungewaendea mashekhe zetu wakutengenezee mfano wa hili. Akajibu: Kama wewe? Akaingia ndani na kuniletea kitabu na kusema: Chukua hiki na upokee toka kwangu; lakini sikupokea hata herufi moja toka kwake.44

e: Aliyopokea al-Bayhaqiy katika kitabu chake

Bayhaqiy kapokea kisa cha adhana kwa njia ambazo zote hazikosi dosari moja au nyingi, na yafuatayo ni ishara tu ya wale dhaifu waliyopatikana ndani ya njia zake:

Kwanza: Imemjumuisha Abu Umayri bin Anas toka kwa ami zake wa kianswari. Tayari umeshamjua Abu Umayr bin Anas, yeye kazungumziwa na Ibnu Abdul-Bari kuwa: Hakika yeye hajulikani na wala si hoja45, hupokea kwa jina la ami zake toka kwa watu wasiojulikana46. Wala hakuna dalili yoyote inayothibitisha kuwa hawa walikuwa ni swahaba. Hata tukikadiria kuwa maswahaba wote ni waadilifu na tukasema kuwa ami zake walikuwa ni maswahaba lakini bado hadithi zikomeazo kwa swahaba si hoja kwani hatuna yakini kama kweli kapokea toka kwa nabii.

Pili: Imejumuisha watu ambao huwa si hoja: Muhammad bin Ishaqa bin Yasari Muhammad bin Ibrahim Al-Harithi At-Taymiy 3-Abdallah bin Zaid. Na hawa wote tayari umeshajua wasifu wao.

Tatu: Imemjumuisha Ibnu Shihabi Az-Zahariy ambaye anapokea toka kwa Saidi bin Al-Musayyab aliyefariki mwaka 94 A.H. toka kwa Abdallah bin Zaidi47 . Tayari umeshajua kuwa wote wawili hawakuwepo zama za uhai wa Abdallah bin Zaidi

f: Aliyopokea Ad-Darqutniy katika kitabu chake

Ad-Darqutniy kapokea kisa cha ndoto ya adhana kwa njia nyingi na ufuatao ni uchambuzi wake: Katusimulia Muhammad bin Yahya bin Murdasi kuwa: Katusimulia Abu Daudi kuwa: Katusimulia Uthuman bin Abi Shaybat kuwa: Katusimulia Hamadi bin Khalid kuwa: Katusimulia Muhammad bin Amru toka kwa Muhammad bin Abdallah toka kwa ami yake Abdallah bin Zaidi.

Katusimulia Muhammad bin Yahya Katusimulia Abi Daudi kuwa: Katusimulia Ubaydullah bin Omar kuwa: Katusimulia Abdul-Rahmani bin Mahdi kuwa: Katusimulia Muhammad bin Amru amesema: Nilimsikia Abdallah bin Muhammad akisema: Babu yangu Abdallah bin Zaidi alikuwa akisimulia habari hii48.

Njia zote mbili zimemjumuisha Muhammad bin Amru huku yeye hajulikani ni yupi kati ya answari, ambaye ndani ya sahihi na vitabu vya hadithi hana riwaya isipokuwa hii tu. Ad-Dhahabiy amesema: Hajulikani. Yupo pia Muhammad bin Amru ambaye ni Abu Sahlu Al-Answari ambaye Yahya bin Al-Qitaniyna Ibnu Muini na Ibnu Adiy wamemdhoofisha49.

Ametusimulia Muhammad bin Sa’id kuwa: Alitusimulia Al-Hasan bin Yunus kuwa: Alitusimulia Al-As.wadi bin Amiri kuwa: Alitusimulia Abubakar bin Iyashi toka kwa Al-Aamashi toka kwa Amru bin Marati toka kwa Al-Rahman bin Abi Layli toka kwa Maadhi bin Jabali kuwa amesema: Alisimama mtu toka kwa answari Abdallah bin Zaid akaenda kwa Mtume na kusema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika mimi nimeona usingizini50.

