Rafed English

Kuwa Na Uhuru Na Kutokuwa Nao

Kuwa Na Uhuru Na Kutokuwa Nao by : Sayyid Mujtaba Musawi Lari

 

Moja ya maswali yanayovutia watu wengi wakiwemo wanafalsafa ni juu ya asili ya mwanadamu na maisha yake kwa ujumla, tatizo lenyewe linaanzia katika kutaka kufahamu kama binadamu ana uhuru kamili katika matendo yake au anadhibitiwa? Je, matamanio yake na mwelekeo wa maisha na uhuru alionao katika maamuzi ndio vitu pekee vinavyomfanya awe katika hali fulani? Au matendo na tabia zake vyote hivyo vimedhibitiwa? (Yaani kuwa hali amri juu ya mwelekeo wake). Je, kuna vitu fulani katika mazingira anamoishi vinamlazimisha yeye kuwa katika hali fulani?

Ili kufahamu umuhimu wa swali hili ni vyema ikumbukwe kwamba ufumbuzi/jibu lake linategemea faida/manufaa tunayoweza kuyapata ya kiuchumi, sheria, dini, saikolojia na matawi mengine mengi ya taaluma ambayo binadamu ndio mlengwa mkuu.

Suala la kuwa binadamu anao uhuru katika mambo yake au sio halihusu nyanja ya kielimu au falsafa tu, bali yapaswa lihusishe kila nyanja.

Lakini juu ya jambo kwamba huyu binadamu anao uhuru pia sio la kulipinga moja kwa moja kwa sababu kama hanao uhuru wowote vipi juu ya hukumu ya siku ya Mwisho? Kwa waliofanya mema watalipwa pepo na wale watakaofanya maovu kuwa watapewa adhabu ya Moto. Baada ya kuenea kwa Uislamu, Waislamu nao walikuwa wakijihusisha kwa kiasi kikubwa kupata majibu ya swali hilo kwamba binadamu yu ana uhuru au la?

Watu wa vipindi vyote viwili, wakati uliopo au wakati uliopita wanaweza kugawanywa katika makundi mawili kuhusiana na suala hilo la kuwa binadmu anao uhuru au la? Kundi la kwanza lenyewe linapinga kuwa binadamu anao uhuru katika vitendo vyake na kama matendo yake yataonyesha aina fulani ya uhuru basi hiyo ni kwa sababu ya ufinyu wa ufahamu wa binadamu (yaani kwamba ni kutokana na makosa tu).

Kundi la pili ni lile linalo amini kwamba binadamu anao uhuru kamili katika mambo yake, uwezo wake wa kufikiri na kuamua una athari kubwa katika matendo yake na wala hautegemei mazingira.

Kwa kweli binadmu anazungukwa/anakabiliwa na mambo fulani ambayo hana amri juu yake. Mfano kuzaliwa, kufa na mambo mengine mengi tu yanayomzunguka. Kwa sababu hiyo ndio maana watu wengine wakalazimika kuamini kwamba binadamu hana uhuru kabisa katika matendo yake.

Wakati huohuo binadamu anatambua kwamba yeye yuko huru kabisa. Mfano anao uwezo wa kupambana na vikwazo vingi katika maisha yake pia katika harakati za kuyakabili mazingira yanayomzunguka kwa kutumia elimu aliyo nayo, lakini kuna ukweli ambao kamwe hawezi kukanusha nao ni juu ya jinsi anavyoweza kuitumia mikono yake na miguu, lakini wakati huo huo akashindwa kufanya hivyo kwa viungo kama vile moyo, ini na mapafu.

Kwa kuwa na matakwa, uwezo wa kufahamu na uwezo wa kuchagua vitu ambavyo vinavyompa sifa ya ubinadamu na ndio chanzo cha majukumu na wajibu alionao, binadamu anatambua wazi kabisa kwamba kuna mambo ambayo yanauwezo wakufanyika pasipo ridhaa ya mwanadamu huyo na mambo hayo yanachukua sehemu kubwa sana ya maisha ya mwanadamu.
Wale wanaofuata dhana ya kuwa binadamu hana uhuru katika mambo yake hawaamini kwamba mwanadamu hana uhuru katika mambo yake, wanatheolojia wa Kiislamu ambao nao pia wanafuata dhana hiyo. Mfano Ash-ariah kwa kutumia baadhi ya aya ambazo hawana ufahamu nazo vizuri za Qur’an na wameamua kuwa vipofu wa kutotazama aya zingine na hawataki kujua mamlaka aliyonayo Mwenyezi Mungu; wao wanasema kwamba binadamu hana uhuru hata chembe katika mambo yake.

Pia wanakanusha kwamba kuna vituo/mambo fulani ambavyo yanaweza kupelekea matokeo fulani. Kwa kifupi wao wanasema kwamba kila kitu kimeshapangwa na Mwenyezi Mungu japokuwa mwanadamu ana uwezo fulani lakini uwezo wake huo hauna nafasi ya kusababisha/kupelekea kutenda mambo yake. Mambo yote yanayofanywa na binadamu yanakuwa yameshapangwa na Mwenyezi Mungu.

Binadamu anaweza kwa kiasi fulani kuyapamba matendo yake; mfano kuna namna mbili ambapo kwa mujibu wao ni ubaya au uzuri. Zaidi ya hapo binadamu si chochote isipokuwa chombo cha kutimiza matakwa ya Mwenyezi Mungu.

Wanaendelea kusema kwamba ikiwa watu wataamini kwamba Binadamu ana uhuru wa namna yoyote ile katika matendo yake basi tutakuwa twampunguzia Mwenyezi Mungu mamlaka na uwezo wake; ili mamlaka na uwezo wa Mwenyezi Mungu utimizwe lazima tukubali kwamba yeye pekee ndiye mpangaji wa kila jambo hususani yale yaliyoumbwa ikiwa pamoja na matendo ya Mwanadamu.

Ikiwa tutakubali kwamba binadamu ana uwezo wa kutayarisha hatima yake/kwamba yote yanayofanywa na mwanadamu yanatokana na utashi wake basi tutakuwa tumepunguza mamlaka yake Mwenyezi Mungu, kwa hiyo itikadi ya kuamini kwamba binadamu yuko huru ni ushirikina.

Watu wengine wanatumia mwanya wa kuwa wanahaki na uhuru wa kufanya mambo fulani, kutenda mambo maovu ambayo mambo hayo yanakwenda kinyume na dini. Baadhi ya watu wanachukulia kuwa kwa kuwa wao hawana mamlaka juu ya matendo yao kwamba tayari yamepangwa na Mwenyezi Mungu kama ni nafasi ya kujifanyia wanavyotaka kwa kuwa sio wao bali Mungu ameshawapangia.