Njia hii ni pungufu kwa sababu Maadhi alifariki mwaka wa ishirini au kumi na nane. Na Abdul-Rahmani bin Abi Layli kazaliwa mwaka wa kumi na saba. Zaidi ya hapo ni kuwa Ad-Darqutniy kamdhoofisha Abdurahmani kwa kusema: Ni dhaifu wa hadithi mwenye kumbukumbu mbaya. Huku Ibnu Abi Layli haujathibitika usikivu wake toka kwa Abdallah bin Zaid51

Mpaka hapa mazungumzo kuhusu sehemu ya kwanza yamekamilika na imedhihiri kuwa: Sheria ya adhana ililetwa kwa njia ya ufunuo wa Mwenyezi Mungu na wala si kwa ndoto ya Abdallah bin Zaid wala si kwa ndoto ya Umar bin Al-Khattabi wala si kwa ndoto ya mtu yoyote. Na ni kwamba hizi hadithi zinapingana, na hazina njia timilifu kimapokezi wala hazithibitishi chochote. Zaidi ya hapo ni kama tulivyosema mwanzo wa uchambuzi kuwa akili salama haikubaliani na hilo.

Sasa umefika wakati wa kuchambua jinsi kilivyoingizwa kipengele cha ziada ndani ya adhana ya alfajiri. Na hii ni sehemu ya pili tutakayokuletea hivyo tunasema:
________________________
1. Riwaya mbili hazipingani kwani ni mara ngapi Imam ameshuka na ufunuo wa aya moja mara mbili, na atakayefuatilia ataona wazi kuwa lengo la adhana katika riwaya ya mwanzo si lile lililopo kwenye riwaya ya pili.

2. Ali tangu udogo alikuwa akisikia maneno ya malaika: Angalia Sahih Bukhari: 4 / 200, na sherehe yake: Irshadil-Sari: 6 /99 na nyingine. Mlango: Watu wanasemeshwa na malaika bila ya kuwa manabii. Amepokea Abu Huraira toka
kwa Mtume kuwa alisema: .Lilikuwa likifanyika hata kwa waliyokuwa kabla yenu kwa Bani Israili ...

3. Al-Kulayniy: Al-Kafy: 3/302 mlango: Chanzo cha adhana hadithi ya 1 na 2

4. Al-Kafy: 3/482 Juz. 1. Mlango wa mambo nadra. Tutakuletea huko kuwa karibuni
watu kumi na nne walidai eti wameiota adhana.

5. Itakufikia riwaya toka ndani ya vitabu sita (As-Sunan)

6. Wasailul-Shiat: Juzuu ya 4/612 Mlango wa kwanza kati ya milango ya adhana
na iqama. Hadithi 3

7. Kilichopokewa toka kwao (a.s.) ni kuwa iqama ni mara mbilimbili isipokua kifungu cha mwisho ndio mara moja

8. Al-Hakimu: Al-Mustadarak: 3/181, Kitabu: Kuwajua Maswahaba

9. Al-Mutaqiy Al-Hindiy: Kanzul-Amali: 12/350 namba 35354

10. Burhanul-dini Al-Halabiy: As-Sirat Al-Halabiyat: 2/300-301.

11. Kanzul-Ummal:8/329 namba 231338, kipengele cha adhana

12. Abdurazaqi bin Hamam Al-Swinaiy (126-211 ) mtunzi: 1/456 namba 1775

13. As-Sirat Al-Halabiyat : 2/296 mlango: Kuanza sheria ya adhana

14. Hivi inasihi kiakili mtu afiche ndoto hiyo siku ishirini ndoto ambayo ina raha kwa Mtume na maswahaba zake, kisha baada ya kuisikia kwa Ibnu Zaidi atoe udhuru kuwa aliona aibu, ilihali hata mimi siwezi kuwa na akili kama hizi za khalifa. Zaidi ya hapo inagongana na hadithi ya pili.

15. Abu Daud: As-Sunan: 1/134/135 namba 498-499 Utafiti wa Muhammad Muhyi-dini. Hadithi hii inazungumzia kitendo cha Omar kujua adhana baada ya adhana ya Bilal, kinyume na hadithi iliyotangulia.

16. Ibnu Majah : As-Sunan: 1/232-233 mlango: kuanza kwa adhana namba 706- 707.

17. Al-Tirmidhi : As-Sunan: 1/358-361, mlango: yanayohusu mwanzo wa adhana namba 189.

18. (1, 2, 3) At-Tirmidhiy; As-Sunan:1/362 namba 190 na An-Nasai: As-Sunani

19. 2/3. Al-Bayhaqiy: As-Sunani: 1/389 mlango: Kuanza kwa adhana. Hadithi ya kwanza

20. As-Sirat Al-Halabiyat: 2/297

21. Al-Bayhaqiy: As-Sunan: 1/390, hadithi 1

22. As-Sirat Al-Halabiyat: 2/300

23. Al-Bukhari: Al-Swahihi:1/120 mlango: Mwanzo wa adhana

24. Angalia hadithi namba 2

25. Sharafu dini: An-Nasu wal-ijtihadi: 137

26. Ibnu Hajar: Tahdhibul-Tahdhibi:12/188 namba. 867

27. Jamaludini Al-Maziy: Tahadhibul-Kamali:34/142 namba 7545

28. Tahdhibul-Kamali:24/304

29. Chanzo cha mwanzo 24/423-424, Angalia Tarikhu Baghdadi: 1/221-224.

30. As-Sunan: Al-Tirmidhiy:1/361, Ibnu Hajar: Tahdhibul-Tahadhibi: 5/224

31. Tahdhibul-Kamali: 14/541

32. Al-Hakimu: Al-Mustadarak, 3/336 riwaya na riwaya zote zilizotoka kwake ni pungufu kwasababu aliuwawa vita vya Uhud

33. Tahdhibul-Kamali:16/ 519 namba 3755

34. Tahdhibul-Kamali 25/139 namba 5178

35. Al Shaukaniy: Naylul-Atuwar:2/37-38

36. Al-Imam Ahmadi: Al-Musnadi: 4/42-43

37. Al-Dhahabiy: Mizanul-Itidali: 2/100 namba 2997

38. Al-Daramiy: As-Sunan:1/268-269 mlango: mwanzo wa adhana

39. Maliki: Al-Muwatwau:15 mlango: yanayohusu wito wa sala namba 1

40. Siratul-Aalamu Al-Nubalau: 5/468 namba 213

41. Kitab Tabakatil Kubra

42. Siratul-Aalamu Al-Nubalau:2/376 namba 79.

43. Jamalul-Dini Al-Maziy: Tahdhibul-Kamali:27/508 namba 5925.

44. Chimbuko lile lile

45. Al-Bayhaqiy: As-Sunan:1/390.

46. Ibnu Hajar Tahdhibul-Tahadhibi: 12/188 namba 868

47. Al-Bayhaqiy: As-Sunani: 1/390

48. Ad-Daruqutniy: As-Sunan: 1/245 namba 56 na 57

49. Al-Dhahabiy: Mizanul-Itidali: 3/674 namba 8017 na 8018. Jamalul-Dini Al-Maziy: Tahdhibil-Kamali: 26/220 namba 5516. Ibnu Hajar: Tahdhibul-Tahadhibi: 9/378 namba 620

50. Ad-Daruqutniy: As-Sunan:1/242 namba 31 Abdallah bin Zaid

51. Ad-Daruqutniy: As-Sunan:1/241

Uchambuzi Kuhusu Historia Ya Kuingia Kipengele Cha Kuhimiza (Tathuwibi) Katika Adhana ya Alfajiri

At-Tathuwibi ni neno la Kiarabu litokanalo na kitenzi Thaba - Yathubu: Linaweza kuwa na maana ya kurejea, hivyo katika adhana litamaanisha kurejea kwenye amri kwa kuharakisha kuelekea kwenye Sala. Hivyo muadhini akisema: Njooni kwenye Sala atakuwa kawaita waelekee kwenye Sala, hivyo akisema tena: Sala ni bora kuliko usingizi atakuwa karejea katika maneno ambayo maana yake ni kuharakisha kwenda kwenye Sala. Mwandishi wa kamusi iitwayo: Al-Qamusi amefasiri kwa maana mbalimbali kati ya hizo maana ni: Kuomba waelekee kwenye Sala. Na ile hali ya kurudia mara mbili mbili ni ombi. Na pia kusema katika adhana ya alfajiri: Sala ni bora kuliko usingizi mara mbili - ni ombi.