Kanuni hii ya hawa watu inakwenda kinyume kabisa na uadilifu, moja wapo ya sifa ya Mwenyezi Mungu na hata ya binadamu mwenyewe, tazama Qur’an (3:18).
شَهِدَ اللَّهُ أَنَّهُ لَا إِلَٰهَ إِلَّا هُوَ وَالْمَلَائِكَةُ وَأُولُو الْعِلْمِ قَائِمًا بِالْقِسْطِ ۚ لَا إِلَٰهَ إِلَّا هُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُۚ
“Mwenyezi Mungu, na Malaika, na wenye ilimu, wameshuhudia kuwa hakika hapana Mungu ila yeye, ndiye Mwenye kusimamisha uadilifu, hapana Mungu ila Yeye Mwenye nguvu na Mwenye hekima.”
Mwenyezi Mungu anaelezea suala la kuletwa haki duniani kama ni sehemu mojawapo ya malengo ya kuletwa kwa Mitume na anasema ni lengo lake kuona wanadamu wanadumisha haki duniani. “kwa hakika tuliwatelemsha Mitume kwa hoja na miujiza ya wazi kabisa na kisha tukaleta ili kwamba watu watende haki” , Qur’an (57:25).
لَقَدْ أَرْسَلْنَا رُسُلَنَا بِالْبَيِّنَاتِ وَأَنْزَلْنَا مَعَهُمُ الْكِتَابَ وَالْمِيزَانَ لِيَقُومَ النَّاسُ بِالْقِسْطِ ۖ وَأَنْزَلْنَا الْحَدِيدَ فِيهِ بَأْسٌ شَدِيدٌ وَمَنَافِعُ لِلنَّاسِ وَلِيَعْلَمَ اللَّهُ مَنْ يَنْصُرُهُ وَرُسُلَهُ بِالْغَيْبِ ۚ إِنَّ اللَّهَ قَوِيٌّ عَزِيزٌۚ
“Kwa hakika tuliwatuma Mitume wetu kwa dalili wazi wazi, na tukateremsha kitabu pamoja nao na Mizani, ili watu wasimamie uadilifu, na tumeteremsha chuma chenye nguvu nyngi na manufaa kwa watu, na ili Mwenyezi Mungu amjue anaye mnusuru yeye na Mitume wake kwa ghaibu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Mwenye kushinda.”
Siku ya Ufufuo Mwenyezi Mungu atawahukumu waja wake kwa haki, hakuna atakayefanyiwa dhuluma. Qur’an inasema:
وَنَضَعُ الْمَوَازِينَ الْقِسْطَ لِيَوْمِ الْقِيَامَةِ فَلَا تُظْلَمُ نَفْسٌ شَيْئًا ۖ وَإِنْ كَانَ مِثْقَالَ حَبَّةٍ مِنْ خَرْدَلٍ أَتَيْنَا بِهَاۗ وَكَفَىٰ بِنَا حَاسِبِينَۚ
“Nasi tutaweka mizani za uadilifu kwa Siku ya Kiyama. Basi nafsi haitadhulumiwa kitu chochote. Hata ikiwa ni uzito wa chembe ya khardali tutaileta. Nasi tunatosha kuwa washika hisabu.” (21:47).
Sasa, hivi itakuwa halali kumlazimisha mtu kufanya dhambi, halafu uje umhukumu siku ya kiyama? Kama kungekuwa na mahakama yenye kutoa hukumu kama hiyo basi mahakama hiyo ingekuwa haitendi haki kama tutaamini kwamba binadamu hana uhuru, basi hatokuwa na viumbe wengine kwamba yale yanayofanywa nao yanasababishwa na mambo/vitu vilivyo nje ya uwezo wao na wala siyo hiari yao.

Lakini kama Mwenyezi Mungu ameumba mwanadamu na kisha kumfanya awe na uwezo wa kufanya atakavyo ni kama yeye ndiye aliyeumba dhambi na hata kujifanyia mwenza, basi ni vipi, yake ya kuwa mkamilifu itakuwa imetimia?

Itikadi ya kuamini kwamba matendo ya mwanadamu ndiyo yanayosababisha matokeo yote katika maisha ya mwanadamu inaondoa/futa kabisa suala la kuwapo kwa Mitume na Utume (wajibu wao). Mfano suala la ujumbe mtukufu (ufunuo) sheria tukufu zilizoletwa na Mtume kwa wanadamu vitu vyote hivyo havitokuwepo.

Ikiwa tutaamini kuwa matendo yanayofanywa na mwanadamu yanatokana na nguvu fulani na wala siyo nafsi yake kuwa imeamrisha kufanya hivyo basi haitokuwa na maana kuamini Mitume waliletwa ili kumsaidia mwanadamu kiroho na hivyo basi jitihada zote za kumfanya mwanadamu kuwa kiumbe chenye sifa ya kuwa amestarabika zitakuwa pia hazifai.

Lakini ukweli ni kwamba binadamu ana wajibu mkubwa sana katika kuleta ukombozi au maangamizi kwake yeye mwenyewe au wenzie. Chaguo lake ndilo linapoelekea matokeo fulani na punde anapotambua kuwa kila jambo atakalo lifanya litakuwa na matokeo fulani aidha mabaya au mazuri basi atakuwa makini sana katika maamuzi yake. Utegemezi wake kwa Mwenyezi Mungu ndio kutakako mfanya awe na mwanga zaidi.

Inaweza kupingwa/kuhojiwa kwamba kutokana na uwezo mkubwa, tena usio na mipaka wa Mwenyezi Mungu haiwezekani kabisa yeye kutofahamu kile kinachofanywa na mwanadamu, hivyo basi bilashaka yeye Mwenyezi Mungu anahusika katika kila kinachofanywa na mwanadamu huyo.

Jibu: Ni kweli kwamba Mwenyezi Mungu anajua yote, madogo na makubwa lakini hiyo haina maana kwamba binadamu anashurutishwa kwa namna yoyote ile. Lakini suala la ufahamu wa Mwenyezi Mungu hapa lina ambatana na ile kanuni ya chanzo/sababu. Mwenyezi Mungu anajua kwamba mwanadamu atafanya jambo fulani ambalo aidha ni la dhambi au jema na hii inatokana na ule uhuru aliokwisha mpa mwanadamu wa kuchagua hatima yake (destiny).

Matumizi ya uhuru huo ndio unaopelekea matokeo fulani katika matendo ya mwanadamu, kwa hiyo ni wanadamu wenyewe ndio wenye uhuru wa kufanya mambo mema au mabaya kwa kutumia uhuru waliopewa ndio kusema kwamba kama inatokea katika jamii fulani kuna maovu mengi yanatokea hii ni kwa sababu ya mkono ya watu wenyewe sio Mwenyezi Mungu.

Ni kweli kwamba katika ule uhuru tunaozungumzia aliopewa binadamu kuna vitu fulani vinavyopingana katikati, mfano mazingira yanayomzunguka kiumbwa na udhaifu alioumbika nao na vitu vingine ambavyo huweza kuchangia kwa kiasi kikubwa sana hatima ya mwanadamu, yaani kwa maana nyingine vitu hivyo pia huchangia kumfanya mtu awe katika hali fulani.

Lakini yafaa ifahamike wazi kwamba mchango wa vitu hivyo ni katika kusaidia ule uhuru aliopewa mtu na wala si vingine, vitu hivyo havina uwezo wa kumlazimisha mwanadamu kufanya jambo fulani bila matakwa yake; anao uwezo wa kupambana na mazingira na vizingiti vingine.

Hebu fikiria mtaalamu wa magari anakagua gari kabla haijaonekana na kukuta kwamba ina udhaifu fulani hivyo akatabiri kwamba gari haiwezi kufika mbali kabla haijapatwa na matatizo. Sasa kama gari itaondoka na kabla haijafika mbali kweli gari inapatwa na matatizo, je, hapa tutasema kwamba yule mtaalamu amehusika katika kuifanya ile gari ishindwe kufika kule ilikokusudiwa? Eti kwa sababu alishatabiri kwamba gari ile isingefika mbali. Bila shaka kila mtu mwenye akili timamu atakiri matatizo yaliyopo katika gari ndio yoliyopelekea kushindwa kwa gari kufika mbali.

Mfano mwingine, mwalimu wa somo Fulani amemtabiria mwanafunzi wake mmoja kwamba atafeli mtihani wake kutokana na mwanafunzi huyo kuwa mvivu. Mara matokeo yametoka na mwanafunzi yule kweli akafeli sasa hapa kilichohusika katika kumfanya yule kijana afeli ni ule uzembe/uvivu wake darasani au utabiri wa mwalimu?

Bila shaka hapa uzembe wake ndio uliomfanya afeli. Mifano hii inaonyesha kwamba uwezo wa Mwenyezi Mungu kujua yajayo n.k. sio kigezo cha kumfanya mwanadamu kutokuwa na uhuru juu ya matendo yake.

Moja wapo ya madhara ya itikadi ya kutokuamini kuwa mwanadmau ana dhima juu ya vitendo vyake ni kuifanya jamii kuwa na kibri kwa kuhisi kwamba wao wamepewa haki ya kuonea na Mwenyezi Mungu kwa sababu mambo yote wanayoyafanya yameshapangwa na Mola.

Mabepari na makundi mengine ya watu katika historia walitumia dhana hiyo ‘ya kuamini kuwa binadamu hana wajibu wowote juu ya matendo yake’ kuendeleza udhalimu wao kwa kisingizio cha kwamba wao wamepewa uwezo na mamlaka na Mwenyezi Mungu hivyo hawatakiwi kupingwa.

Wakati (mmoja wa wanawake katika) familia ya (Doyen) aliyekufa shahidi Imam Al-Husayn ibn Ali amani iwe juu yake, siku moja aliulizwa na Ibn Ziyad kwamba ameshuhudia jinsi Mwenyezi Mungu alivyofanya kwa kaka yake na familia yake?

Yule binti akamjibu kwamba yeye hakuona chochote kibaya kilichofanyika kwa kaka yake al-Husayn kwani yote yaliyotokea yametoka kwa Mwenyezi Mungu; akaendelea kusema ndugu zake wamefanya yale walioamrishwa na Mola wao na kwa hakika sisi wote tutakusanywa siku hiyo mbele ya Mola na kisha ndipo huko itajulikana kuwa nani amesalimika na adhabu ya Mola!

Kuhusiana na kutokuwa na uhuru, watu wasio amini siku ya Mwisho wanajikuta wapo katika matatizo; kwa upande mmoja wanaona mwanadamu hana tofauti na vitu vingine kuwa hana lengo lolote isipokuwa kustarehe tu na baadae kutoweka na kwamba anakabiliwa na mabadiliko ya kila aina na kuwa wakati akijitahidi katika harakati za kujiletea maendeleo kwa hakika hutegemea mazingira tu. Mageuzi yoyote yale ya kijamii yanatokana tu na mabadiliko katika mazingira anayoishi mwanadamu huyo.

Kwa mujibu wa mahusiano baina ya chanzo na matokeo au sababu yakutukia kwa jambo fulani na matokeo yake, hakuna kitu kinachotokea bila ya chanzo chochote sambamba na ule uhuru wa kujiamulia mambo alionao mwanadamu. Mwanadamu analazimika kuchagua hatima (njia) ambayo inakuwa imetokana na mazingira na udhaifu wa akili yake. Kwa hiyo hakuna nafasi yoyote kwa mwanadamu kuwa na nafasi ya kuamua mambo yanayomhusu.

Lakini wakati huohuo wale watu wasioamini itikadi yoyote ya kidini wanamchukulia mwanadamu kuwa ni kiumbe chenye uwezo wa kuathiri mazingira yake; pia kundi hili la watu wasioamini dini wamepatia mwandamu sifa na nafasi ya juu katika viumbe. Wao wana waasa watu wanaoathiriwa na mifumo na itikadi mbali mbali za kibepari kuamka na kupambana na watu hao na hiyo yote ni kutokana na kutumia ule uhuru walionao wanadamu.

Kama makafiri wanadai kwamba kuwahamasisha watu wanaonyanyaswa ili kudai haki zao huwa kunachochea kuzaliwa kwa miundo mipya ya maisha (mabadiliko ya kiutawala) katika jamii basi itakuwa haileti maana kwa sababu tayari wao walisha dai kwamba kila kinachotokea katika jamii kipo nje ya uwezo wa mwanadamu badala yake (Nature) asili/mazingira na wakati ndio hupelekea mabadiliko hayo; hivyo basi kuhamasisha watu (kuleta) mifumo mbalimbali ya maisha iliyo kinyume na matakwa yao ni sawa na kazi bure.

Pia inaweza kusemwa kwamba uhuru pia hujumuisha kuzijua kanuni za mazingira/asili ili kuweza kuzitumia kwa mintarafu/makusudi ya kufikia malengo fulani lakini hiyo bado haijatosha kuelezea swala asili (Nature) kuwa ndio yenye kuleta mabadiliko hayo kwa sababu sio asili inayomlazimisha mwanadamu kufanya mambo fulani isipokuwa binadamu ndiye mwenye kuchagua kanuni au taratibu zipi za kuzifuata miongoni mwa hizo kanuni za mazingira/asili.

Kama Mwanadamu yuko huru kuchagua, je, matakwa na maamuzi yake yanategemea asili/mazingira?

Makafiri wanamchukulia binadamu kuwa ni kiumbe chenye kiasi kwamba hata imani yake, mitazamo yake vyote vinatokana na kuathiriwa katika aidha siasa au uchumi, kwa kifupi ni kwamba katika harakati za kushughulikia matazi yake ya kiuchumi na mambo mengineyo ndipo humfanya (awe na) itikadi katika mfumo fulani.

Ni kweli kabisa kwamba binadamu kwa kiasi fulani huweza kuathiriwa na hali ya kijiografia na maumbile ya kitu n.k. lakini pia kuna mambo mengine ambao yanatokana na akili ya mwanadamu mwenyewe hupelekea kupata hatima fulani.