Na amesema ndani ya kitabu Al-Magharibi kuwa: At-Tathuwibi ya zamani ilikuwa ni ile kauli aisemayo muadhini katika adhana ya asubuhi: Sala ni bora kuliko usingizi - mara mbili - Na hivi sasa At- Tathuwibi ni kusema: Sala Sala, imesimama 1

Dhahiri ni kuwa tathuwibi inatumika sana kwa maimam wa hadithi wakimaanisha ile kauli inayotajwa ndani ya adhana. Pia huenda ikatumika kumaanisha wito wowote unaokuja baada ya wito wa mwanzo hivyo hujumuisha wito wowote autoawo muadhini baada ya kumaliza adhana kwa kutamka tamko lolote alipendalo lenye maana ya wito wenye kuelekeza kwenye Sala.

As-Sanadiy amesema katika maelezo yake ya ziada ndani ya kitabu Sunanin-Nasai kuwa: Tathuwibi maana yake ni kurudia tangazo baada ya tangazo, Hivyo kauli ya muadhini: Sala ni bora kuliko usingizi ni sawa na hali hiyo hiyo, hivyo ikaitwa tathuwibi.2

Makusudio ya sehemu hii ni kutaka kudhihirisha hukumu ya kauli ya muadhini ndani ya adhana ya Sala ya alfajiri: Sala ni bora kuliko usingizi. Je ni kauli ya kisheria au ni bidaa iliyozushwa baada ya Mtume kutokana na pendekezo la baadhi ya watu walioona kuwa ni vizuri iwekwe kwenye adhana. Hiyo ni sawa iwe ndani ya adhana au hata baada ya adhana kwa wito wowote unaoelekeza kwenye Sala. Sawa iwe kwa tamko hili au lingine.

Hivyo tunasema kuwa tathuwibi kwa maana hii (Sala ni bora kuliko usingizi) imepatikana ndani ya hadithi za kisa cha ndoto ya adhana, na imepatikana tena katika hadithi nyingine. Ama katika fungu la kwanza imepatikana katika riwaya zifuatazo:

1. Riwaya aliyoipokea Ibnu Majah (Riwaya ya nne) na tayari umeshasikia maelezo ya As-Shaukaniy jinsi ilivyodhoofika3

2. Riwaya aliyoipokea Imam Ahmad nayo umeshajua udhaifu wa njia yake kwani yumo Muhammad bin Is’haqa na Abdallah bin Zaid bin Abdurabah4 . Riwaya aliyoipokea Saad katika kitabu chake At-Twabaqat. Katika njia yake yumo Muslim bin Khalid bin Qarqarat. Udhaifu wake tayari umeshaujua5.

Ama katika fungu la pili yaani tathuwibi katika hadithi zisizo za kisa cha ndoto ya adhana ni kwamba hadithi hizo zimenukuliwa na waandishi wa vitabu sita, na yafuatayo ni maelezo yao:

Aliyonukuu Ibnu Majah: ni kwa njia ifuatayo:

Alitusimulia Abu Bakr bin Shaybati kuwa: Alitusimulia Muhammad bin Abdallah Al-Asadiy toka kwa Abi Izraili toka kwa Al-Hakamu toka kwa Abdurahmani bin Layli toka kwa Bilal amesema kuwa: Mtume aliniamrisha nihimize (Sala ni bora kuliko usingizi ) katika Sala ya Asubuhi na akanikataza katika Sala ya Isha6.

Katika riwaya hii kuna dalili inayoonyesha kuwa katika kuhimiza unaweza kutumia wito wowote unaoelekeza kwenye Sala hata kama si tamko la: Sala ni bora kuliko usingizi. Dalili juu ya hilo ni kile kitendo cha kukataza kuhimiza katika Sala ya isha kwa sababu huwezi kuhimiza katika Sala hii isipokuwa kwa tamko lingine, mfano wa: Salat jamia, au imesimama Sala, au tamko lingine.

5-Ametusimulia Umar bin Rafi kuwa: Ametusimulia Abdallah bin Al- Mubarak toka kwa Maamari toka kwa Az-Zahariy toka kwa Saidi bin Al- Musayab toka kwa Bilal kuwa: Alikuja kumuadhinia Mtume kwa ajili ya sala ya asubuhi akaambiwa amelala, hapo akasema: Sala ni bora kuliko usingizi, Sala ni bora kuliko usingizi, basi ikaidhinishwa iwekwe kwenye adhana ya Sala ya alfajiri. Basi kwa namna hiyo jambo hilo likathibiti7. Njia zote mbili za upokezi ni pungufu.