Hamna shaka kwamba binadamu yu katika uelekeo wa kuvutwa na mazingira na kwamba nguvu/mvuto wa kihistoria na kiuchumi huweza kupelekea kuibuka kwa matukio fulani lakini yafaa ikumbukwe kwamba hatima ya binadmau inategemea mwanadamu mwenyewe na wala sio mazingira pamoja kwamba mazingira huweza kuchangia kwa kiasi fulani.

Binadamu hajafungwa na asili, bado anao uwezo mkubwa wa kuyatumia mazingira kwa makusudio mbalimbali kama ilivyo, mabadiliko ni kitu cha lazima sana katika maisha; yawe maisha ya mtu au kitu kwa hiyo binadamu na yeye hakuachwa pekee naye yumo katika mkumbo wa kukumbwa na mabadiliko hayo.

Katika Qur’an kuna aya nyingi sana ambazo zinaonyesha ni kwa vipi vitu kama maonevu, dhuluma (ukosefu wa haki) madhambi pamoja na rushwa vimebadili historia ya watu fulani Qur’an (17:16).
 
وَإِذَا أَرَدْنَا أَنْ نُهْلِكَ قَرْيَةً أَمَرْنَا مُتْرَفِيهَا فَفَسَقُوا فِيهَا فَحَقَّ عَلَيْهَا الْقَوْلُ فَدَمَّرْنَاهَا تَدْمِيرًا
“Na pindi tukitaka kuuteketeza mji huwaamrisha wale wenye starehe na taanusi, lakini wao huendelea kutenda maovu humo. Basi hapo kauli huthibiti juu ya mji huo, nasi tukauangamiza kwa maangamizo makubwa.”
Pia tazama Qur’an (89:6-14).
أَلَمْ تَرَ كَيْفَ فَعَلَ رَبُّكَ بِعَادٍ ۖإِرَمَ ذَاتِ الْعِمَادِ ۖالَّتِي لَمْ يُخْلَقْ مِثْلُهَا فِي الْبِلَادِ ۖوَثَمُودَ الَّذِينَ جَابُوا الصَّخْرَ بِالْوَادِ ۖ وَفِرْعَوْنَ ذِي الْأَوْتَادِ ۖالَّذِينَ طَغَوْا فِي الْبِلَاد ۖفَأَكْثَرُوا فِيهَا الْفَسَادَ ۖفَصَبَّ عَلَيْهِمْ رَبُّكَ سَوْطَ عَذَابٍ ۖإِنَّ رَبَّكَ لَبِالْمِرْصَادِ ۚ
“Kwani hukuona jinsi Mola wako Mlezi alivyo wafanya kina A'di? Wa Iram, wenye majumba marefu? Ambao haukuumbwa mfano wake katika nchi? Na Thamudi walio chonga majabali huko bondeni? Na Firauni mwenye vigingi?
Ambao walifanya jeuri katika nchi? Wakakithirisha humo ufisadi? Basi Mola wako Mlezi aliwapiga mjeledi wa adhabu. Hakika Mola wako Mlezi yupo kwenye mavizio anawavizia.”
Pia Qur’an inatukumbusha kuwa watu wanaoabudia matakwa yao na kuutii upotofu wao husababisha maafa makubwa sana katika jamii tazama Qur’an (28:4).
إِنَّ فِرْعَوْنَ عَلَا فِي الْأَرْضِ وَجعَلَ أَهْلَهَا شِيَعًا يَسْتَضْعِفُ طَائِفَةً مِنْهُمْ يُذَبِّحُ أَبْنَاءَهُمْ وَيَسْتَحْيِي نِسَاءَهُمْۚ
إِنَّهُ كَانَ مِنَ الْمُفْسِدِينَۚ
“Hakika Firauni alitakabari katika nchi, na akawagawa wananchi makundi mbali mbali. Akalidhoofisha taifa moja miongoni mwao, akiwachinja watoto wao wanaume na akiwaacha watoto wao wanawake. Hakika yeye alikuwa katika mafisadi.”
Pia Qur’an (43:54)’inaeleza:
فَاسْتَخَفَّ قَوْمَهُ فَأَطَاعُوهُ ۚ إِنَّهُمْ كَانُوا قَوْمًا فَاسِقِينَۚ
“Basi aliwachezea watu wake, na wakamtii. Kwa hakika hao walikuwa watu wapotovu.”
Ni mara ngapi umwagaji wa damu, uharibifu wa mali na mvurugano katika jamii ni matokeo ya kupenda madaraka na watu kupenda mambo maovu?
Binadamu ambaye ni sehemu ya jamii anayo akili na uhuru/matakwa kabla hata ya kuwa mwanachama wa jamii husika kwa maana nyingine ukiachilia mbali yale mambo yaliyopo katika jamii ambayo kila mwanajamii anawajibika kuyafuata yeye (mtu) ana mambo ya kwake mwenyewe.
Wapo wale wenye kuamini kwamba watu ambao ndio wanaojenga jamii wanachukua nafasi sawa yaani kila mwanajamii yuko sawa na mwingine, kitu ambacho siyo sahihi.
Ukweli ni kwamba pamoja na jamii kuwa ina nafasi na mamlaka makubwa kuliko mtu binafsi lakini hiyo haina maana kwamba mwanajamii huyo analazimika kufuta kila jambo la jamii hiyo.
Japokuwa Uislamu unasisitiza juu ya Umoja na kwamba wenyewe una nguvu fulani kwa wanachama wake lakini bado unatambua kwamba mtu binafsi anao uhuru; uhuru mkubwa wa kukubali ama kupinga jambo fulani linalotendeka katika jamii.
Qur’an tukufu inasema:
يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا عَلَيْكُمْ أَنْفُسَكُمْ ۖ لَا يَضُرُّكُمْ مَنْ ضَلَّ إِذَا اهْتَدَيْتُمْ ۚ إِلَى اللَّهِ مَرْجِعُكُمْ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُكُمْ بِمَا كُنْتُمْ تَعْمَلُونَۚ
“Enyi mlioamini shikilieni imani yenu imara kwani kwa kuwa kwenu imara kutawafanya hata wengine wenye upotovu washindwa kuwashawishi kufuata upotovu wao.” Qur’an (5:105).
Pia katika Qur’an (4:97) Mwenyezi Mungu anasema:
إِنَّ الَّذِينَ تَوَفَّاهُمُ الْمَلَائِكَةُ ظَالِمِي أَنْفُسِهِمْ قَالُوا فِيمَ كُنْتُمْ ۖ قَالُوا كُنَّا مُسْتَضْعَفِينَ فِي الْأَرْضِ ۚ قَالُوا أَلَمْ تَكُنْ أَرْضُ اللَّهِ وَاسِعَةً فَتُهَاجِرُوا فِيهَا ۚ فَأُولَٰئِكَ مَأْوَاهُمْ جَهَنَّمُ ۖ وَسَاءَتْ مَصِيرًاۚ
“Watakapo kufa watu malaika watawauliza mlifanya nini huko duniani? Watu watajibu “sisi tulikuwa watu dhaifu na hatukuwa na nguvu zozote.” Malaika watasema: “ardhi ya Mwenyezi Mungu haikuwa kubwa kwa ninyi kuweza kukimbia kwenda sehemu nyingine ili mkajipatie uwezo?” (Kujikwamua).

Katika aya hii wale wanaosema kwamba sisi tunaishi kwa mujibu wa jamii yetu ilivyo wanashutumiwa na madai ya kutokutimiza amri ya Mwenyezi Mungu siku hiyo hayatokubaliwa.

Ili mwanadamu aweze kuendelea kiroho na kiakili, uwepo wa uhuru wa fikra (mawazo) ni jambo lisilo epukika.

Binadamu ana thamani na thamani yake hiyo itaonekana tu pale atakapotumia ule uhuru wake wala sio kusifiwa. Ni kama mwanadamu hana uhuru kabisa katika maisha yake basi pia hana sababu ya kusifiwa kwa mabaya au mema yake aliyoyafanya kwa sababu sio yeye aliyefanya isipokuwa yeye amelazimishwa tu.

Hivyo basi hakuna kitu chochote kinachomfanya mwanadamu achague mwelekeo/njia fulani ya maisha ila nafsi yake mwenyewe/mapenzi yake.
Wale wanaounyanyua mkono ya itikadi kuwa mtu ana uhuru kamili katika matendo yake anaweza kuamua kadiri atakavyo, mfano majukumu aliyonayo mwanadamu, adhabu zitolewazo kwa wahalifu. Mambo yanayofanywa na jamii ili kuleta mabadiliko ya kihistoria, misingi ya sayansi na teknologia yote hayo yanaonyesha kwamba binadamu yuko huru katika matendo.

Hali kadhalika suala la wajibu alionao mtu katika kutekeleza sheria za dini, ujio wa Mitume na suala la ufufuo na hukumu, vyote hivyo bado vinaonyesha kwamba binadamu huyu yuko huru kabisa.

Itakuwa haina maana endapo Mwenyezi Mungu kwa upande mmoja akawa anawalazimu waja wake kufanya mambo halafu akataraji kuwahukumu au kuwazawadia, halitakuwa jambo la haki kwa muumba wa jambo tulifanyalo liwe amelipanga yeye kisha aje kutuhukumu kutokana na yale tuliyofanya kwa kulazimishwa na yeye.

Kama kila linalofanywa na mtu lina ridhaa, ukatili na maovu yote yanayotendeka katika jamii iwe ni kazi yake yeye Mwenyezi Mungu sifa ambazo ni kinyume kabisa. Kama kweli binadamu asingekuwa na uhuru katika mambo yake basi pasingekuwa na sababu ya kuwashutumu viongozi madhalimu wanyonyaji n.k.

Binadamu ana haki ya kulaumiwa au kusifiwa pale tu anapokuwa ana uhuru katika matendo yake, vinginevyo sifa zote na lawama kwake hazina maana.

Wale wanaoshikilia msimamo huo wameenda mbali sana, wamevuka mpaka kiasi kwamba wanaamini huo uhuru alionao mwanadamu hauna kikomo. Kwa maana nyingine Mungu hana uwezo wa kuzuia matendo ya binadamu; kwa kifupi huo ndio msimamo wa wale wanaoamini kwamba binadamu yu huru.

Wale wanaosema kuwa ni asili tu na matokeo ya matakwa ya mwanadamu ndio vinavyopelekea kutokea kwa mambo mengi duniani wala vitu hivyo havina uhusiano na kuwepo kwa Mwenyezi Mungu. Hawa wanajaribu kupinga uwepo wa Mwenyezi Mungu (swt). Kwa maana nyingine wanajaribu kumwekea Mwenyezi Mungu mwenza katika Uumbaji wake bila ya wao wenyewe kujua.

Kwa hakika kwa msimamo huo, binadamu amejikuta amejiingiza katika itikadi ya ukafiri/ushirikina kukubali kwamba binadamu kabisa kabisa ana uhuru kamili usioweza kuingiliwa na kitu kingine hata Mwenyezi Mungu; itakuwa kupunguza mamlaka ya Mwenyezi Mungu kwa viumbe vyake, wakati ukweli ni kuwa mamlaka aliyonayo Mwenyezi Mungu kwa ulimwengu hauna mipaka.

Wakati tunakubali kuwa kuna mazingira ambayo huwa na nafasi fulani katika mabadiliko ya Mwanadamu sharti tukubali kuwa hata hayo mazingira yana uhusiano na Mwenyezi Mungu na lazima tukubali kuwa kama Mungu akitaka hata hayo mazingira yasingeweza kuwepo.

Kama ilivyo kuwa, viumbe wote hapa duniani hawana uhuru wakuamua uwepo au kutokuwepo kwao isipokuwa wote wanategemea Mwenyezi Mungu, vivyo hivyo viumbe hivyo vinakosa nafasi ya kuwa ndio vyanzo. Mambo yatukiayo hapa duniani hivyo basi tunashawishika kuamini vitu vyote vipo chini ya Mwenyezi Mungu, si tu uwepo wake bali hata matendo yao.

Hatuwezi kulinganisha uhusiano wa Mwenyezi Mungu na viumbe vyake kuwa sawa na ule wa mwanasanaa na kazi yake, mfano mpakaji akishapaka rangi sehemu basi ule uzuri wa rangi hautegemei tena mpakaji kwa sababu mpakaji aweza kuondoka na uzuri ukabakia. Kwa hiyo kuamini hivyo ni sawa na kumshirikisha Mwenyezi Mungu.

Yoyote yule anayekanusha wajibu majukumu ya Mwenyezi Mungu katika mambo na matendo mbalimbali huyo atakuwa anamwekea Mwenyezi Mungu mipaka katika mamlaka yake na wale wanaoamini hivyo basi atajiona kuwa yeye hana hatia kwa maovu anayoweza kuwatendea wenzie hivyo itikadi kama hiyo ikitawala jamii, basi jamii hiyo haitakuwa na ustawi, amani na utulivu.