Kwanza: Ibnu Abi Layli amezaliwa mwaka wa 17 na Bilal kafariki mwaka wa 20 au 21 huko Sham. Na Bilal alikuwa huko Sham tangu Shamu ilipofunguliwa hivyo Bilal ni mkazi wa Sham na Ibnu Abi Layli ni mkazi wa Kufa, hivyo itakuwaje asikie toka kwa Bilal ilhali kiumri yeye ni mdogo sana kwa Bilal na kimakazi yuko mbali na Bilal8.

Na Tirmidhi kapokea kama hivyo lakini kwa tofauti katika njia (sanad) asema: Hadithi ya Bilal hatuijui isipokuwa kupitia hadithi ya Abi Israii Al- Mlai, na huyu Abi Israili hajaisikia hadithi hii toka kwa Al-Hakamu (Ibnu Utayba).

Akasema: Hakika yeye aliipokea toka kwa Al-Hasani bin Amarat toka kwa Al-Hakam. Na Abu Israili jina lake ni Ismail bin Abi Is.haqa, na yeye kwa watu wa hadithi ni dhaifu9

Pili: ni kuwa Ibnu Majah amenukuu maneno toka kwa Az-zawaidi kwa kusema: Wapokezi wake ni wakweli isipokuwa njia yake ni pungufu kwa sababu Said bin Al-Musayabu hakuisikia toka kwa Bilal10 .

6. Aliyopokea an-Nasaiy

Alitupa habari Suwayd bin Nasri kuwa: Alitupa habari Abdallah toka kwa Sufiani toka kwa Jafari toka kwa Abi Salmani toka kwa Abi Mahdhurat amesema kuwa: Nilikuwa nikimuadhinia Mtume wa Mwenyezi Mungu na nilikuwa nikisema katika adhana ya Alfajiri ya mwanzo: (Njooni kwenye ushindi, Sala ni bora kuliko usingizi, Sala ni bora kuliko usingizi, Allah mkubwa Allah mkubwa, hapana mola wa haki isipokuwa Allah)11 .

Katika Sunan ya Al-Bayhaqiy12 na Subulu Salama13 sehemu ya jina Abi Salmani lipo jina Abi Sulaymani. Al-Bayhaqiy amesema: Na Abu Sulaymani jina lake ni Hamamul-muadhin, wala katika vitabu vyote tulivyonavyo vya wasifu wa wapokezi hakuna wasifu wa Hamamul- Muadhini hivyo Adh-Dhahabiy hakumtaja ndani ya kitabu chake (Mwenendo wa wasomi wema). Wala Al-Mazriy hakumtaja ndani ya Tahdhibil-Kimal na huyu Hamamu ni mtu asiyefahamika.

Ama Abu Mahdhurat yeye ni kati ya swahaba lakini mchache wa riwaya kwani riwaya alizopokea hazizidi kumi na alikuwa muadhini wa Mtume mwaka wa nane wakati wa vita vya Hunayni14 .

7. Aliyopokea Al-Bayhaqiy

Katika kitabu chake (Sunan) kuna njia inayokomea kwa Abi Qadamat toka kwa Muhammad bin Abdul-Malik bin Abi Mahdhurat toka kwa baba yake toka kwa babu yake kuwa amesema: Nilisema: Ewe Mtume wa Allah, nifundishe sunna ya adhana. Akasimulia hadithi husika, na katika maelezo yake Mtume akasema:

حي علي الصلاة حي علي الصلاة

(Njooni kwenye Sala njooni kwenye Sala), ikiwa ni sala ya Asubuhi sema:

الصلاة خيرمن النوم

(Sala ni bora kuliko usingizi, Sala ni bora kuliko usingizi).