Kinyume chake wale watu wanaoishi kwa kuamini kwamba Mwenyezi Mungu yupo na ni yeye ndiye mtawala wa kila kitu, wataishi maisha bora na ya amani kwa sababu kila mmoja atahisi anawajibu wa kutimiza kwa yule aliyemleta hapa duniani ushahidi wa kuonyesha kwamba hana mshirika, tazama Qur’an tukufu (17:111).
وَقُلِ الْحَمْدُ لِلَّهِ الَّذِي لَمْ يَتَّخِذْ وَلَدًا وَلَمْ يَكُنْ لَهُ شَرِيكٌ فِي الْمُلْكِ وَلَمْ يَكُنْ لَهُ وَلِيٌّ مِنَ الذُّلِّ ۖ وَكَبِّرْهُ تَكْبِيرًاۚ
“Na sema: Alhamdulillah, Himdi zote ni za Mwenyezi Mungu ambaye hana mwana, wala hana mshirika katika ufalme, wala hana rafiki wa kumsaidia kwa sababu ya udhaifu wake. na mtukuze kwa utukufu mkubwa.”
Mwenyezi Mung anasema: Qur’an (5:120).
لِلَّهِ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا فِيهِنَّ ۚ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌۚ
“Mwenyezi Mungu ndiye anayethibiti vyote vilivyo mbinguni na vilivyo ardhini na ana mamlaka juu ya vitu vyote hivyo.”
Pia tazama Qur’an (35:44).
أَوَلَمْ يَسِيرُوا فِي الْأَرْضِ فَيَنْظُرُوا كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الَّذِينَ مِنْ قَبْلِهِمْ وَكَانُوا أَشَدَّ مِنْهُمْ قُوَّةً ۚ
وَمَا كَانَ اللَّهُ لِيُعْجِزَهُ مِنْ شَيْءٍ فِي السَّمَاوَاتِ وَلَا فِي الْأَرْضِ ۚ إِنَّهُ كَانَ عَلِيمًا قَدِيرًاۚ
“Je! Hawakusafiri katika ardhi wakaona vipi ulikuwa mwisho wa waliokuwa kabla yao? Na hao walikuwa wana nguvu zaidi kuliko wao. Na hapana kitu kinacho weza kumshinda Mwenyezi Mungu mbinguni wala katika ardhi. Hakika Yeye ni Mwenye, kujua, Mwenye uweza.”
Viumbe vya ulimwengu huu vinahitaji Mwenyezi Mungu ili viweze kuishi kama vile vilivyo hitaji Mungu ili kuwepo/kuja duniani, ubunifu pamoja na matokeo yake ni sawa na ule wa Mwenyezi Mungu kwa sababu ni mwendelezo wa nguvu zake hizo; wao ni wajanja sana kwa kuwa wameweza kuvumbua mambo na vitu mbalimbali bali wanatakiwa waelewe kuwa uwezo huo wamegewa na Mwenyezi Mungu.

Kama ilivyo kwa taa ya umeme ili iweze kuendelea kutoa mwanga, sharti ipate nguvu kutoka katika kituo cha nguvu ya umeme (mfano bwawa la Mtera kwa Tanzania) kwa sharti pawe na chanzo na kisha pawe na umeme ambao pasipo huo, taa hiyo haiwezi kuwaka.

Qur’an tukufu inasema katika surat Faatír (35:15) kwamba

“Binadamu wote wanamhitajia Mungu wala yeye Mwenyezi Mungu si muhitaji kwa wanadamu”.

Al-Imam Ja’afar as-Sadiq a.s, amani iwe juu yake amesema: “Mamlaka/uwezo na nguvu za Mwenyezi Mungu ni kubwa sana kwa nguvu nyingine kuwepo katika dunia bila idhini yake.”

Laiti kama Mwenyezi Mungu asingetujalia kuwa na uhuru na kama asingekuwa anatupa nguvu kila wakati kwa kweli tusingeweza kufanya kitu chochote kile, kwani tunaweza kusema kwamba uhuru tulio nao umejigawa katika tapo (2) mbili yaani kwa upande mmoja kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwa upande mwingine kutoka kwetu sisi wenyewe. Tunaweza kutumia mali ghafi (vitu tulivyopewa na Mungu) aidha kwa manufaa kiuchumi au tunaweza kutumia vibaya hatimae vikatuathiri.

Fikiria kwamba kuna mtu ana moyo wa bandia ambayo tunaweza kuzima betri hiyo au kuwasha hatimae moyo ukafanya kazi; kile tulichokidhibiti pale ni ule mkondo wa umeme unaotoka katika betri na kwenda katika ule wa umeme.

Mara baada ya kuwekwa betri moyo ule utafanya kazi na mtu yule akawa yu katika pilika pilika zake; mfano akiwa anafanya mambo mabaya au mazuri hiyo itatokana na matakwa yake mwenyewe wala siyo wewe uliye muunganisha na betri. Kwa maana nyingine jinsi ya kutumia mkondo ule wa umeme au atakachofanya mara baada ya kuunganishwa na betri ni juu yake.

Vivyo hivyo uwezo tulio nao unafanana sana na suala hili, Mwenyezi Mungu anao uwezo muda wowote wa kutupa nguvu zinazotufanya tufanye shughuli zetu.
Kila kiumbe hapa duniani kinapata muongozo fualni ambao ndio unawafanya wafikie hatua ya maendeleo.

Tunafahamu kwamba mimea ina kazi kubwa ya kupambana na mazingira yake pamoja na ukweli kwamba hujifanya ngangari ili kuyashinda mazingira hayo, tukichunguza sifa za mimea na wanyama utagundua kuna tofauti kubwa sana baina ya makundi hayo mawili ya viumbe hai.

Ili wanyama waweze kujipatia mahitaji yao (chakula) hawana budi kujihusisha katika pilika pilika nyingi zaidi kuliko mimea. Wana hitaji nyenzo kadhaa katika kufikia mafanikio yao.

Japokuwa wanyama wanaonekana kuwa wanaathiriwa sana na silka lakini kuna wakati huwa na uhuru katika mambo yao. Binadamu ambaye amefikia hatua kubwa sana ya maendeleo kutokana na kuwa na uhuru kamili katika matendo yake ana kiwango kidogo sana cha hulka. Mazingira yanatosheleza kwa kiwango fulani mahitaji ya mimea. Kwa upande wa wanyama japokuwa mama anawajibika kufanya juhudi fulani kumbeba, kumnyonyesha na hata kumlinda mtoto wake huyo na madhara mbalimbali, hulka huonekana mapema sana kwa mtoto, mfano mama halazimiki sana kuchukua hatua za kumfundisha mtoto.

Lakini kwa binadamu tunakuta kwamba hana kiwango kikubwa cha hulka kiasi kwamba uwezo wake wa kupambana na hali isiyofaa kutoka katika mazingira yake ni dhaifu ukilinganisha na wanyama. Hivyo kiwango cha utegemezi kwa wazazi wake kinakuwa ni kikubwa sana na huendelea kwa muda mrefu sana mpaka pale mtoto wa (binadamu) anapofikia kujitegemea kwa kutumia viungo vyake.

Qur’an tukufu inaelezea kwa makini juu ya udhaifu wa mwanadamu, tazama Qur’an (4:28) .
يُرِيدُ اللَّهُ أَنْ يُخَفِّفَ عَنْكُمْ ۚ وَخُلِقَ الْإِنْسَانُ ضَعِيفًاۚ
“Mwenyezi Mungu anataka kukupunguzieni taabu, na Mwanadamu ameumbwa dhaifu”
Mazingira/asili imemwacha mwanadamu katika hali ya kuwa huru zaidi kuliko ilivyokuwa kwa wanyama. Tunaona kuwa binadamu kwa upande mwingine kuwa ana uhuru usioweza kuelezeka na kukua kwa ufahamu.

Wakati binadamu akifurahia uhuru alionao, binadamu amekuwa na uhuru wa kuchagua mambo anayoyataka, lazima kutakuwa na kitu kitachokuwa kinapinga hulka.

Mara binadamu anapokuwa katika migogoro, kamwe hatoweza kupata ustawi (utulivu) au hawezi kabisa katika hali hiyo ya mgogoro kuchagua njia iliyo bora. Ukizingatia kwamba binadamu, yeye ndiye aliyeamua kubeba jukumu kubwa kabisa, jukumu la kuufikisha ujumbe wa Mwenyezi Mungu na kuutekeleza kama inavyopaswa kazi ambayo mbingu na ardhi zimeshindwa kulibeba jukumu hilo. Kwa hiyo binadamu anajikuta anakabiliwa na mambo mawili; nayo ni ama aamue kuwa mfungwa/mtumwa wa hulka na tamaa isiyo na kipimo hivyo ikampeleka pabaya au kwa kutumia uwezo mkubwa wa akili na uhuru ili aweze kujiletea maendeleo yake.

Mara mwanadamu anapokuwa amejitoa kutoka katika shuruti yaani kushurutishwa kufuata mfumo au kitu chochote kile ambacho nafsi yake haipendi (hulka) hapo huwa amekatilia mbali minyororo ya utumwa na hatimae kutumia uwezo wake wa kuzaliwa na ule wa kujifunza, basi muundo wake wa fahamu hautopotea; hii ni kutokana na ukweli kwamba kadiri mtu anapotumia sana sehemu ya kiungo cha mwili wake ndipo kiungo hicho kinavyoweza kuendelea, akikiacha bila ya kutumia hudumaa.

Uwezo wa kumiliki sayansi na kustarabika, yote haya ni matokeo ya uhuru alionao mwanadamu; mara binadamu anapopata uhuru kamili na akaendelea na juhudi zake za kujiletea manufaa basi uwezekano wa kuendelea mbele ni mkubwa sana kadiri ya kipawa alichonacho na uwezo wake unavyokomaa ndipo atakapobadilika kuwa ni chanzo cha ustawi katika jamii.

Matokeo ya uhuru wa binadamu hivi sasa yanaonekana katika kila kona. Na sasa hebu tuone ni kitu gani kinachoweza kumzuia mtu kutotumia uhuru au vikwazo vilivyopo katika utumiaji na uwezo aliopewa mwanadamu.

Mtazamo sahihi wa shia ambao wameutoa kutoka katika Qur’an na pia kutokana na maneno ya Maimam ambayo yanawakilisha ‘mtazamo wa tatu’ ambao baina ya makundi yale mawili nayo ni yale ya wale wanaosema kwamba binadamu yupo huru kabisa na lile kundi linalosema kwamba binadamu yupo katika namna mbili (2), anao uhuru na pia uhuru wake umedhibitiwa kwa kiasi fulani.

Ni wazi kwamba uhuru tulionao katika matendo yetu unatofautiana sana na jinsi jua linavyotembea, pia mwezi, na dunia au jinsi mimea yanavyo kuwa na wanyama wanavyotembea, uhuru tulionao katika kuchagu kufanya mambo mema au mabaya unatokana na nafasi ya maamuzi yaliyopo katika nafsi zetu.

Sasa ni wajibu wetu kutumia nafasi hiyo kwa umakini, kabla ya kufanya jambo sharti tulipime hilo jambo na hatimae kufanya maamuzi sahihi. Haya ni mapenzi yake Mwenyezi Mungu kwamba sisi waja wake tuwe na nafasi/uamuzi katika mambo yetu.

Kila tunalolifanya katika ulimwengu sharti litakuwa tayari limeshatambuliwa na Mwenyezi Mungu. Kila nyanja ya maisha yetu sharti Mwenyezi Mungu awe ana ujuzi nalo.

Kwa hiyo Mwenyezi Mungu anayatazama matendo yetu kwa karibu sana kiasi kwamba sisi wenyewe hatuna uwezo wa kutambua jinsi yeye anavyoshughulikia mambo yetu.

Mwisho, uhuru wetu hauwezi kuvuka mipaka ya mapenzi yake yeye (Mwenyezi Mungu) pamoja na kuwa na uwezo wa kuyatawala mazingira yake bado mwanadamu anadhibitiwa na mambo fulani ambayo yako nje ya uwezo wake, mfano amekuja hapa duniani bila ya ridhaa yake na pia hufunga macho (kufa) bila ridhaa yao.

Al-Imam Ja’afar as-Sadiq a.s amani iwe juu yake amesema

“ kwa hakika mwanadamu hayupo katika makundi yote haya mawili yaani kwamba ana uhuru kamili au matendo yake yanadhibitiwa na Mwenyezi Mungu bali yupo baina ya makundi haya mawili.”

Ni sawa kuwa mwanadamu anao uhuru katika mambo yake lakini kuamini kwamba uhuru alionao hauna mipaka ni sawa kabisa na kumshirikisha Mwenyezi Mungu kwa sababu yeye pekee ndiye mwenye mamlaka yasiyo na mipaka. Bali uhuru alionao mwanadamu umewekwa na Mwenyezi Mungu nao una mipaka yake kutegemea mapenzi yake Mwenyezi Mungu.

Kwa mtazamo wa Uislamu binadamu siyo kiumbe kilichopo bila ya makusudio yoyote; yule aliyemuumba mwanadamu amempa mwongozo ili kwa kuufuata huo atakuwa amefikia lengo la kuumbwa kwake, mfano amepewa akili, maarifa, uwezo wa kutambuana, kubuni. Makosa yaliyofanywa na makundi yote mawili ni kudhani kwamba huyu binadamu yuko katika uelekeo wa aina mbili tu, mmoja ni ule kuwa binadmu hana hata chembe ya uhuru katika mambo yake, kila analofanya limepangwa na Mwenyezi Mungu au kuwa anao uhuru usio na mipaka katika matendo, kitu ambacho itakuwa sawa na kumwekea Mwenyezi Mungu mwenza (shirki).

Bali ukweli ni kwamba matendo ya mwanadamu kwa upande mmoja yanaweza kuyahusisha mwanadamu mwenyewe na kwa upande mwingine sharti yahusishwa na Mwenyezi Mungu; yaani binadamu anahusika katika matendo yake uhusika wa Mwenyezi Mungu sio wa moja kwa moja, lakini mahusiano yote hayo ni kweli na sahihi kabisa, tazama Qur’an tukufu (2:6-7).

“Hakika wale walio kufuru ni sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye, hawaamini. Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao na juu ya masikio yao, na juu ya macho yao pana kifuniko. Basi watapata adhabu kubwa.”

Wakati mwingine madhambi yanaweza kuwa siyo makubwa kiasi kwamba nafasi ya msamaha isiwepo hali yapo madhambi ambayo mtu akiyafanya anao uwezo wa kuomba msamaha.