8. Pia kapokea kwa njia inayokomea kwa Uthman bin Al-Saibu:

Alinipa habari baba yangu na mama wa Abdul-Maliki bin Abi Mahdhurat toka kwa Abi Mahdhurat toka kwa Mtume. Mfano wa riwaya iliyopita15. Umeshajua hali ya Muhammad bin Abdul-Malik. Na Uthman bin Al-Saibu ni mtoto na mzazi wasiyojulikana hawana riwaya isipokuwa hiyo moja tu16

9. Aliyopokea Abu Daud

Amepokea kwa njia inayokomea kwa Al-Harith bin Ubaydi toka kwa Muhammad bin Abdul-Malik toka kwa baba yake toka kwa babu yake amesema kuwa: Nilisema: Ewe Mtume wa Allah nifundishe sunna ya adhana. Akaendelea mpaka akasema: Kama ni Sala ya asubuhi utasema: (Sala ni bora kuliko usingizi Sala ni bora kuliko usingizi)17.

Njia hii imemjumuisha Muhammad bin Abdul-Malik. Amesema Ibnu Hajari kuwa: Amesema Abdul-haqi kuwa: Njia hii si hoja. Na Ibnu Qaytani akasema: Huyu hajulikani, hatumjui aliyopokea toka kwake isipokuwa Al- Harith18. Na Amesema Al-Shaukani kuhusu Muhammad bin Abdul-Malik bin Abi Mahdhurat kuwa wasifu wake haujulikani. Na Al-Harith bin Ubaydi na yeye ana maelezo yake 19.

10. Pia amepokea kwa njia inayokomea kwa Uthman bin Saibu:

Alinijulisha baba yangu na mama wa Muhammad binAbdul-Malik bin Abi Mahdhurat toka kwa baba Mahdhurat toka kwa Mtume Mfano wa habari hii20. Tayari umeshajua udhaifu wa njia hii.

11. Pia amepokea kwa njia inayokomea kwa Ibrahim bin Ismail bin Muhammad bin Abdul-Malik bin Abi Mahdhurat amesema kuwa: Nilimsikia babu yangu Abdul-Malik bin Abi Mahdhurat akisema kuwa alimsikia Abi Mahdhurat akisema kuwa: Mtume alinifundisha adhana herufi baada ya herufi - mpaka akasema: Alikuwa akisema katika Sala ya Alfajiri:

الصلاة خيرمن النوم

(Sala ni bora kuliko usingizi).21

Na Ibrahim bin Ismail ana riwaya moja tu na ukweli wake haujathibitishwa 22. Zaidi ya hapo huenda njia hii ni pungufu. Aliyopokea Ad-Darqutniy

Nayo yamegawanyika:

12. Zipo riwaya zinazoonyesha kuwa ni sunna ndani ya adhana, amezipokea toka kwa Anas na Umar bila kuzinasibisha kwa Mtume nazo ni hadithi tatu:23

13. Zinazoonyesha kuwa Mtume alimuamrisha Bilal kufanya hivyo, lakini njia hiyo ni pungufu. Amepokea Abdul-Rahman bin Abi Layli toka kwa Bilal24 huku njia yake ni dhaifu kwa kuwemo Abdur-rahmani bin Al- Hasan ambaye huitwa Abu Mas.udi Az-Zajaju.Na Abu Hatim kamuelezea kwa kusema: Yeye si hoja hata kama wengine wakimlainisha 25.

14. Zipo zinazoonyesha tangazo kabla ya adhana kwa namna yoyote ile. Na hilo liko nje ya mada. Na baadhi ya waliyomo katika mtiririko wa njia hii wameidhoofisha26.

Aliyopokea Al-Daramiy

15. Ad-Daramiy kapokea kwa njia inayokomea kwa Az-Zahariy toka kwa Hafsa bin Umar bin Suad Muadhini.Hafsa amesema: .Walinisimulia ndugu zangu kuwa Bilal alikwenda kumuadhinia Mtume kwa ajili ya Sala ya Asubuhi, wakamwambia Mtume amelala, hapo Bilal akanadi kwa sauti ya juu:

الصلاة خيرمن النوم

(Sala ni bora kuliko usingizi:, ndipo ikapitishwa na kuwekwa ndani ya adhana ya Sala ya Alfajiri27. Riwaya hii si hoja: Kwanza kwa kuwemo Az-Zahriy na Hafsa ambaye hana riwaya isipokuwa moja tu nayo ni hii28.

Zaidi ya hapo ni kuwa hajulikani ni nani asili aliyenukuu riwaya hii.

16. Aliyopokea Imam Malik

Ni kuwa muadhini alikwenda kumuadhinia Umar bin Al-Khatab kwa ajili ya Sala ya Asubuhi hivyo akamkuta amelala, muadhini akasema:

الصلاة خيرمن النوم

(Sala ni bora kuliko usingizi), ndipo Umar akaamrisha kipengele hicho kiwekwe ndani ya wito wa Sala ya Asubuhi29.

 

Matokeo Ya Riwaya

Hakika riwaya zinazoelezea kipengele cha kuhimiza (Sala ni bora kuliko usingizi) zinapingana sana huwezi kuzioanisha katika maana moja. Na vifuatavyo ni vifungu vyake:

1. Zipo zinazoonyesha kuwa Abdallah bin Zaid aliota usingizini kipengele cha (Sala ni bora kuliko usingizi) katika ndoto yake na ilikuwa ni sehemu ya adhana tangu mwanzo wa adhana.

2. Zipo zinazoonyesha kuwa Bilal aliongeza kipengele hicho ndani ya adhana, na Mtume akakipitisha na kumtaka Bilal akiweke kiwe sehemu ya adhana, na hilo ni kama ilivyo kwenye riwaya ya Ad-Daramiy.

3. Zipo zinazoonyesha kuwa Umar bin Al-Khatabi alimuamrisha muadhini akiweke ndani ya wito wa asubuhi, hilo ni kama alivyopokea Imam Malik.

4. Zipo zinazoonyesha kuwa Mtume wa Allah alimfundisha Abi Mahdhurat, hilo ni kama ilivyo katika riwaya ya Al-Bayhaqiy katika kitabu chake.

5. Dhahiri ni kuwa Bilal alikuwa akinadi asubuhi akisema: حي علي خيرالعمل (Njooni kwenye amali bora), hivyo Mtume akamwamrisha atoe kipengele hicho na sehemu yake aweke kipengele:

الصلاة خيرمن النوم

(Sala ni bora kuliko usingizi), na aache حي علي خيرالعمل (njooni kwenye amali bora.
Haya ni kama alivyopokea Al-Muttaqiy Al-Hindiy ndani ya kitabu chake Kanzu 8 / 345 namba 23188 ).

Kutokana na mgongano huu wa wazi hatuwezi kutegemea riwaya hizo. Na kwa kuwa jambo lenyewe lipo kati ya hali mbili: ima liwe ni sunna au bidaa basi tunapasa kuliacha kwa kuwa hatutoadhibiwa iwapo tutaliacha kinyume na litakapokuwa ni bidaa.

Maneno Yawanavyuoni Kuhusiana Na: Kuhimiza Sala Ni Bora Kuliko Usingizi

Upande wa swahaba na tabiina wapo wanaoona kuwa jambo hilo ni bidaa wala Mtume hakuliamrisha, na kuwa lilizuka baada ya Mtume. Yafuatayo ni maelezo yao:

1. Ibnu Jariri anasema: .Amr bin Hafsa alinipa habari kuwa Saad muadhini ndiye mtu wa kwanza aliyesema:
 

الصلاة خيرمن النوم

(Sala ni bora kuliko usingizi), ilikuwa wakati wa utawala wa Umar hivyo Umar akasema: Ni bidaa, kisha akamuacha na wala Bilal hakumuadhinia Umar.

2. Pia amepokea toka kwake kuwa: Alinipa habari Hasan Muslim kuwa kuna mtu alimuuliza Twausi: Ni lini ilianza: Arabic text (Sala ni bora kuliko usingizi)? Akajibu: .Haikutamkwa hii wakati wa Mtume lakini Bilal aliisikia zama za Abu Bakr baada ya kifo cha Mtume (s.a.w.w.) ilikuwa ikitamkwa na mtu asiye muadhini, hivyo akaichukua toka kwake, kisha akaadhini kwa kipengele hicho, lakini toka wakati huo Abu Bakr hakuishi sana zikawa zimeingia zama za Umar. Akasema Umar: Tungemkataza Bilal kuhusu hili alilolizusha, utadhani kalisahau ameendelea kuwaadhinia watu kwa hili mpaka leo30.