Lakini kuna madhambi mengine ukiyafanya Mwenyezi Mungu ndio kwanza anakuelekeza huko huko na huweka alama/kizibo nyoyo za watu kama hao. Imam amekaririwa akisema kwamba Mwenyezi Mungu ameumba kila kitu kwa lengo yaani kila tukio, jambo linalotokea lazima pawepo na chanzo cha kutokea kwa hicho kitu/jambo. Mojawapo ya chanzo alichoumba ni mwanadamu na uhuru alionao mwanadamu ili kuweza kwenda sambamba na ile kanuni isemayo kila jambo lina chanzo chake.

Hii ni kanuni muhimu sana katika maisha yetu; machaguo yetu na matakwa tulionayo yanakuja kuchukua nafasi ya mwisho kabisa katika muundo ule wa vyanzo.

Aya za Qur’an zinazoelezea mambo yote na Mwenyezi Mungu (yaani kwamba kila kitu kinahusishwa moja kwa moja na Mwenyezi Mungu) hizi zinaelezea ule mfumo kwamba vitu vyote asili yake ni yeye kwa sababu yeye ndiye wa mwanzo ndiye mbunifu wa kila kile kinacho onekena na kisicho onekana. Hata ule uhuru tunaosema kwamba binadamu anao, yeye ndiye aliyempa mwanadamu kwa hiyo mwanadamu amepewa uhuru wa kufuata matamanio ya nafsi yake yeye mwenyewe ili asije akalaumu kwamba amepangiwa njia ya kufuata.

Kama kuna shuruti/lazima yoyote ni ile kufuata matamanio ya nafsi yake kwa kuwa hilo lilishapangwa na Mwenyezi Mungu kwamba mwanadamu sharti atumie akili yake katika baadhi ya mambo katika maisha yake. Lakini sio kwamba mwanadamu hulazimishwa kufanya mambo na Mwenyezi Mungu.

Hivyo tunapofanya mambo mazuri uwezo ule wa kufanya mambo hayo unatoka kwake Mwenyezi Mungu isipokuwa chaguo la kufanya linatoka kwetu yaani chaguo la kutumia uwezo ule unatoka kwake Mwenyezi Mungu. Kuna aya nyingi zinazoonyesha kuwa Mwenyezi Mungu anatambua kwamba huyu mwanadamu ana uhuru, mfano tazama Qur’an (99:7-8).
فَمَنْ يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ خَيْرًا يَرَهُۚ وَمَنْ يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ شَرًّا يَرَهُۚ
“Basi anaye tenda chembe ya wema, atauona! “Na anaye tenda chembe ya uovu atauona!
“Kwa hakika mnawajibika kwa matendo yenu mnayoyatenda” Qur’an (16:93).
وَلَوْ شَاءَ اللَّهُ لَجَعَلَكُمْ أُمَّةً وَاحِدَةً وَلَٰكِنْ يُضِلُّ مَنْ يَشَاءُ وَيَهْدِي مَنْ يَشَاءُ ۚ وَلَتُسْأَلُنَّ عَمَّا كُنْتُمْ تَعْمَلُونَۚ
“Na Mwenyezi Mungu angelitaka, kwa yakini angeli kufanyeni Umma mmoja. Lakini anamwachia kupotea anaye mtaka na anamwongoa amtakaye. Na hakika mtaulizwa kwa yale mliyo kuwa mkiyafanya.”
Pia tazama Qur’an (6:148).
سَيَقُولُ الَّذِينَ أَشْرَكُوا لَوْ شَاءَ اللَّهُ مَا أَشْرَكْنَا وَلَا آبَاؤُنَا وَلَا حَرَّمْنَا مِنْ شَيْءٍ ۚ كَذَٰلِكَ كَذَّبَ الَّذِينَ مِنْ قَبْلِهِمْ حَتَّىٰ ذَاقُوا بَأْسَنَا ۗ قُلْ هَلْ عِنْدَكُمْ مِنْ عِلْمٍ فَتُخْرِجُوهُ لَنَا ۖ إِنْ تَتَّبِعُونَ إِلَّا الظَّنَّ وَإِنْ أَنْتُمْ إِلَّا تَخْرُصُونۚ
“Na watasema walio shirikisha: Lau kuwa Mwenyezi Mungu angetaka tusingeli shiriki sisi, wala baba zetu, wala tusingeli harimisha kitu chochote. Vivi hivi walikanusha walio kuwa kabla yao mpaka walipo onja adhabu yetu. Sema: Je, nyinyi mnayo ilimu mtutolee? Nyinyi hamfuati ila dhana. Wala hamsemi ila uwongo tu.”
Kama ingekuwa uokovu na upotovu wa binadamu unategemea tu matakwa ya Mwenyezi Mungu basi pasinge kuwepo na hata chembe ya udhalimu katika dunia/ardhi. Kungekuwa na uongofu tu. Baadhi ya watu waovu ambao wamedai kwamba kila jambo walilolifanya liwe baya au jema lilikuwa na ridhaa ya Mwenyezi Mungu, Qur’an ina sema tazama (7:28).
 وَاللَّهُ أَمَرَنَا بِهَا ۗ قُلْ إِنَّ اللَّهَ لَا يَأْمُرُ بِالْفَحْشَاءِ ۖ….
“....na Mwenyezi Mungu ametuamrisha hayo. Sema: Hakika Mwenyezi Mungu haamrishi mambo machafu”.
Kama ilivyo kwamba Mwenyezi Mungu atawalipa mema wale waliofanya mambo mazuri hapa duniani. Pia atawa adhibu wale waliofanya maovu katika dunia hii.
Mtazamo wa Uislamu kwa mujibu wa shia juu ya hoja hiyo ni kwamba binadamu hana ule uhuru kama watu wanavyodhani, uhuru usio na mipaka kiasi kwamba akafanya mambo kinyume na ule utaratibu ulio wekwa na Mwenyezi Mungu (swt).
Kama watu watakubali kwamba binadamu anao uhuru usio na mipaka basi hiyo itakuwa na maana kwamba Mwenyezi Mungu atakuwa anafarikiana na viumbe vyake hali si kweli hiyo siyo sifa yake Mwenyezi Mungu kwamba ashindane na viumbe vyake. Wakati huo huo ni vizuri ieleweke kwamba mwanadamu sio mfungwa kiasi akashindwa kutumia uhuru na uwezo aliopewa katika mambo yanayomkabili (maisha yake); mwanadamu hayupo kama mnyama ambaye anatawaliwa na hulka.
Qur’an tukufu inasema wazi kwamba Mwenyezi Mungu amemuonyesha mwanadamu njia ya uongofu lakini hakumlazimisha kuifuata njia hiyo wala hakumlazimisha kuingia katika upotevu tazama Qur’an (76:3).
ۚ إِنَّا هَدَيْنَاهُ السَّبِيلَ إِمَّا شَاكِرًا وَإِمَّا كَفُورًا
“Hakika Sisi tumembainishia Njia. Ama ni mwenye kushukuru, au mwenye kukufuru”.

 

Share this article

Comments 0

Your comment

Comment description

Latest Post

Most Reviews

MOST READ