3. Amepokea Abdur-Razaqi toka kwa Uyynati toka kwa Laythu toka kwa Mujahidu kuwa amasema: .Nilikuwa na Ibnu Umar akasikia mtu akihimiza (tathuwibi). Akasema: .Hebu twende zetu tutoke kwa mtu huyu wa bidaa31.

Kwa riwaya ya Abu Daud ndani ya Sunan yake, dhahiri ni kuwa mtu huyo alihimiza katika Sala ya adhuhuri na Sala ya Alasiri na si Sala ya Asubuhi32

4. Yaliyopokewa toka kwa Abu Hanifa kama ilivyo ndani ya Jamiul- Masanidi toka kwa Hamadi toka kwa Ibrahimu amesema: Nilimuuliza kuhusu tamko la himizo (tathuwibi) akasema: Hilo ni katika mambo yaliyozushwa na watu, nalo ni jambo zuri kati ya mambo waliyoyazusha. Kisha akaongeza kuwa: wao tamko hilo lilikuwa baada ya muadhini kumaliza adhana yake husema: Arabic text (Sala ni bora kuliko usingizi) . mara mbili.

Amesema: Riwaya hii ameitoa Imam Muhammad bin Al-Hasan (As- Shaybani) ndani ya kitabu chake Al-athar. Wao wawili wamepokea toka kwa Abu Hanifa. Kisha Muhammad akasema: Nayo ni kauli ya Abu Hanifa na ndio tunayoifuata33.

Riwaya hii inaonyesha kuwa kipengele hiki kilikuwa kinawekwa baada ya kumaliza adhana hizo ni zama za mtukufu Mtume au makhalifa na wala hakikuwa ni sehemu ya adhana bali muadhini alikitamka yeye mwenyewe kwa ajili ya kuamsha watu toka usingizin, kisha baadaye kikaingizwa ndani ya adhana.

5. As-Shaukani kanukuu toka kwenye Al-Bahri Al-Zakhari kuwa: Alikizua Omar. Mwanae akasema: .Hii ni bidaa. Imepokewa toka kwa Ali (a.s.) kuwa baada ya kusikia tamko hilo (tathuwibi) alisema: .Msizidishe ndani ya adhana kitu ambacho hakimo.. Kisha baada ya kutaja hadithi ya Abu Mahdhurat na Bilal akasema: .Tunasema ikiwa ni kwa sababu ya kukanushwa na Ali (as) na mwana wa Omar na Twausi basi tumekubali. Hivyo timeamrishwa kwa ajili ya kuhisisha hali na wala si kama sheria, hiyo ni ili tuoanishe kati ya riwaya hizo34.

6. Al-Amiru Al-Yamaniy As-Swinaiy (Aliyefariki mwaka 182) amesema: .Nilisema: Kutokana na haya ni kuwa kipengele hiki

الصلاة خيرمن النوم

(Sala ni bora kuliko usingizi) si miongoni mwa matamshi ya adhana iliyowekwa na sheria kwa ajili ya kuwaita watu waelekee kwenye Sala huku ikionyesha kuwa wakati wa Sala umeingia. Bali kipengele hiki ni kati ya matamshi ambayo yalianzishwa ili kumuamsha yule aliyelala, hivyo matamshi hayo ni sawa na ile tasbihi ya mwisho ambayo hivi sasa watu wameizoea hasa badala ya adhana ya kwanza.
Kisha akasema: Basi ukishalijua hili utakuwa mwepesi kwako mjadala uliyozoeleka kati ya wanazuoni kuhusiana na matamshi hayo, Je yenyewe ni sehemu ya matamshi ya adhana au siyo. Na je ni bidaa au siyo35

7. Ibnu Qaddama amenukuu toka kwa Is.haqa kuwa baada ya kunukuu riwaya ya Abi Mahdhurat alisema: Hili ni jambo walilolizua watu.

Abu Isa amesema: .Hiki ndio kipengele cha kuhimiza (tathuwibi) kilichochukiwa na wanazuoni, na ndicho kilichomsababisha mwana wa Umar atoke msikitini alipokisikia36.

8. Kwa sababu riwaya nyingi zilizotoka kwa Maimam wa Ahlul-Bait zinathibitisha kuwa ni bidaa. Amepokea Sheikh Tusiy kwa njia sahihi toka kw

Share this article

Comments 0

Your comment

Comment description

Latest Post

Most Reviews

MOST READ